HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, July 21, 2020

HESLB yaanza kupokea maombi ya mikopo kwa 2020-2021, bajeti mwaka huu yaongezeka

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) Dkt. Abdul-Razaq Badru (katikati) akizungumza na waandishi wa vyombo vya Habari kuhusu kufunguliwa kwa dirisha la msimu wa masomo kwa mwaka 2020/21. Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano HESLB, Omega Ngole.

TZS 464 bilioni zatengwa kwa wanufaika 145,000

Na Ismail Ngayonga - HESLB (0717 084252),
BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) leo (Jumanne, Julai 21, 2020) imetangaza kuanza kupokea maombi ya mikopo kwa njia ya mtandao kwa mwaka wa masomo 2020/2021 kuanzia leo hadi Agosti 31, 2020.

Akizungumza na wanahabari katika ofisi za HESLB zilizopo eneo la TAZARA jijini Dar es salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru amesema waombaji wote wa mkopo wanashauriwa kusoma na kuuzingatia ‘Mwongozo wa Utoaji Mikopo kwa 2020-2021’ unaopatikana katika tovuti ya HESLB (www.heslb.go.tz).

“Mwombaji anaweza kuingia kwenye mfumo wetu kupitia tovuti yetu ambayo ni www.heslb.go.tz na atapata maelekezo ya kutosha ya kuingia katika mfumo wa OLAS – Online Loan Application System,” amesema Badru.



Kuhusu bajeti ya fedha za mikopo, Badru amesema Serikali imetenga TZS 464 bilioni kwa mwaka 2020/2021 ambazo zinatarajia kuwanufaisha jumla ya wanafunzi 145,000. Kati yao 54,000, watakua ni mwaka wa kwanza na wengine 91,000 ni wanaoendelea na masomo.

Bajeti ya mikopo kwa 2020-2021
“Bajeti hii ya TZS 464 bilioni kwa 2020/2021 imeongezeka kutoka TZS 450 bilioni mwaka 2019/2020 ambazo zinawanufaisha jumla ya wanafunzi 132,119,” amesema Badru wakati akifafanua swali la mwanahabari aliyetaka kujua iwapo kuna ongezeko la bajeti.

Katika mkutano huo, Badru pia amezungumzia wanafunzi wahitaji wa mkopo waliomaliza kidato cha sita na wanatarajia kujiunga kambi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kusema utaratibu wa kuwafikia unaandaliwa.

“Tunafahamu kuwa kuna wanafunzi waliomaliza kidato cha sita wanaotarajia kujiunga na kambi 18 za Jeshi la Kujenga Taifa kuanzia mwezi Agosti, 2020, tunakamilisha utaratibu kwa kushauriana na Makao Makuu ya JKT ili kuwawezesha kuwezeshwa wakati huo,” amesema.

Malipo ya robo ya nne ya fedha za chakula na malazi
Akitoa ufafanuzi kuhusu malipo ya robo ya nne ya fedha za chakula na malazi kwa wanafunzi waliopo vyuoni hivi sasa, Badru amesema HESLB inakamilisha malipo hayo kwa wanafunzi 132,119 ambao wananufaika hivi sasa.

“Tumeanza kulipa na tunakamilisha malipo hayo ambayo hulipwa kwa mwanafunzi mnufaika moja kwa moja ili kumuwezesha kumudu gharama za chakula na malazi katika siku zote anazokuwa chuoni kama tunavyoelezwa na chuo husika,” amesema Badru na kuongeza:

“Ufafanuzi huu tunautoa kwa kuwa tumepokea maoni kuwa baadhi ya wateja wetu ambao ni wanafunzi hawajaelewa vizuri utaratibu huu wa malipo haya na ada za mafunzo ambazo hulipwa mara mbili kwa mwaka,” amefafanua.

Mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa kuomba
Akizungumza katika mkutano huo, Afisa Mikopo Mwandamizi wa HESLB Josephat Bwathondi amewakumbusha waombaji kuhakikisha wanafuata maelekezo ikiwemo kutumia namba moja ya kidato cha nne katika kuomba mkopo na kuomba udahili chuoni.

Kwa mujibu wa Bwathondi, uzoefu wa uchambuzi wa maombi ya mikopo umeonesha kuwa baadhi ya waombaji hukosea kwa kuambatisha nyaraka zisizotambulika na hivyo kukosa mkopo na kushindwa kutimiza ndoto zao.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad