HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 21, 2020

JKT Yatangaza Nafasi Vijana wa Kujitolea

Mkuu wa  Tawi  la Utawala Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Kanali  Julius Kadawi akisisitiza kuhusu nafasi zilizotolewa kwa vijana wanaopenda kujiunga na Jeshi hilo kwa kujitolea kwa mwaka 2020, hayo yemejiri leo Agosti 20, 2020 Makao Makuu ya Jeshi hilo Chamwino mkoani Dodoma. 
(Picha na MAELEZO)

Na Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma

Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) latangaza nafasi  za kujiunga na mafunzo ya Jeshi hilo kwa kujitolea mwaka 2020.

Hayo yamesemwa leo Agosti 20 Makao Makuu ya Jeshi hilo, Chamwino mkoani Dodoma na Mkuu wa Tawi la Utawala wa Jeshi hilo, Kanali Julius Kadawi ambapo amesema kuwa, Mkuu wa Jeshi hilo Meja Jenerali Charles Mbuge anawatangazia vijana wote wa Tanzania Bara na Visiwani nafasi za kujiunga na mafunzo hayo ili waweze kujengewa stadi za kuweza kujiajiri na kuwa wazalendo.

“Jeshi la Kujenga Taifa linapenda kuwaarifu vijana watakaopata fursa hiyo kuwa halitoi ajira kwa vijana, pia halihusiki kuwatafutia vijana ajira katika asasi, vyombo vya ulinzi na usalama na mashirika mbalimbali ya Serikali na yasiyo ya Kiserikali”, alisisitiza Kanali Kadawi.

Aliongeza kuwa uratibu wa vijana kuomba na hatimaye kuchaguliwa kujiunga na mafunzo hayo, unaratibiwa na Ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya ambako mwombaji anaishi.

Akifafanua amesema kuwa Jeshi hilo linatoa mafunzo ambayo yatawasaidia vijana kujiajiri wenyewe mara baada ya kumaliza mkataba wao na JKT.

“Kutokana na ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID- 19), tahadhari za kuzuia maambukizi ya ugonjwa huo kama zilivyoelekezwa na Serikali kupitia Wizara ya Afya zitazingatiwa kwa kipindi chote vijana watakapokuwa katika mafunzo,” alisisitiza Kanali Kadawi.

Aidha, alibainisha  kuwa Meja Jenerali Charles Mbuge anawaalika vijana wote watakaopata fursa hiyo kwenda kujifunza uzalendo, ukakamavu, stadi za kazi, stadi za maisha na pia kuwa  tayari kulilinda na kulitumikia Taifa.

Baadhi ya sifa za vijna wanaotakiwa ni pamoja na; kuwa raia wa Tanzania, awe na afya njema, mwenye nidhamu na tabia nzuri na hajawahi kupatikana na hatia Mahakamani na hajawahi kufungwa, asiwe ametumikia Jeshi la Magereza, Polisi, KMKM, Chuo cha Mafunzo, wala kuajiriwa na idara nyingine Serikalini.

Kigezo kingine asiwe amepitia JKT katika operesheni za nyuma, asiwe amejihusisha na matumizi ya dawa za kulevya.Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) limekuwa likiwaandaa vijana kujiajiri kwa kuwajengea stadi za maisha na kuwawezesha kuwa wazalendo, waadilifu na walio tayari kulilinda Taifa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad