HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 11, 2019

WANAFUNZI 29,264 MANYARA KUFANYA MTIHANI WA DARASA LA SABA

Wanafunzi wa darasa la saba 29,264 wanatarajia kufanya mtihani wa kuhitimu elimu ya shule ya msingi kwenye Halmashauri saba za wilaya kwenye Mkoa wa Manyara.

Katibu Tawala wa mkoa wa Manyara, Missaile Mussa alisema mitihani hiyo inafanyika kwa muda wa siku mbili za jumatano na alhamisi.

Mussa alisema kati ya wanafunzi hao 29,264 wanaotarajiwa kufanya mitihani wasichana ni 15, 502 na wavulana ni 13,762

Alisema wanafunzi hao wanatarajiwa kufanya mtihani huo kwenye shule 606 zilizopo kwenye halmashauri saba za wilaya ya Babati mji, halmashauri ya wilaya ya Babati, Kiteto, Simanjiro, halmashauri ya wilaya ya Mbulu, Hanang' na Mbulu mji.

"Tumejipanga vizuri kuhakikisha unafanyika ipasavyo, hatuna mashaka, usalama utakuwepo wakati wote wanafunzi wamejiandaa na mtihani na wasimamizi tuliwapa semina ya namna ya kusimamia," alisema Mussa.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kiteto, Tamim Kambona alisema wanafunzi 3,808 wanatarajia kufanya mtihani huo kwenye shule za msingi 87.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbulu, Hudson Kamoga alisema wanafunzi 3,900 watafanya mtihani kwenye shule za msingi 88 zenye mikondo 177.

Mkurugenzi wa mji wa Babati, Fortunatus Fwema alisema wanafunzi 2,171 watafanya mtihani kwenye shule za msingi 39.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Simanjiro Yefred Myenzi alisema wanafunzi 3,243 watafanya mtihani huo kwenye shule za msingi 81.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Babati, Hamis Malinga alisema wanafunzi 7,213 wakiwemo wavulana 3,225 na wasichana 3,988 wanatarajia kufanya mtihani kwenye shule 141.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad