HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, March 9, 2020

NMB yafungua tawi la 225 ikiahidi neema kwa wakulima, wafugaji

Benki ya NMB imezindua tawi jipya Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu na kufikisha matawi 225 nchi nzima huku ikitangaza neema ya huduma bora na mikopo nafuu kwa wananchi wakiwemo wakulima, wafugaji na wavuvi kusaidia shughuli za kiuchumi.

Akitoa taarifa ya utendaji wa benki hiyo kwa Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa hafla ya ufunguzi wa tawi hilo mwishoni mwa wiki, Kaimu Mkurugenzi mtendaji wa NMB, Ruth Zaipuna alisema ufunguzi wa tawi hilo pamoja na mengine maeneo ya vijijini ni utekelezaji sera huduma jumuishi ya kifedha kwa makundi yote ya kijamii hadi vijijini.

Alitaja baadhi ya huduma jumuishi zinazotolewa na benki hiyo hadi katika ngazi ya wilaya, kata na vijiji kupitia mawakala kuwa ni pamoja na mikopo ya mitaji kwa wafanyabiashara wadogo, kati na wakubwa, pembejeo kwa wakulima na aina zote za bima kuanzia ya afya, vyombo vya usafirishaji na ujenzi wa nyumba bora.

Alisema pamoja na huduma za kibenki ikiwemo mikopo yenye riba nafuu, NMB pia inatoa huduma ya aina zote za bima, malipo kwa njia ya mtandao na elimu ya usimamizi wa fedha kwa wakulima kupitia vyama vyao vya msingi vya ushirika (Amcos) kupitia NMB Foundation.

“NMB imetoa mikopo kwa Amcos 202 kati ya 383 za mkoa wa Simiyu,” alisema Zaipuna.

Alisema kupitia huduma ya NMB Mkononi, wateja wa benki hiyo wataweza kufungua akaunti kupitia simu zao za kiganjani bila kulazimika kwenda benki na kuwaomba wananchi walioko maeneo ambako hakuna matawi ya benki kuchangamkia fursa.

Akizindua tawi hilo, Makamu wa Rais Mhe. Samia Hassan Suluhu alisema uimara na huduma ya sekta ya fedha ni mhimili muhimu katika katika maendeleo na uchumi wa Taifa na kuzitaka mabenki na taasisi za fedha kuimarisha shughuli zao huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira bora na wezeshi kuendeleza sekta hiyo.

Aliipongeza Benki ya NMB kwa uendeshaji mzuri unaoiwezesha kupata faida na hivyo kuiwezesha Serikali kuvuna zaidi ya shilingi bilioni 586 kupitia kodi na ushuru mbalimbali.

Makamu wa Rais pia aliishukuru NMB kwa kutenga na kutumia zaidi ya shilingi bilioni 5 kugharamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kupitia sera ya kurejesha sehemu ya faida kwa jamii.

#NMBBankKaribuYako
 Uzinduzi Rasmi: Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan (wapili kulia), akikata utepe kuzindua tawi la 225 la benki ya NMB lililopo Busega mkoani Simiyu akiwa pamoja na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Ashatu Kijaji( watatu kulia),  Mbunge wa Busega, Raphael Chegeni na Kaimu Mkurugenzi wa benki hiyo Ruth Zaipuna (pili kushoto). Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka. Kabla ya tawi hili la NMB Busega kuzinduliwa, wananchi walilazimika kusafiri hadi Magu takribani kilomita Zaidi ya 30 kupata huduma za kibenki.
 Uzinduzi Rasmi:  Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, akipata maelezo kutoka kwa meneja wa tawi la Magu Stanley Betty kuhusu huduma za kibenki za kisasa wananchi watakazo pata kupitia tawi jipya la benki ya NMB lililopo Busega mkoani Simiyu ambalo ni la 225 nchini. Kabla ya tawi hili la NMB Busega wananchi walilazimika kusafiri hadi Magu takribani kilomita Zaidi ya 30 kupata huduma za kibenki. 
  Salaam bila kupeana mikono: Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan (kushoto) akisalimiana na Mjumbe wa Bodi ya NMB Mathias Magwanya (wa nne kulia) akiwa ameambatana na Kaimu Mkurugenzi wa benki hiyo Ruth Zaipuna pamoja na wafanyakazi wengine wa Benki hiyo. Kabla ya tawi hili la NMB Busega kuzinduliwa, wananchi walilazimika kusafiri hadi Magu takribani kilomita Zaidi ya 30 kupata huduma za kibenki. 
 Kaimu Mkurugenzi wa NMB Ruth Zaipuna, akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa tawi la Busega Mkoani Simiyu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad