HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 27, 2019

Viongozi wa Vijiji na Halmashauri watakiwa kutenga fedha za kuunganisha umeme

Na Hafsa Omar, Rukwa
Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amewaagiza viongozi wa Serikali za Vijiji na Halmashauri kote nchini, kutenga  fedha kwa ajili ya kulipia gharama za kuunganisha umeme kwenye  Taasisi za Umma na hivyo kuboresha huduma za kijamii katika maeneo yao.

Alitoa agizo hilo Agosti 26, 2019, akiwa katika Kijiji cha Mkinga na Mkomolo wilayani Nkasi Mkoa wa Rukwa wakati  akizungumza na wananchi wa vijiji hivyo kabla ya kuwasha umeme kwenye Vijiji husika.

 Dkt Kalemani aliwaambia viongozi hao  kuwa,  umeme unapofika kwenye maeneo yao, umekuwa ukisambazwa  kwenye nyumba za wananchi na wanazisahau taasisi za umma hivyo ni muhimu kwa Taasisi hizo kupewa kipaumbele..

“Niwaombe viongozi wa Serikali za Vijiji, Mwenyekiti wa Halmashauri na Mkurugenzi mtenge fedha kwa ajili ya kuunganisha umeme kwenye taasisi za umma, kama umeme upo jambo la kwanza kwenye vijiji ni kuunganisha umeme kwenye Zahanati au Shule.” Alisema Dkt Kalemani.

Aidha, Dkt Kalemani aliwaagiza wakandarasi wa umeme vijijini, kuajiri vibarua wengi ili kazi ya usambazaji umeme ifanyike kwa kasi na wananchi pamoja na taasisi mbali mbali za umma zipate umeme wa uhakika na  kwa haraka.

Alitoa msisitizo kuhusu kuajiri vijana kutoka maeneo ambayo kazi za usambazaji umeme zinafanyika ili kutoa ajira kwa wakazi wa maeneo hayo ya vijijini, “nimeshapiga marufuku vibarua wa kutoka maeneo ya mbali, kazi za hapa zifanywe na vibarua kutoka eneo hili, Mwenyekiti wa kijiji simamia hili.” Alisema Dkt Kalemani.

Vile vile, Dkt Kalemani aliwahamasisha wananchi wa vijiji hivyo kujenga viwanda vya kukoboa na kusaga nafaka ili kuboresha maisha yao na kutunza miundombinu ya umeme ili wanufaike na nishati hiyo ambayo itakuwa ni mkombozi wa maisha yao, “mtunze miundombinu ya umeme msikate nyaya, msichome moto nguzo, wala msiibe transfora.”alisisitiza.

 Pia, Dkt. Kalemani alitoa agizo kwa TANESCO kudhibiti suala la uwepo wa vishoka kwa  kubandika katika ofisi za Tanesco, majina ya wakandarasi wote wenye vigezo vya kufanya kazi za wiring kwenye makazi ya wananchi.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika Kijiji cha Mkinga wilayani Nkasi ili kukagua kazi ya usambazaji umeme na kuwasha rasmi umeme kwenye Kijiji hicho.
 Baadhi ya wananchi katika Kijiji cha Mkomolo wilayani Nkasi, wakimsikiliza Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani mara baada ya kufika Kijijini hapo ili kukagua kazi ya usambazaji umeme na kuwasha rasmi umeme kwenye Kijiji hicho.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa pili kushoto) akifurahi mara baada ya kukata utepe, kuashiria uwashaji rasmi umeme  katika Kijiji cha Mkinga wilayani Nkasi. Wa Pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Said Mtanda.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akizungumza na wananchi  katika Kijiji cha Mkinga wilayani Nkasi baada ya kufika kijijini hapo kukagua kazi ya usambazaji umeme na kuwasha rasmi umeme kwenye Kijiji hicho.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad