HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, July 26, 2019

WALIOFUJA FEDHA MRADI WA MIYOGWEZI UKEREWE KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA

NA BALTAZAR MASHAKA, UKEREWE
SERIKALI imesema waliohusika kwenye ubadhirifu wa fedha za Mradi wa Umwagiliaji wa Miyogwezi wilayani Ukerewe na kusababisha ujengwe chini ya kiwango na kutokamilika licha ya sh. milioni 750 kutolewa watachukuliwa hatua za kisheria.

Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba alisema jana wilayani Ukerewe baada ya kutembelea na kukagua miradi ya umwagiliaji ya Miyogwezi na Bugorola ambao miundombinu yake imechoka na kusababisha ushindwe kufanya kazi.

Akizungumza kwenye eneo la mradi wa Miyogwezi na wakulima wanaotumia bonde la mradi huo kwa kilimo, alisema kuna harufu ya rushwa kwenye mradi huo ambao mkandarasi alilipwa sh. milioni 684 kati ya sh. milioni 750 bila kuukamilisha na kuhoji nani alisababisha fedha zikatumika kinyume cha utaratibu wa serikali.

Alisema serikali iliamua kujenga miradi ya umwagiliaji ili kuleta maendeleo endelevu kwenye sekta ya kilimo baada ya kukusanya na kutenga fedha ili wananchi wafaidi keki ya nchi na kulima kwa tija lakini wajanja wa wizara yake wakaleta kampuni za mifukoni zila fedha, kwamba si haki na hawakuwatendea haki watanzania.

Alisema cha kushangaza Ukerewe ilipewa mradi wa miyogwezi na kampuni ya CODA ya nchini Kenya iliyopewa kazi ya kujenga mradi huo ililipwa bila kustahili malipo ya sh. milioni 684 bila kukamilisha mradi huo kwa asilimia 55 baada ya kujenga mabanio mawili chini ya kiwango, magati, mitaro miwili ya maji lakini haikusakafiwa na haikufika mwisho pamoja na vigawa maji 16.

“Siamini nilichokiona hapa na kilichopo kwenye nyaraka (mkataba), mradi huu una harufu ya rushwa na matumizi mabaya ya fedha za umma.Thamani ya mradi ni sh. milioni zaidi ya 700 bado haujakamilika,umetekelezwa kwa asilimia 45 tu.Mkandarasi amelipwa wakati kazi hailingani na thamani ya fedha na waliofanya hayo bado wapo ofisini na kwa nini bado wapo,” alisema Mgumba.

Alionya fedha hizo hazitakwenda bure na kuiagiza Tume ya Umwagiliaji kuandaa taarifa ya kina ya mradi wa Miyogwezi ikiainisha nani alilipwa wakati kazi haikukamilika,waliohusika kwenye ubadhirifu huo, nani aliyesababisha fedha zitumike kinyume cha mipango ya serikali ili ijue njia wanazotumia kutafuna fedha za umma na makosa yasirudiwe.

Naibu Waziri huyo wa Kilimo alisema miongoni mwa kanda ambazo hazikufanya vizuri kwenye miradi ya umwagiliaji ni Mwanza, kwani miradi hiyo ilijengwa chini ya kiwango na kushangaa kwa nini watendaji waliokuwa wakisimamia miradi hiyo bado wako ofisini na kuwataka wajipime kama wanafaa kukalia nafasi hizo.

Mgumba akijibu ombi la wakulima hao la kutaka waletewe fedha zingine baada ya wajanja wakupiga (walikula) fedha za mradi huo alisema serikali haiwezi kuleta fedha hadi ijue nani aliipiga ili achukuliwe hatua za kisheria na liwe fundisho kwa wengine na kueleza kuwa serikali inafanya kazi kwa bajeti iliyopitishwa na bunge.

Aidha, alieleza kuwa wataalamu wanayo kazi ya kuisaidia serikali ili mradi huo wa Miyogwezi ukamilike na itakuwa tayari kutoa fedha baad ya kujiridhisha kuwa fedha za awali zililiwa ndo maana Tume ya Umwagiliaji imeundwa kusimamia miradi ya umwagiliaji.

Awali Mbunge wa Ukerewe (CCM) Josephat Mkundi alisema mradi huo wa kilimo cha umwagiliaji uliokuwa ukisimamiwa na District Agriculture Investment Project (DASIP) ulijengwa mwaka 2013 kwenye kwa ajili ya kuwanufaisha wakulima 194 lakini haufanyi kazi kutokana na miundombinu yake kutokamilika.

Mbunge huyo wa Ukerewe alisema sh. milioni 200 zilitolewa na Dairy Processing & Infrastructure Development Fund (DIDF) ambapo DASIP ilitoa milioni 550 kwa ajili ya mradi huo lakini hadi sasa haujakamilika ambapo akiwa bungeni Januari mwaka huu alihoji serikali ni lini mradi wa Miyogwezi utaboreshwa na kamilika ili kuweza kuwasaidia wakulima wanaotumia bonde hilo kwa kilimo, kulima kwa tija.
 Naibu Waziri wa Kilimo Omari Mgumba ,wa pili akielekea kukagua miundombinu ya mradi wa umwagiliaji wa Miyogwezi wilayania Ukerewe jana.Wa tatu ni Mbunge wa Ukerewe Josephat Mkundi, nyuma ya Mkundi ni Mhandisi wa Tume ya Umwangiliaji Kanda ya Mwanza, Adelialid Mwesiga na mwisho ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Focus Majumbi.Picha na Baltazar Mashaka
 Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba, wa tatu kutoka kulia akiwa ameanda juu ya banio la maji la mradi wa Miyogwezi jana alipokagua mradi huo uliokwama tangu mwaka 2013.Kulia ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Ukerewe Focua M Majumbi.Wa tatu kutoka kushoto ni Mbunge wa Ukerewe, Josephat Mkundi. Picha na Baltazar Mashaka.

 Kaimu Ofisa Kilimo Wilaya ya Ukerewe Issa Mugenyi (kulia) akitoa maelezo ya mradi wa Miyogwezi kwa Naibu wa Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba (wa pili kulia,aliyesimama juu ya banio la maji ) jana alipokwenda kukagua miundombinu ya mradi huo wilayani Ukerewe.Nyuma ya Naibu waziri ni Mbunge wa Ukerewe Josephat Mkundi na kulia wa kwanza ni Katibu Tawala wa Wilaya na Kaimu Mkuu wa wilaya hiyo Focus Majumbi.


 Naibu Waziri wa Kilimo , Omari Mgumba , wa pili akikagua moja ya mitaro ya mradi wa umwagiliaji wa mradi wa Miyogwezi wilayania Ukerewe, numa ni mbunge wa jimbo hilo Josephat Mkundi.

Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba (katikati) akimhoji jambo kaimu Ofisa kilimo Wilaya ya Ukerewe Issa Mugenyi (kulia) baada ya kumpa maelezo yasiyoridhisha ya mradi wa umwagiliaji wa Miyogwezi wilayani Ukerewe jana.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad