Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo
Bw.Gerald Kusaya akiongea na watumishi wa Bodi ya Mkonge Tanzania leo
alipofanya ziara ya kikazi jijini Tanga kufanya ufuatiliaji wa maagizo
ya Waziri Mkuu.
Katibu Mkuu Wizara ya
Kilimo akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji wa Bodi ya Mkonge
Tanzania na wanahabari leo alipotembelea makao makuu ya Bodi hiyo Jijini
Tanga.
Picha na habari na Wizara ya Kilimo.
Serikali imefanikiwa kutoa
shilingi Bilioni Tatu katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kuongeza
utafiti na uzalishaji wa mbegu bora za mkonge zitakazo gawiwa kwa
wakulima kwenye mikoa 17 inayolima zao la mkonge nchini.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo Bw. Gerald Kusaya ametoa kauli leo
akiwa ziarani Mkoa wa Tanga kufanya ufuatiliaji wa maagizo ya Waziri
Mkuu aliyoyatoa mwezi Juni mwaka huu.
”Serikali ya Awamu ya Tano tayari imekipatia kituo cha Utafiti
TARI Mlingano Bilioni 3 za kukiwezesha kuongeza utafiti na uzalishaji
mbegu bora zenye kutoa mavuno mengi ambazo zitagawiwa kwa wakulima wa
mkonge nchini” amesema Kusaya
Kusaya alisema lengo la Wizara ya
Kilimo ni kuona kituo cha Utafiti TARI Mlingano kinazalisha mbegu bora
Milioni Tano mwaka huu 2020/21 ili zigawiwe kwa wakulima waongeze uzalishaji wa mkonge toka tani 36,000 za sasa kufikia lengo la tani 120,000 kwa mwaka ifikapo mwaka 2025.
Ili kufikia lengo hilo la
uzalishaji mbegu bora za mkonge Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti TARI
Mlingano Dkt.Beatrice Senkoro alimweleza Katibu Mkuu kuwa wameanza
kutekeleza kwa kuongeza eneo linalolimwa mbegu toka hekta 2 za sasa hadi
hekta 65 .
”Jumla ya hekta 65 zimelimwa
ambapo kati yake hekta 15 zimepandwa miche ya mkonge ipatayo milioni
moja na laki Tano kufikia mwezi huu Agosti mwaka huu” alisema Dkt.Senkoro.
Dkt.Senkoro ameiomba Wizara
kuendelea kukiwezesha kituo hicho kuwa na maabara ya kisasa ili kiweze
kuongeza kasi ya Utafiti wa mbegu bora za mkonge kwa njia ya "
Tissue Culture Laboratory" inayotoa matokeo mazuri na mbegu
nyingi.
Aliongeza kusema mahitaji ya mbegu bora za mkonge kwa wakulima
wadogo nchini kwenye mikoa yote 17 inayolima yamefikia Milioni Moja na
Laki Mbili wakati lengo la Wizara ni kuzalisha mbegu bora Milioni Tano
kwa mwaka.
Dkt.Senkoro alitaja pia mafanikio ya Kituo cha TARI Mlingano ni
pamoja na kuwafundisha kanuni bora za kilimo cha mkonge kwa Maafisa
Ugani 427 na pia kimetoa mafunzo kwa wakulima 22,000 wakati wa Maonesho
ya Kilimo Nanenane mkoani Simiyu ikishirikiana na Bodi ya Mkonge Tanzania.
Katika hatua nyingine Katibu Mkuu Kusaya ameitaka Menejimenti ya
Bodi ya Mkonge ( TSB) kufanya sensa ya wakulima wa mkonge na kiasi cha
eneo wanalolima ili mashamba yasiyolimwa Wizara ishauri serikali
kuyatwaa na kuwapa wawekezaji wenye uwezo.
Kusaya ameelekeza pia Bodi hiyo ya
Mkonge kusimamia zoezi malipo ya wakulima wa majani ya mkonge wanaodai
kutolipwa na AMCOS na pia kudhibiti vitendo vya baadhi ya wakulima
kuvuna mkonge usiokomaa na kuharibu ubora unatotakiwa .Katibu Mkuu katika ziara hiyo
ameipongeza Bodi ya Mkonge kwa kutekeleza agizo la Waziri Mkuu la
kuhamia kwenye jengo lao la Mkonge House jijini Tanga.
” Nimefurahi leo kuona Bodi
imehamia kwenye jengo hili la Mkonge House kama alivyoagiza Waziri
Mkuu,sasa nataka mfanye kazi kubwa kusimamia uongezaji uzalishaji wa mkonge kwa wakulima zaidi kuhamasishwa kulima ili
ardhi yote iliyokusudiwa kupandwa mkonge ilimwe”alisisitiza Kusaya
Katika hatua nyingine Kusaya
alisema tayari serikali imetoa shilingi Milioni 400 kwa ajili ya
ukarabati wa jengo la Ofisi ya Bodi hiyo ili liwe bora baada ya
kutwaliwa kutoka kwa mwananchi aliyemilikishwa kinyume na utaratibu.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa
Bodi ya Mkonge Tanzania Saad Kambona alisema tayari kazi ya usajili wa
wakulima wa mkonge imeanza na kuwa wakulima 7,551 wadogo wa mkonge wamesajiliwa kwenye mkoa Tanga ,Kilimanjaro na Morogoro.
Kambona amesema Bodi yake itaendelea kuhamasisha na kuelimisha
wakulima wengi kuanzisha mashamba mapya ya mkonge na kupanda mbegu bora
ili uzalishaji uweze kukua zaidi.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo huyo ametembelea pia kiwanda cha kuzalisha mbolea cha ABM Tanga kukagua uzalishaji wa mbolea.
No comments:
Post a Comment