Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dkt. Simon Chacha akichimba Msingi kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma inayojengwa kwenye Kata ya Mahembe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Pendo Mangalia (mbele) akishiri kuchimba msingi kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya katika Kata ya Mahembe.
Wakazi wa Kata ya Mahembe wakishiriki kuchimba msingi kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Pendo
Mangalia (Katikati) akiongozana na wakazi wa kata ya Mahembe kuelekea eneo la
ujenzi wa Hospitali ya Wilaya.
Mwandishi Wetu,
Serikali imeanza Ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya
Kigoma ili kukabiliana na changamoto ya wananchi wa Wilaya hiyo ya kutembea
umbali mrefu kutafuta huduma za Afya.
Katika kuhakikisha matokeo chanya, Wananchi wa Kata ya Mahembe
inapojengwa Hospitali hiyo, wamejitokeza kuchangia nguvu zao katika shughuli ya
Uchimbaji wa Msingi wa Jengo ambalo baada ya kukamilika kwake
litawaondolea adha ya kutembea takribani Kilometa nane kufuata huduma za Afya.
Akizungumza wakati wa kuanza kwa ujenzi wa Msingi wa Hospitali
hiyo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Dkt. SIMON CHACHA amesema mradi huo
utagharimu shilingi bilioni moja na milioni mia tano hadi kukamilika
kwake.
Dkt. Chacha amesema ujenzi wa Hospitali hiyo umepangwa
kukamilika mwishoni mwa mwezi Septemba mwaka huu.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi wa
Mahembe wameishukuru Serikali kwa kuwapelekea maendeleo hatua ambayo haikuwahi
kufikiwa kwa miaka mingi iliyopita.
"Muda tuliokuwa tukiutumia kwenda umbali mrefu kutafuta
tiba au kupeleka huduma mbali, tutautumia kuendeleza shughuli zetu za
kiuchumi" walisema.
Aidha, wameipongeza Serikali kwa kufikia Uchumi wa kati kabla ya
muda uliopangwa huku wakionesha matumaini makubwa ya maendeleo ndani ya kipindi
cha miaka mitano ijayo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Pendo
Mangalia amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma
katika maeneo ya karibu na kuwaondoa na adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta
huduma.
Amesema wananchi wamehamasika na kuchangia nguvu zao kuhakikisha
maendeleo yanapatikana.
Kukamilika kwa ujenzi wa hospitalii hiyo katika eneo la
Mahembe kunafanya kuwa na Hospitali Tano za Wilaya Mkoani Kigoma.
No comments:
Post a Comment