Wajasiriamali wadogo maarufu kama wamachinga katika wilaya ya
Kigamboni sasa kuanza kufurahia mikopo kwa ajili ya kukuza na kuboresha
biashara zao kupitia uwezeshaji unatolewa na Benki ya CRDB kupitia mkopo
wa ‘Jiwezeshe’.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mikopo
hiyo ya ‘Jiwezeshe’, Nainu Waziri Ofisi ya Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa Mheshimiwa Japhet Kandege aliipongeza Benki ya CRDB kwa kuwa
Benki ya kwanza nchini kuitikia wito uliofanywa na Mheshimiwa Rais wa
kuwawezesha wajasirimali wadogo maarafu kama wamachinga ambao wengi wao
ni vijana.
“Ni fahari sasa kuona vitambulisho vya Magufuli,
vikizidi kuleta neema kwa wajasiriamali wetu wamamchinga kupitia mikopo
hii ya ‘Jiwezeshe’ kutoka Benki yetu ya CRDB. Salamu hizi mlizotuletea
Benki ya CRDB tutazifikisha kwa Mheshimiwa Rais kumueleza namna ambavyo
mmemuunga mkono,” alisema Naibu Waziri Kandege.
Kwa upande wake,
Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania Dkt. Benard Kibesse aliipongeza
Benki ya CRDB kwa kuwa Benki ya kwanza nchini kutoa mikopo kwa
wajasiliamari wadogo bila riba. “CRDB mmeomyesha njia kuwa hili
linawezekana. Mwaka huu mmeanza na wajasiliamari 3,000, nawapa
changamoto kuwa mwakani tukikutana kama hivi, muwe mmeshatoa mikopo kwa
wajasiliamari 10,000” alisema Dkt.Kibese.
Mkurugenzi Mtendaji wa
Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema mikopo hiyo ya ‘Jiwezeshe’
inatolewa kidijitali kupitia huduma ya SimAccount ambapo wateja wataweza
kukopa kuanzia kiasi cha shilingi 10,000 hadi shilingi 500,000 kupitia
simu zao za mkononi.
“Mjasiriamali anatakiwa kufungua SimAccount
kwa kupiga *150*62# na kisha kujisajili kutumia kitambulisho chake cha
ujasiriamli, ambapo ataweza kunufaika na mkopo binafsi wa ‘Jiwezeshe’ au
kupitia kikundi,” aliongezea Nsekela.
Nsekela alisema kwa
kuzingatia mazingira ya biashara za wajasiriamali wamachinga, Benki ya
CRDB imeachana na mpango wa kutoza riba kwa asilimia na badala yake
mteja atatozwa kiwango kidogo cha kati ya shilingi 5,00 na 2,000 tu
pindi arejeshapo mkopo.
“Tumefanya hivi ili kuwapunguzia mzigo
wajasiriamali hawa wadogo, ili waweze kuwekeza zaidi faidi wanayoipata
kupitia mikopo hii ya ‘Jiwezeshe’,” alisema Nsekela.
Kwa upande
wake Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Sara Msafiri aliwahamasisha
wajasiriamali wadogo katika wilaya hiyo kuchangamkia fursa hiyo ya
mikopo ya ‘Jiwezeshe’ kwa kujiunga na huduma ya SimAccount ya Benki ya
CRDB.
Kupata maelezo zaidi juu ya mikopo ya ‘Jiwezeshe’ tembelea www.crdbbank.co.tz
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Dkt. Faustine Ndugulile (kushoto) akizungumza jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela wakati wa Uzinduzi wa Mikopo ya kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wa Kigamboni, iliyofanyila leo katika Ukumbi wa Kibada Garden, jijini Dar es salaam. Wengine pichani ni Naibu Waziri wa TAMISEMI ambaye pia alikuwa Mgeni Rasmi kwenye hafla hiyo, Josephat Kandege (wa pili kushoto) pamoja na Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Dkt. Bernard Kibese (kulia).
Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya CRDB, Tully Esther Mwambapa akizungumza wakati alipokuwa akiongoza katika hafla ya Uzinduzi wa Mikopo ya kuwawezesha wafanyabiashara wadogo wa Kigamboni, iliyofanyila leo katika Ukumbi wa Kibada Garden, jijini Dar es salaam.
No comments:
Post a Comment