HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, August 29, 2019

TBS yawanoa wazalishaji, waagizaji, wasambazaji na wauzaji wa nondo nchini

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI), Leodgar Tenga, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuhusiana na umuhimu wa viwango kwa bidhaa za ndono wakati wa semina iliyoandalisha na Shirika la Viwango Tanzania (TBS). 
Picha na Chalila Chibuda.

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limewapatia elimu wazalishaji, waagizaji, wasambazaji na wauzaji wa nondo nchini kuhusiana na taratibu na mifumo ya ukaguzi wa bidhaa hizo nje kabla ya kuingizwa nchini ili kuhakikisha zinakidhi viwango.

Semina hiyo ambayo ilifanyika Makao Makuu ya Shirika hilo, Ubungo, jijini Dar es Salaam ilifunguliwa na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Yusuf Ngenya.

Amesema kupitia semina hiyo ambayo ni sehemu ya taratibu za shirika hilo kwa wazalishaji wa bidhaa mbalimbali, wadau hao wataelimishwa utaratibu za uthibitishaji ubora wa bidhaa za nondo, matakwa ya viwango na taratibu za kupata huduma za shirika hilo kwa kutumia mfumo wa kielektroniki.

Hivi karibuni maofisa ukaguzi na udhibiti walifanya ukaguzi wa kushtukiza kwenye masoko na kubaini kuwepo kwa nondo zenye dosari mbali mbali hasa kwenye viwango  vya urefu na upana.

Dkt. Ngenya, amewaambia washiriki wa semina hiyo kuwa nondo ni bidhaa muhimu kwa Taifa hasa kipindi hiki ambacho taifa lipo kwenye mkakati wa ujenzi viwanda. "Hivyo tumeona ni muhimu kukaa na wadau wote wa nondo na kukumbushana umuhimu wa kuzalisha, kuagiza, kusambaza na kuuza nondo zenye viwango," alisema Dkt. Ngenya.

Amekiri kwamba kuna kasoro ndogo ndogo wamezibaini kwenye uzalishaji wa nondo na kwamba hiyo ni moja ya sababu ya kuja na semina hiyo.  

Ametoa mwito kwa Watanzania kutonunua nondo bila kujua urefu na upana wake ni kiasi gani. Alifafanua kwamba wanatambua kwamba sio rahisi kwa mnunuzi kujua viwango vya nondo kwa macho, ndiyo maana shirika hilo linaweka msisitiza kwa wazalishaji, waagizaji, wasambazaji na wauzaji ili kuhakikisha wazalisha nondo zenye viwango. 

Amesema kwa kuzingatia kifungu cha 36 cha Sheria ya Viwango Na.2 ya mwaka 2009, Serikali ilipitisha kanuni za udhibiti wa shehena kupitia notisi ya Serikali Na. 405 ya Desemba 2009.

Kwa mujibu wa Dkt. Ngenya kanuni hizo ziliipa TBS mamlaka ya kudhibiti ubora wa bidhaa zinazoingia nchini kabla ya kusambazwa kwenye soko la ndani.

Amesema Februali 1, mwaka 20012 shirika hilo lilianzisha mfumo wa ukaguzi wa bidhaa kabla ya kusafirishwa kuletwa nchini kama mpango wa udhibiti ubora wa bidhaa katika nchi zinakotoka ambao unasaidia kutatua changamoto zilizokuwepo wakati wa bidhaa zilipokuwa zinakaguliwa baada ya kufika nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirikisho la Wenye Viwanda Tanzania (CTI), Leodgar Tenga, aliipongeza TBS kwa kuandaa semina hiyo hasa kwa kuzingatia kwamba viwango ni jambo la muhimu sana.

"Ni muhimu kwa wazalishaji wote kuhakikisha viwango vinaheshimika,"alisema Tenda. Amesisitiza kwamba ubora wa nondo zinazozalishwa nchini na zinazotoka nje ni muhimu sana, hivyo alitoa mwito kwa wadau wote kuzingatia viwango.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad