Wananchi
wameshauriwa kujenga tabia ya kupima afya zao mara kwa mara kwa kufanya hivyo
watatambua kama wana maradhi au la na kama wana maradhi wataweza kupata huduma za matibabu kwa wakati.
Pia wameombwa kuwa na
bima ya afya ambazo zitawasaidia kupata matibabu pindi watakapouguwa kwani maradhi huja muda wowote, wakati wowote
na mahala popote bila ya kupiga hodi.
Rai hiyo imetolewa hivi
karibuni na aliyekuwa Mbunge wa Nzega Mhe. Lucas Lumambo Selelii
aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa kusimamisha moyo na kupandikiza mshipa wa damu
kwenye moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Akizungumza kwa
furaha na mwandishi wa habari hii Mhe. Selelii alisema huduma za matibabu ya
moyo ya kibingwa ambayo hapo awali yalikuwa yakipatikana nje ya nchi sasa
yanapatikana hapa nchini kwa kiwango cha juu kupitia madaktari wabobezi na
wataalam wa upasuaji wa moyo.
“Matibabu niliyoyapata
pamoja na mengine yanatotolewa katika Taasisi hii yanatokana
na jitihada zilizofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kwa kuwekeza vifaa tiba vya matibabu ya kibingwa ya magonjwa ya moyo ili
kuwawezesha wananchi wa matabaka yote kupata huduma hapa nchini.
Mhe. Selelii alisema
kabla ya kufanyiwa upasuaji huo alianza kusikia moyo unapata vichomi maumivu
ambayo yalikuwa yakienda hadi mgongoni, ni ugonjwa ambao hakuwahi kuugua katika maisha yake.
“Nilikuja Dar es Salaam
kwa ajili ya mambo yangu binafsi lakini ghafla nikiwa hotelini usiku ndio
nikaanza kupata maumivu ambayo yalinifanya niamke asubuhi na mapema kwenda hospitali
kwa ajili ya matibabu,”
“Vipimo vya awali
vilionesha nina shinikizo la juu la damu la 170 kwa 120, na kushauriwa nitumie
dawa za presha, baada ya kuwasiliana na ndugu na jamaa kuhusu hali niliyokutwa
nayo walinishauri nifike hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa ajili ya
uchunguzi zaidi,” alisema Mhe Selelii.
Baada ya kufanyiwa
vipimo katika hospitali ya Muhimbili ilionekana kuwa na viashiria vya magonjwa
ya moyo hivyo kufikishwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili
ya vipimo zaidi na matibabu.
“Kwakuwa sijawahi
kuugua toka kuzaliwa kwangu, sikuwahi kukata bima ya afya, hivyo nilivyoambiwa
nina tatizo la moyo niende JKCI niliwakatalia na kuwaambia sina hela wala bima
ya afya, nashukuru wahudumu wa afya walinishawishi na kuniambia hela hutafutwa lakini
maisha huwezi kuyatafuta mara ya pili hivyo ni vyema kufanyiwa uchunguzi wa
kina ili ijulikane unanatizo gani,”
“Nimefurahia kwa huduma
ya upasuaji wa moyo niliyoipata hapa JKCI maana waliniandaa na kuniambia kila
kitu nitakachofanyiwa katika upasuaji huo na hivyo kunifanya kuwa tayari
kufanyiwa upasuaji bila uoga wowote”, alizungumza kwa furaha Mhe. Selelii.
Kwa upande wake daktari
bingwa wa upasuaji wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Evarist Nyawawa alisema walimpokea Mhe. Selelii
akiwa na matatizo ya kushindwa kupumua na kuishiwa nguvu, ambapo baada ya
vipimo ilionekana mishipa mitatu ya damu inayopeleka damu katika misuli ya moyo
kuziba.
“Upasuaji tuliomfanyia
ni wa kuvuna mishipa ya damu kutoka katika miguu na kuipandikiza kwenye moyo, upasuaji huu umechukua masaa matano na
baada kufanikisha matibabu hayo mgonjwa tulimuhamishia katika chumba cha
uangalizi maalum (ICU) baada ya hali yake kuimarika alipelekwa wodini na
anaweza kuruhusiwa siku yoyote kuanzia sasa”, alisema Dkt. Nyawawa.
Upasuaji uliofanyika ni
wa kuvuna mshipa mkubwa wa damu kutoka kwenye mguu na ndani ya kifua na kuipandikiza juu ya mishipa ya damu ya moyo iliyokuwa imeziba ili
kuifanya damu iweze kupita vizuri (Coronary
Artery Bypass Grafting -CABG).
Picha na JKCI
No comments:
Post a Comment