HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, July 16, 2019

CHINA KUENDELEA KUIUNGA MKONO ZANZIBAR KATIKA SEKTA YA AFYA

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
BALOZI mdogo wa Jamhuri ya watu wa China Xie Xiuowu amesema nchi yake itaendeleza azma yake ya kuisaidia Zanzibar katika nyanja tofauti ikiwemosekta ya afya ikiwa ni juhudi zake za kukuza uhusiano miongoni mwa nchi hizo mbili.

Alisema misaada wanayoitoa inaongozwa na dhamira njema hasa kwa watu wenye mahitaji ili kuona nao wanaendelea kufurahia maisha yao ya kila siku.

Balozi Xie aliyasema hayo katika hafla ya kuwaaga madaktari wa China wanaomaliza muda wao na kuwakaribisha madaktari wapya ambao nao watahudumu katika sekta ya afya Zanzibar kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Alikumbusha kuwa Jamhuri ya Watu wa China ilianzisha utaratibu wa kuleta madaktari Zanzibar tokea mwaka 1964 na utaratibu huo unaendelezwa na kuimarishwa zaidi hadi sasa.

Alisema kwa sasa wanatekeleza mradi wa kupambana na kichocho, saratani ya shingo ya kizazi na kuwajengea uwezo watendaji katika sekta ya tofauti ili kuimarisha uhusiano kati ya Zanzibar na China.

Kwa upande wake Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed alisema uhusiano wa China na Zanzibar unaendelea kuimarika siku hadi siku na kuiomba China ifikirie namna ya kuwafanya madaktari hao kutumia muda wa miaka miwili Zanzibar badala ya mmoja ili kutoa huduma zaidi.

Alisema kupitia uhusiano huo China imeweza kuimarisha ujenzi wa miundombinu ikiwemo hospital ya Abdalla Mzee kisiwani Pemba.

Aidha aliongeza kuwa wataalam wanaokuja kutoka China husaidia pia huwaongezea ujuzi wananchi na madakri wa Zanzibar kupitia programu mbali mbali ikiwemo za televisheni na hospitalini.

Waziri Hamad aliwashukuru kupitia mradi wa kupambana na maradhi ya kichocho ambapo dola za Marekani Milioni 5 walizotoa zitasaidia kupambana na maradhi ya Kichocho Zanzibar.

Alisema pesa hizo pia zitatumika katika programu ya miaka mitano ya kupambana na maradhi ya saratani ya shingo ya mlango wa kizazi kwa wanawake wa Zanzibar.

“Kiujumla misaada wanayoitoa ndugu zetu hawa ni mingi sana na hawajawahi kutuwekea masharti yanayotubana, tunashirikiana nao vyema tofauti na misaada ya nchi nyingine”, alibainisha Waziri Hamad.

Aidha Hamad aliwasifia madaktari hao kwa nidhamu ya kazi ambayo inapaswa kuigwa na madaktari wazalendo ikiwemo ya kuwahi kazini mapema bila ya malalamiko yoyote.

“Hili la nidhamu ya kazi kwa kweli sisi kama Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla tunapaswa tuige. Wanawahi kazini na kuondoka kwa wakati na husikii wakipewa lawama na wananchi wanaowahudumia”, alisema Waziri Hamad.

Kuhusu timu ya madaktari wapya, Waziri Hamad alisema waliokuja ni wataalamu zaidi ambao pia watatumika kutoa elimu katika ngazi za vyuo vikuu vya Zanzibar.

Akitoa salamu za shukran kwa niaba ya wenzake Mkuu wa madakrari waliomaliza muda wao Dk.Zhang Zhen ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ukarimu wao waliouonesha katika kipindi chote cha kuhudumia wananchi Zanzibar.

Alisifia mazingira safi ya visiwa vya bahari ya Hindi ikiwemo Zanzibar ambavyo vitaendelea kubaki katika kumbukumbu zake.

Nae Kiongozi wa timu mpya ya madaktari hao Dk. Yang Xiaodong aliahidi kufanya kazi kwa uadilifu, uaminifu na weledi ili kutimiza malengo yaliyokusudiwa.
 Balozi mdogo wa China Xie Xiuowu msitari wa pili waliokaa na Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed kushoto kwake wakiwa katika Picha ya pamoja na Timu ya Madaktari wnaomaliza muda wao wa mwaka mmoja kutoa huduma kwa wananchi wa Zanzibar.
 Balozi mdogo wa China Xie Xiuowu katikati na Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed kushoto kwake, wakiwa katika Picha ya pamoja na Timu ya Madaktari wapya kutoka China ambao watakuwa wakifanya kazi ya kuhudumia wagonjwa kwa kipindi cha mwaka mmoja Zanzibar.
 Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid akibadilishana mawazo na Balozi mdogo wa China Xie Xiuowu wakati wa hafla ya kuwaaga Madaktari wanaomaliza muda wao na kuwakaribisha madaktari wapya kuhudumu kwa kipindi cha mwaka mmoja. Hafla hiyo ilifanyika Ubalozi mdogo wa China mjini Zanzibar
 Balozi mdogo wa China Xie Xiuowu akitoa hotuba yake katika Hafla maalum ya kuwaaga Madaktari kutoka China wanaomaliza muda wao na kuwakaribisha Madaktari wapya watakaohudumia wananchi kwa kipindi cha Mwaka mmoja. Hafla hiyo ilifanyika Ubalozi mdogo wa China mjini Zanzibar
 Waziri wa Afya Hamad Rashid akitoa hotuba yake katika Hafla maalum ya kuwaaga Madaktari kutoka China wanaomaliza muda wao na kuwakaribisha Madaktari wapya watakaohudumia wananchi kwa kipindi cha Mwaka mmoja. Hafla hiyo ilifanyika Ubalozi mdogo wa China mjini Zanzibar
 Kiongozi wa Timu ya Madaktari wa kutoka China waliomaliza muda wao wa kuhudumu katika sekta ya Afya Zanzibar akitoa neno la shukran katika hafla maalum ya kuagwa kwao na kukaribishwa kwa Madaktari wapya. Hafla hiyo ilifanyika Ubalozi mdogo wa China mjini Zanzibar
 Kiongozi wa Timu ya Madaktari wapya kutoka China Dkt.Yang Xiaodong akitoa nasaha zake katika hafla ya kuagwa na kukaribishwa kwa madaktari hao ambao watahudumu Zanzibar katikakipindi cha mwaka mmoja.
Baadhi ya Madaktari wa kutoka China waliohudhuria katika Hafla maalum ya kuwaaga Madaktari wanaomaliza muda wao na kukaribishwa kwa Madtari wapya watakaotoa huduma mbalimbali ikiwemo upasuaji na Kichocho. Hafla hiyo ilifanyika Ubalozi mdogo wa China mjini Zanzibar Picha na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad