HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, February 14, 2020

MAMLAKA ZA MAJI ZITUMIE WATAALAMU KUTOKA NDANI ILI KUPUNGUZA GHARAMA

Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa akizungunza na watendaji wa maji kutoka Mamlaka za  DAWASA na RUWASA wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji ndani ya Mji wa Kisarawe.


Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
Mamlaka za maji nchini zimetakiwa kuanza kutumia wataalamu wa ndani katika ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa amesema sasa hivi mamlaka zote zinatakiwa zianze kutumia wataalamu kutoka ndani ili zipunguze gharama za ujenzi.

Amesema hayo wakati wa kutembelea miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam na Pwani (DAWASA) katika mkoa wa Kihuduma wa Kisarawe.

Mbarawa amesema kutokana na gharama kubwa za wakandarasi wakati wa ujenzi wa miradi mbalimbali ya maji haina budi kwa sasa kuanza kuwatumia watalaamu wa ndani zaidi kwani wanauwezo mzuri.

Amesema, jitihada kubwa zimefanywa na Dawasa katika kukamilisha mradi huo wa Kisarawe wenye thamani ya Bilioni 10.6 kwa kutumia mapato yao ya ndani ya kila mwezi.

"Nawapongeza Dawasa, wamekamilisha mradi huu kwa asilimia 100 kwa fedha zao za ndani kwani wakati tunaingia wizarani tulitoa maagizo kuwa Mamlaka zote nchini zinatakiwa kukusanya mapato yao na kujenga miradi," amesema Mbarawa.

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi wa Dawasa Lastone Msongola amesema wamekamilisha mradi wa Kisarawe kama maagizo ya Rais wa Jamhuri ga Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli alivyoagiza wakati wa uzinduzi wa mradi wa chanzo cha Maji Ruvu Juu.

Afisa Mtendaji Mkuu Wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema, kutoka kuanza kwa mradi huo wameweza kuwaunganishia wananchi wengi na bado maombi yanaendelea kuja katika ofisi zao.

Ameeleza kuwa, katika makusanyo ya mwezi mmoja wameweza kukusanya milioni 8 ambapo mwezi  Uliopita wamekusanya milioni 15 na amemuagiza Meneja wa Dawasa Mkoa wa Kihuduma Mkuranga kuhakikisha wanaongeza makusanyo na kufikia Milioni 50 kwa mwezi.

Katibu Tawala wa Wilaya ya Kisarawe Mtela Mwampamba ameishukuru Serikali ya awamu ya tano chini Dkt Magufuli kwa kufanikisha mji wa Kisarawe kupata maji kwa mara ya kwanza toka kupatikana kwa uhuru wa nchi.

Amesema, Dawasa wamekamilisha mradi huu na kwa sasa wananchi wanapata maji ya uhakika na wanaunganishwa kwa Mkopo.

Wananchi wa Kisarawe wameishukuru serikali ya asamu ya tano kwa kuwapelekea maji ndani ya mji wao ambao ulisahaulika kwa kipindi kirefu. 

Ziara hiyo ilihusisha pia na wakurugenzi wa bodi ya Mamlaka ya DAWASA na watendaji mbalimbali wa serikali wakiwamo RUWASA akianzia katika kituo cha kusukumia maji Kibamba hadi tenki la kuhifadhia maji Kisarawe lenye uwezo wa kuhifadhi lita za ujazo milioni 6.
Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa akielezea jambo kwa wakurugenzi wa bodi ya DAWASA wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka hiyo.
Msimamizi wa mradi wa maji Kisarawe kutoka DAWASA Mhandisi Ishmael Kakwezi akieleza jambo kwa Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka hiyo.
Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa akielezea jambo kwa wakurugenzi wa bodi ya DAWASA wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka hiyo.
Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa akielezea jambo kwa wakurugenzi wa bodi ya DAWASA wakati wa ziara yake ya kutembelea miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka hiyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad