NA BALTAZAR MASHAKA, UKEREWE
SERIKALI imesema waliohusika kwenye ubadhirifu wa fedha za Mradi wa
Umwagiliaji wa Miyogwezi wilayani Ukerewe na kusababisha ujengwe chini
ya kiwango na kutokamilika licha ya sh. milioni 750 kutolewa
watachukuliwa hatua za kisheria.
Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba alisema jana wilayani Ukerewe
baada ya kutembelea na kukagua miradi ya umwagiliaji ya Miyogwezi na
Bugorola ambao miundombinu yake imechoka na kusababisha ushindwe
kufanya kazi.
Akizungumza kwenye eneo la mradi wa Miyogwezi na wakulima wanaotumia
bonde la mradi huo kwa kilimo, alisema kuna harufu ya rushwa kwenye
mradi huo ambao mkandarasi alilipwa sh. milioni 684 kati ya sh.
milioni 750 bila kuukamilisha na kuhoji nani alisababisha fedha
zikatumika kinyume cha utaratibu wa serikali.
Alisema serikali iliamua kujenga miradi ya umwagiliaji ili kuleta
maendeleo endelevu kwenye sekta ya kilimo baada ya kukusanya na
kutenga fedha ili wananchi wafaidi keki ya nchi na kulima kwa tija
lakini wajanja wa wizara yake wakaleta kampuni za mifukoni zila fedha,
kwamba si haki na hawakuwatendea haki watanzania.
Alisema cha kushangaza Ukerewe ilipewa mradi wa miyogwezi na kampuni
ya CODA ya nchini Kenya iliyopewa kazi ya kujenga mradi huo ililipwa
bila kustahili malipo ya sh. milioni 684 bila kukamilisha mradi huo
kwa asilimia 55 baada ya kujenga mabanio mawili chini ya kiwango,
magati, mitaro miwili ya maji lakini haikusakafiwa na haikufika mwisho
pamoja na vigawa maji 16.
“Siamini nilichokiona hapa na kilichopo kwenye nyaraka (mkataba),
mradi huu una harufu ya rushwa na matumizi mabaya ya fedha za
umma.Thamani ya mradi ni sh. milioni zaidi ya 700 bado
haujakamilika,umetekelezwa kwa asilimia 45 tu.Mkandarasi amelipwa
wakati kazi hailingani na thamani ya fedha na waliofanya hayo bado
wapo ofisini na kwa nini bado wapo,” alisema Mgumba.
Alionya fedha hizo hazitakwenda bure na kuiagiza Tume ya Umwagiliaji
kuandaa taarifa ya kina ya mradi wa Miyogwezi ikiainisha nani alilipwa
wakati kazi haikukamilika,waliohusika kwenye ubadhirifu huo, nani
aliyesababisha fedha zitumike kinyume cha mipango ya serikali ili ijue
njia wanazotumia kutafuna fedha za umma na makosa yasirudiwe.
Naibu Waziri huyo wa Kilimo alisema miongoni mwa kanda ambazo
hazikufanya vizuri kwenye miradi ya umwagiliaji ni Mwanza, kwani
miradi hiyo ilijengwa chini ya kiwango na kushangaa kwa nini watendaji
waliokuwa wakisimamia miradi hiyo bado wako ofisini na kuwataka
wajipime kama wanafaa kukalia nafasi hizo.
Mgumba akijibu ombi la wakulima hao la kutaka waletewe fedha zingine
baada ya wajanja wakupiga (walikula) fedha za mradi huo alisema
serikali haiwezi kuleta fedha hadi ijue nani aliipiga ili achukuliwe
hatua za kisheria na liwe fundisho kwa wengine na kueleza kuwa
serikali inafanya kazi kwa bajeti iliyopitishwa na bunge.
Aidha, alieleza kuwa wataalamu wanayo kazi ya kuisaidia serikali ili
mradi huo wa Miyogwezi ukamilike na itakuwa tayari kutoa fedha baad ya
kujiridhisha kuwa fedha za awali zililiwa ndo maana Tume ya
Umwagiliaji imeundwa kusimamia miradi ya umwagiliaji.
Awali Mbunge wa Ukerewe (CCM) Josephat Mkundi alisema mradi huo wa
kilimo cha umwagiliaji uliokuwa ukisimamiwa na District Agriculture
Investment Project (DASIP) ulijengwa mwaka 2013 kwenye kwa ajili ya
kuwanufaisha wakulima 194 lakini haufanyi kazi kutokana na miundombinu
yake kutokamilika.
Mbunge huyo wa Ukerewe alisema sh. milioni 200 zilitolewa na Dairy
Processing & Infrastructure Development Fund (DIDF) ambapo DASIP
ilitoa milioni 550 kwa ajili ya mradi huo lakini hadi sasa
haujakamilika ambapo akiwa bungeni Januari mwaka huu alihoji serikali
ni lini mradi wa Miyogwezi utaboreshwa na kamilika ili kuweza
kuwasaidia wakulima wanaotumia bonde hilo kwa kilimo, kulima kwa tija.
Naibu Waziri wa Kilimo Omari Mgumba ,wa pili akielekea kukagua miundombinu ya mradi wa umwagiliaji wa Miyogwezi wilayania Ukerewe jana.Wa tatu ni Mbunge wa Ukerewe Josephat Mkundi, nyuma ya Mkundi ni Mhandisi wa Tume ya Umwangiliaji Kanda ya Mwanza, Adelialid Mwesiga na mwisho ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Focus Majumbi.Picha na Baltazar Mashaka
Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba, wa tatu kutoka kulia akiwa ameanda juu ya banio la maji la mradi wa Miyogwezi jana alipokagua mradi huo uliokwama tangu mwaka 2013.Kulia ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Ukerewe Focua M Majumbi.Wa tatu kutoka kushoto ni Mbunge wa Ukerewe, Josephat Mkundi. Picha na Baltazar Mashaka.
Kaimu Ofisa Kilimo Wilaya ya Ukerewe Issa Mugenyi (kulia) akitoa maelezo ya mradi wa Miyogwezi kwa Naibu wa Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba (wa pili kulia,aliyesimama juu ya banio la maji ) jana alipokwenda kukagua miundombinu ya mradi huo wilayani Ukerewe.Nyuma ya Naibu waziri ni Mbunge wa Ukerewe Josephat Mkundi na kulia wa kwanza ni Katibu Tawala wa Wilaya na Kaimu Mkuu wa wilaya hiyo Focus Majumbi.
Naibu Waziri wa Kilimo , Omari Mgumba , wa pili akikagua moja ya mitaro ya mradi wa umwagiliaji wa mradi wa Miyogwezi wilayania Ukerewe, numa ni mbunge wa jimbo hilo Josephat Mkundi.
Naibu Waziri wa Kilimo, Omari Mgumba (katikati) akimhoji jambo kaimu Ofisa kilimo Wilaya ya Ukerewe Issa Mugenyi (kulia) baada ya kumpa maelezo yasiyoridhisha ya mradi wa umwagiliaji wa Miyogwezi wilayani Ukerewe jana.
No comments:
Post a Comment