HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 17, 2020

Tayoa yaendesha mdahalo na wanafunzi kwa Tehama

Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Vijana Nchini (Tayoa) kwa ufadhili wa Wizara ya Afya kupitia mradi wa Global Fund, limefanya mdahalo wa kwanza kupitia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) ambapo zaidi ya wanafunzi na viongozi wapatao 680 wameshiriki.

Mdahalo huo wa Timiza Malengo 2020 ulifanyika kwa njia ya mtandao wa Zoom ulishirikisha wanafunzi 680 na wakuu wa vitivo 40 kutoka taasisi 32 za elimu ya juu  nchini uliandaliwa na Tayoa kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto na NACP.

Wengine walishirikiana na Tayoa kufanikisha mdahalo huo  wenye lengo la kuwafanya vijana kutimiza ndoto zao kwa kujilinda dhidi ya maambukizi yaa VVU ni Kampuni ya Vodacom, Tigo, Zantel, Halotel, Airtel, TTCL, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Shirika la Afya na Utafiti Afrika (AMREF).

Mkurugenzi wa Tayoa, Peter Masika alisema kufanikiwa kwa mdahalo huo kwa njia ya Zoom ni ushahidi tosha kwamba kama nchi itawekeza kwenye matumizi ya Tehama italeta mabadiliko na maendeleo ya haraka kwani wanafunzi wengi walioshiriki  walikuwa vyuoni na mikoani.

Alisema tayoa inaendesha kampeni ya Timiza Malengo 2020 ili kuhamasisha vijana na wanafunzi kuwa na malengo yao na kuyatekeleza nia ikiwa ni kujenga tabia kwa vijana na wanafunzi ya kujitafutia maarifa na stadi mbalimbali.

Masika alisema Tayoa imepanga kuwa na midahalo ya Timiza Malengo kila mwezi ili kuwajenga zaidi vijana kiafya nan a kuwa wajasiriamali watakaotengeneza ajira mpya na kulipa kodi ili jamii iweze kupata maendeleo endelevu.

Masika alisema Tayoa imeshuhudia ongezeko la watu wanaotuhumia huduma za 117 lakini wasichana wengi hawajahamasika kutumia huduma hizo ambazo hutolewa bila malipo ili kuwapa fursa wengi kupata msaada.

“Kwa mfano kila siku zaidi ya watu 10,000 hupiga simu kutafuta taarifa sahihi za afya na ushauri nasaha lakini wasichana ni asilimia 30 tu, hivyo tunawashauri wasichana wajitokeze kwa wingi nao kupiga simu ambapo wataelimishwa kuhusu mambo mbalimbali,” alisema Masika

Akizungumza kwenye mdahalo huo, Jeremia Mushi kutoka Mpango wa Taifa wa Kupambana na Ukimwi (NACP), aliwataka watanzania hususani vijana kuwa makini wasipate maambukizi ya virusi vinavyosababisha ugonjwa wa ukimwi (VVU) kwani takwimu zinaonyesha kuwa kila dakika moja watanzania wanne wanapata maambukizi mapya.

Mushi alisema hadi sasa watanzania milioni 1.7 wamethibitika kuwa na maambukizi ya VVU na asilimia 95 ya hao wanatumia dawa za kufubaza virusi hivyo huku kila mwaka watu 72,000 wakipata maambukizi mapya.

Alisema takwimu zinaonyesha kuwa kila mwezi watu 6,000 hupata maambukizi mapya wakati kwa siku watu 200 hupata maambukizi hayo na wanne hupata maambukizi hayo kila dakika moja.

Naye Eda Charles kutoka NACP alisema wasichana wengi wanajikuta wakipata ujauzito na wengine kushindwa kutimiza ndoto zao kutokana na mazingira magumu yanayowakabili wanapokuwa shuleni kwani wengi wao hulazimika kutembea umbali mrefu kufika shuleni.

“Wasichana wanakosa mahitaji muhimu sasa watu wazima wanaowatamani  hutumia mwanya wa changamoto zinazowakabili kuwapata na mwisho wa siku wanaweza kuambukizwa VVU au kupata mimba wasizotarajia na kukatisha ndoto zao” alisema Eda

Mratibu wa UMATI, Fredi Turuka alisema vijana wengi wamekuwa wakiogopa zaidi kupata mimba lakini wanadharau kuvaa kinga wakati wa kujamiiana jambo ambalo limekuwa likichangia kuongezeka kwa maambukizi mapya.

“Wakati wanapofanya mapenzi wanazingatia sana kutopata mimba kuliko Ukimwi wamekuwa wakisema kuwa hawasikii radha ya tendo sasa hali hii ndiyo imesababisha kundi la vijana kuwa kwenye hatari zaidi ya kupata maambukizi mapya ya VVU,” alisema Turuka

Amesema jamii inawajibu wa kuwalinda vijana wafikie ndoto zao ili kufikia maendeleo na wenyewe wanawajibika kujilinda kwa kuhakikisha wanafanya ngono salama na kwa wakati unaokubalika.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad