HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 31, 2019

Wachimbaji Madini Ujenzi watakiwa kuwa na Mikataba ya Utoaji Huduma kwa Jamii

Na Greyson Mwase,  Morogoro
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amewataka wachimbaji wa madini ya ujenzi kuwa na mikataba ya utoaji wa huduma kwa jamii inayotambulika kisheria ili kuepuka migongano inayoweza kujitokeza baina yao na wananchi wa  vijiji vinavyozunguka machimbo.

Profesa Kikula alitoa kauli yake katika nyakati tofauti  mkoani Morogoro leo tarehe 30 Oktoba, 2019 kwenye ziara yake  yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini  ujenzi pamoja na kutatua kero mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wa madini hayo.

Katika ziara yake Profesa Kikula aliambatana  na Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Shija, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Morogoro (MOREMA), Dk. Omari Mzeru, Mwenyekiti wa  Madini ya Ujenzi na Wachimbaji Wasio Rasmi, Aquilin Magalambula na  Katibu Tawala wa Wilaya ya Morogoro aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Yahya Nania.

Wengine ni pamoja na Wawakilishi kutoka katika Kurugenzi ya Manispaa ya Morogoro, Kurugenzi ya Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro na Maafisa kutoka Tume ya Madini.

Profesa Kikula mara baada ya kusikiliza  kero za wachimbaji wa madini ya ujenzi katika maeneo tofauti alielekeza kuwa ni vyema wachimbaji wa madini ya ujenzi wakahakikisha wanaingia makubaliano ya kisheria na wanavijiji wanaozunguka machimbo yao  kuhusu utoaji wa huduma kwa jamii kama vile  maji, barabara, ujenzi wa madarasa ili kuepuka migogoro inayoweza kujitokeza mbeleni.

Katika hatua nyingine, Profesa Kikula aliwataka wamiliki wa machimbo ya mchanga kuhakikisha wanakuwa na mipango ya  maandalizi ya ufungaji wa machimbo mara baada ya shughuli za uchimbaji kumalizika na kuanza kuitekeleza kwa kurudishia mashimo vizuri.

“Mnatakiwa kuwa na mpango wa kuanza kurudishia mazingira katika hali nzuri  kabla ya shughuli za uchimbaji wa mchanga kuisha ili kuepuka mashimo ambayo ni hatari kwa wananchi,” alisisitiza Profesa Kikula.

Aidha, aliwataka wamiliki wa machimbo  ya mchanga kuhakikisha wanaweka mazingira mazuri ya kazi kwa wafanyakazi hao kwa kuhakikisha wanakuwa na nyumba na vyoo salama ikiwa ni sehemu ya usalama kwenye machimbo hayo kama Sheria ya Madini na kanuni zake inavyofafanua.

Profesa Kikula aliongeza kuwa, wamiliki wa machimbo hayo wanatakiwa kuhakikisha  wanakuwa na mpango wa huduma ya kwanza kwenye machimbo pamoja na kuhakikisha wachimbaji wanavaa vifaa vya kujikinga na madhara mbalimbali kwenye shughuli zao.

Wakati huohuo, Profesa Kikula alifanya ziara kwenye viwanda vidogo vya kufyatua matofali vya Vibrate Block na Nak Vibrate vilivyopo Wilayani  Morogoro na kuwataka wamiliki wake kuhakikisha wananunua mchanga kwa wachimbaji wenye leseni za madini.

“Ikumbukwe tu kuwa ni kosa la kisheria kununua mchanga kwa mchimbaji asiye na leseni ya madini, adhabu yake ni faini pamoja na kutaifishwa kwa mchanga pamoja na vifaa,”alisisitiza Profesa Kikula.

Profesa Kikula alimwelekeza Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Morogoro (MOREMA), Dk. Omari Mzeru kwa kushirikiana na Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Morogoro kutoa elimu kwa wachimbaji wa madini ya ujenzi kuhusu umuhimu wa kuendesha shughuli za madini  kwa kuwa na leseni za madini, umuhimu wa kuwa na mpango wa utoaji wa huduma ya kwanza kwenye machimbo.

Wakizungumza katika nyakati tofauti wachimbaji wa madini ya ujenzi pamoja na wamiliki wa viwanda vidogo vya kufyatua tofali Wilayani Morogoro walimpongeza Profesa Kikula kwa  kusikiliza na kutatua kero zao.
 Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kulia) akikagua risiti ya malipo kwenye machimbo yanayomilikiwa na Mathayo Mkude yaliyopo katika eneo la Kiegea B Wilayani Morogoro kwenye ziara yake aliyoifanya wilayani humo tarehe 30 Oktoba, 2019 yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi. Kushoto ni Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Shija.
 Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kulia) akitoa maelekezo  kwa wachimbaji wa madini ya ujenzi  kwenye machimbo yanayomilikiwa na Mathayo Mkude yaliyopo katika eneo la Kiegea B Wilayani Morogoro kwenye ziara yake aliyoifanya wilayani humo tarehe 30 Oktoba, 2019 yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi.
Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Shija (mbele) akimwongoza Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula pamoja na  msafara wake kwenye ziara katika machimbo yanayomilikiwa na Mathayo Mkude yaliyopo katika eneo la Kiegea B Wilayani Morogoro kwenye ziara yake aliyoifanya wilayani humo tarehe 30 Oktoba, 2019 yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad