Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Joachim Wangabo amemtaka mkandarasi wa
Kampuni ya Tender International kuhakikisha anamaliza ujenzi wa Chuo
cha Ufundi VETA kilichopo Kata ya Sumbawanga Wenyeji Wilayani
Sumbawanga ndani ya mwaka huu ili kufikia mwezi Januari mwaka 2020
kianze kudahili wanafunzi katika fani mbalimbali za ufundi.
Chuo hicho ambacho ujenzi wake ulitakiwa kumalizika Septemba 21, 2019
bado haujakamilika kutokana na Mkandarasi huyo kutegemea fedha za
ujenzi kutoka serikalini na hivyo kuomba kuongezewa muda wa miezi
minne ili aweze kumalizia ambapo hadi sasa ameshalipwa shilingi
bilioni 2.6 kwaajili ya ujenzi wa majengo 22 ikiwemo karakana
mbalimbali za mafunzo, mabweni, madarasa na nyumba za watumishi.
Mbali na changamoto hiyo Mh. Wangabo pia amepongeza kiwango cha ubora
wa majengo hayo ambayo kwasasa yapo katika hatua ya kupauliwa na
kuongeza kuwa kama kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa imeridhishwa na
kiwango cha majengo ya chuo hicho hadi hapo kilipofikia.
“VETA hii ilianza kujengwa mwaka jana mwezi wa tisa na ilitegemewa iwe
imemalizika mwaka huu, kipindi cha mwaka mmoja. Lakini kumekuwa na
changamoto za hapa na pale upande wa mkandarasi n ahata upande wa
wizara inayohusika, basi hizi changamoto zimefikia kwenye hatua ambayo
sasa tunaweza kwenda vizuri, Mkandarasi ameomba kuongezewa miezi minne
na hii mimi nitaifuatilia, kuhakikisha kwamba hii ‘extention’
inakwenda haraka ili ikamilike ili ianze kuchukua wananfunzi Januari
2020,” Alisema.
Ameyasema hayo leo tarehe 29.8.2019 alipotembelea katika eneo la
Ujenzi wa Chuo hicho kinachotarajiwa kudahili wanafunzi 600 wa masomo
ya muda mrefu na wanafunzi 2000 wa masomo ya muda mfupi katika fani za
umeme wa majumbani, umeme wa magari, ushonaji, mapishi, ufundi wa
kompyuta, ufundi wa magari, useremala, na usindikaji wa chakula.
Awali akizungumza wakati wa kutoa taarifa ya ujenzi wa Chuo hicho
karani wa Mradi Mhandisi Jeremiah Longido alisema kuwa endapo serikali
italipa fedha za ujenzi kwa wakati wana uhakika kwamba majengo hayo
yatakamilika katika kipindi hicho cha miezi minne waliyoiomba na
hatimae kufikia mwezi January, 2020 kuanza kudahili wanafunzi.
“Kama ‘Cash flow’ itakwenda vizuri, hii miezi minne kama kazi
itafanyika kwa nguvu tunaweza kumaliza kazi, kwasababi amelipwa
‘certificate’ namba nne ambayo ni kama milioni 130 lakini kuna
‘certificate’ namba tano kama milioni 640 amabyo ipo tayari ambapo mda
wowote anaweza kulipwa kwahiyo kama hiyo atapokea inamaanisha tutakuwa
vizuri,” Alisema.
Katika Hatua nyingine, Mh. Wangabo amesikitishwa na kasi ya konokono
katika ujenzi wa hospitali za Wilaya ambazo kwa mujinbu wa tarehe za
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, hospitali hizo
ziliongezewa muda wa kuisha kwake na zilitakiwa kumalizika na
kukabidhiwa tarehe 31.8.2019 kwaajili ya kuanza kutumika.
“Kasi yenu ni ndogo, kasi ya konokono, vifaa havipo hata ujenzi katika
jengo hili la utawala hakuna, hali kwakweli ni hovyo na si nzuri ni
mbaya muda umekwishaisha, kwahiyo nashindwa hata kuwaambia kuna siku
za nyongeza kwasababu kuna ‘deadline’ ya TAMISEMI. Sasa fanyeni juu
chini kwa siku zilizobakia mmalize hapa sasa sijui mtaweka hema ama
mtafanyaje lakini fanyeni juu chini hii kazi iishe,” Alisisitiza
Ameyasema hayo baada ya kukagua ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya
Sumbawanga akiwa na kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa, viongozi na
wataalamu wa wilaya ya Sumbawanga ambapo kabla ya kufika hapo pia
alitembelea hospitali ya Wilaya ya Nkasi na hospitali ya Wilaya ya
Kalambo.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ( wa Mbele) akikagua jengo la Utawala katika Hospitali ya Wilaya ya Sumbawanga iliyoko katika Kata ya Mtowisa, bonde la ziwa Rukwa
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ( wa pili toka kulia) akiongozana akiongozana na Karani wa Mradi wa ujenzi wa Chuo Cha Ufundi VETA Mkoani Rukwa Mhandisi Jeremiah Longido wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa chuo hicho.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa mbele) pamoja na viongozi na wataalamu wengine wakitoka katika jengo la Maabara la hospitali ya Wilaya ya Nkasi.
Baadhi ya majengo ya Chuo Cha Ufundi VETA Mkoani Rukwa
No comments:
Post a Comment