HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, July 8, 2020

Mfumuko wa Bei Mwezi Juni Waendelea kuwa Asilimia 3.2


Mfumuko wa bei wa Taifa kwa  mwezi Juni 2020 umeendelea kuwa asilimia 3.2 kama ilivyokuwa mwezi  Mei, 2020.
Akizungumza leo Julai 8, 2020 Jijini Dodoma,  Kaimu Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Bi. Ruth Minja amesema kuwa hali hiyo inamaanisha kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka unaoishia mwezi Juni umebaki kuwa sawa na iliyokuwepo kwa mwezi Mei.

Akifafanua, Bi Minja amesema kuwa baadhi ya bidhaa za vyakula zilipungua bei kwa mwezi Juni 2020 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2019, baadhi ya bidhaa hizo ni pamoja unga wa mahindi kwa asilimia 1.6, matunda kwa asilimia 2.1, viazi mviringo asilimia 0.5 na mihogo asilimia 13.3.

Kwa upande wa bidhaa zisizo za vyakula amesema kuwa ziliongezeka bei kwa mwezi Juni, 2020 ikilinganishwa na bei za mwezi Juni 2019, bidhaa hizo ni pamoja na mavazi kwa asilimia 2.7, gesi ya kupikia kwa asilimia 7.8 , mkaa asilimia 11.2, samani asilimia 2.7 na vitabu vya shule kwa asilimia 1.5.

Mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umepungua hadi asilimia 3.8 kutoka asilimia 4.4 kwa mwaka unaoishia mwezi Mei, 2020.

Kwa upande wa nchi ya Kenya Bi Minja amesema kuwa Mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umepungua hadi kufikia asilimia 4.59 kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2020. Kwa upande wa Uganda, Mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2020 umeongezeka hadi asilimia 4.1 kutoka asilimia 2.8 kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2020.
 Kaimu Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii  Bi. Ruth  Minja  akieleza kwa waandishi leo Julai 8, 2020 wa habari  kuhusu  mfumuko wa Bei kwa mwezi June 2020 ambao umeendelea kuwa asilimia 3.2 kama ilivyokuwa mwezi Mei, 2020.
Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia mkutano wa kutangaza mfumuko wa bei kwa mwezi June, 2020 Jijini Dodoma leo  Julai 8, 2020.
(Picha zote na NBS)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad