Na Ales Mbilinyi – JKCI
Tafiti saba za magonjwa ya moyo zilizofanywa na Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) zinatarajiwa kuwasilishwa katika mkutano
wa wanasayansi, madaktari bingwa na wahudumu wa afya wanaotoka katika
nchi za ukanda wa Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika utakaofanyika
wiki ijayo nchini Zambia.
Tafiti hizo ambazo zimefanyika mwaka jana na mwaka huu ni kuhusu
mwenendo wa mapigo ya moyo kwa mgonjwa, wagonjwa wenye moyo ambao
uwezo wake wa kufanya kazi umepungua jinsi wanavyozingatia matibabu
kama walivyoshauriwa na madaktari, shinikizo la damu na tatizo la
kisukari.
Tafiti nyingine zitakazowasilishwa ni upungufu wa nguvu za kiume
katika jamii, uelewa wa sababu hatarishi za magonjwa ya moyo katika
jamii, magonjwa matatu kwa pamoja yaani moyo na figo kushindwa
kufanya kazi na upungufu wa damu mwilini.
Akizungumza kuhusu tafiti hizo Mkuu wa Kitengo cha Utafiti wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Pedro Pallangyo alisema tafiti hizo
zimefanyika katika mkoa wa Dar es Salaam kwa kipindi cha miaka miwili
na na kwa wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi hiyo.
“Tumekuwa tukifanya tafiti mbalimbali kuhusu magonjwa ya moyo ambazo
zinatusaidia kufahamu wagonjwa wetu pamoja na wananchi wanaotuzunguka
wanakabiliwa na matatizo gani katika afya za moyo na hii inatusaidia
kuweza kuboresha huduma zetu”,.
Akizungumza kuhusu mkutano huo wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza Dkt.
Pedro alisema kwa upande wa magonjwa ya moyo utawasaidia
kubadilishana matokeo ya huduma za matibabu wanazozitoa hasa tafiti
zinazofanywa katika nchi mbalimbali ili kuboresha huduma zinazotolewa
kwa wagonjwa.
Kwa upande wake Afisa uuguzi wa JKCI Jalack Milinga ambaye alishiriki
katika kufanya tafiti hizo alisema kwake ni mara ya kwanza kuhudhuria
mkutano huo ambao utamsaidia kuongeza ujuzi katika utoaji wa huduma
kwa wagonjwa wa moyo lakini pia kubadilishana uzoefu na wauguzi
wenzake watakaoshiriki katika mkutano huo.
“Utafiti wangu uliangalia jinsi ya uzingatiaji wa unywaji wa dawa za
moyo kwa wagonjwa ambao mioyo yao haifanyi kazi vizuri. Hivyo naamini
ushiriki wangu katika mkutano huu utaniwezesha kupata mbinu mpya za
kusimamia jukumu la kuwasaidia wagonjwa wetu kuzingatia matibabu ili
kupata matokeo bora ya tiba”, alisema Jalack.
Naye daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI Smita Bhalia alisema
ushiriki wa wataalamu kutoka Tanzania umelenga kutoa matokeo ya
utafiti uliofanywa hapa nchini na kuonesha baadhi ya magonjwa yasiyo
ya kuambukiza jinsi yanavyoweza kusababisha magonjwa ya moyo ama
magonjwa ya moyo yanavyoweza kupelekea mtu kupata magonjwa mengine
yasiyo ya kuambukiza.
Malengo ya mkutano huo ni kwa nchi washiriki kutoka ukanda wa
Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika kuona jinsi ya kushirikiana
katika kufanya tafiti za ndani, kuwa na njia bora na za kisasa za
matibabu ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza na kuwa na mbinu mpya za
kuweza kuzia magonjwa hayo.
Mkutano huo ambao hufanyika kila mwaka unatarajia kufayika mjini
Living stone nchini Zambia kuanzia tarehe tano hadi saba mwezi ujao
ambapo mwaka jana mkutano kama huo ulifanyika jijini Nairobi nchini
Kenya.
Mkuu wa Kitengo cha Utafiti kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Pedro Pallangyo akiwaeleza wafanyakazi wa Taasisi hiyo
(hawapo pichani) kuhusu tafiti saba za magonjwa ya moyo zilizofanywa na
Taasisi hiyo ambazo zitawasilishwa katika mkutano wa kimataifa wa
magonjwa yasiyo ya kuambukiza utakaofanyika wiki ijayo nchini Zambia.
Daktari
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Happiness Swai akiwaeleza
wafanyakazi wa Taasisi hiyo (hawapo pichani) kuhusu utafiti wa shinikizo
la damu na tatizo la kisukari uliofanywa na Taasisi hiyo ambao ni moja
ya tafiti saba za magonjwa ya moyo ambazo zitawasilishwa katika mkutano
wa kimataifa wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza utakaofanyika wiki ijayo
nchini Zambia.
Wataalamu
wa Afya kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambao walifanya
tafiti saba za magonjwa ya moyo ambazo zitawasilishwa katika mkutano wa
kimataifa wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza utakaofanyika wiki ijayo
nchini Zambia wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuzielezea
tafiti hizo kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo leo jijini Dar es Salaam.
Picha na JKCI
No comments:
Post a Comment