HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, May 20, 2020

Benki ya CRDB yaikabidhi BAKWATA milioni 10 kusaidia mapambano dhidi ya Corona

Meneja Mwandamizi wa Mawasiliano na Mahusiano wa Benki ya CRDB, Emmanuel Kiondo (kushoto) akimkabidhi Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA), Nuhu Jabir Mruma, mfano wa hundi yenye thamani wa Sh. Milioni 10, zitakazoenda kusaidia kununua vifaa vya mapambano dhidi ya ugonjwa wa Korona katika maeneo ya ibada nchini. Makabidhiano hayo yamefanyika leo Mei 20, 2020 kwenye makao makuu ya Benki hiyo, jijini Dar es salaam.

==     ===   ==
Benki ya CRDB imekabidhi mchango wa shilingi milioni 10 kwa Baraza la Waislam Tanzania (BAKWATA) kusaidia mapambano dhidi ya corona. Akizungumza katika hafla hiyo fupi ya makabidhiano, Meneja mwandamizi wa Iadara ya Mawasiliano kwa Umma wa Benki ya CRDB, Emmanuel Kiondo alisema Benki hiyo ikiwa sehemu ya jamii imekuwa ikishirikiana na Serikali na jamii kwa ujumla katika mapambano dhidi ya corona ikiwamo ni pamoja na kusaidia uboreshwaji wa miundombinu ya afya na upatikanaji wa vifaa kinga.

“Tunatambua kuwa ili kuweza kuushinda ugonjwa huu wa corona tunahitaji kushirikiana kwa pamoja kama jamii, ni imani yetu kuwa mchango huu utakwenda kusaidia kuweka mazingira salama katika sehemu zetu za ibada,” alisema Kiondo huku akibainisha kuwa Benki hiyo tayari imeshatoa mchango wa zaidi ya shilingi milioni 290 kwa Serikali na wadau wengine katika kusaidia mapambano dhidi ya virusi vya corona.

Benki ya CRDB imetoa mchango huo wakati ambao Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amekua akisisitiza umuhimu wa kuliombea Taifa wakati huu huku tahadhari zikiendelea kuchukuliwa. “Sote tunafahamu Ramadhan ni wakati wa kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu kupitia ibada na kutoa zaka na sadaka kwa wingi, tuyafanye hayo yote tukimuomba Mungu atuvushe katika janga hili” alisema Kiondo.
Meneja Mwandamizi wa Mawasiliano na Mahusiano wa Benki ya CRDB, Emmanuel Kiondo akizungumza na waandishi wa habari wakati wa makabidhiano hayo.

Pamoja na msaada huo wa shilingi milioni 10 uliotolewa leo, Kiondo alisema katika Ramadhan ya mwaka huu 2020, Benki ya CRDB imetoa msaada wa futari wenye thamani ya shilingi milioni 55 kusaidia kununua futari kwa vituo 95 katika mikoa yote nchini.

“Katika kipindi hiki cha mwezi Mtukufu ambapo mioyo na fikra vipo katika kumnyenyekea Muumba tumeona ni jambo la faraja kujumuika kwa pamoja na watoto yatima nchini kote katika ibada hii ya funga kwa kuwapatia futari,” aliongeza Kiondo.

Naye Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA), Sheik Nuhu Jabir Mruma ameishukuru Benki ya CRDB kwa msaada huo ambao amesema utasaidia kwenda kuongeza usalama wa sehemu za ibada katika kipindi hiki ambacho Serikali na taasisi nyengine zinapambana kuweka mazingira salama yakujilinda na kusambaa kwa ugonjwa wa corona.
Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA), Nuhu Jabir Mruma akizungumza wakati akitoa shukrani kwa Benki ya CRDB kwa msaada huo.

“Msaada huu tutauelekeza katika kununua vifaa kama barakoa, vitakasa mkono, pamoja na kuweka miundo mbinu ya maji na sabuni ili kuweka mazingira salama kwa watu wanaohudhuria ibada,” alisema Sheikh Mruma.

Sheikh Mruma pia aliipongeza Benki ya CRDB kwa msaada wa futari ulioutoa kwa vituo vya watima nchi nzima, huku akitanabaisha kuwa msaada huo wa futari ni ibada na unafungua milango ya baraka kwa Benki ya CRDB.

“Mafundisho ya Mtume SAW tunafundishwa atakayemfuturisha aliye na swaum atapata thawabu kama zake bila ya mwenye swaum kupungukiwa na kitu. Kwa niaba ya BAKWATA niwashukuru sana na Mwenyezi Mungu aendelee kuibariki Benki yetu ya CRDB,” alimalizia Sheikh Mruma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad