HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, June 13, 2019

WAZIRI WA AFYA HAMAD RASHID AZUNGUMZA NA WAANDISHI WA HABARI ZANZIBAR

Na Ramadhani Ali – Maelezo
Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed amewataka wananchi kuendelea kuchangia damu kwa hiari kwani mahitaji ya damu salama nchini yamekuwa makubwa.

Amesema mahitaji ya damu kwa mwezi ni wastani wa chupa 1,550 kwa matumizi ya kawaida na watumiaji wakubwa ni mama wajawazito, watoto, wahanga wa ajali na wagonjwa wa upasuaji.

Akizungumza na waandishi wa Habari kuhusiana na siku ya wachangiaji damu duniani Ofisini kwake Mnazimmoja, Waziri Hamad alisema kutokana na wananchi wengi kuhamasika kutumia hospitali na vituo vya afya mahitaji ya damu yanaongezeka kwa kiasi.

Waziri wa afya alizipongeza taasisi na vikundi vya hiari vinavyojitokeza kuchangia damu kwa hiari katika mabonanza yanayoandaliwa na kitengo cha damu salama ambapo imekuwa msaada mkubwa katika hospitali na vituo vya afya.

Aliahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na taasisi za kijamii na vikundi mbali mbali vinavyojitolea kuchangia damu ili kuondosha tatizo la damu na kuokoa maisha ya wananchi.

Alisema lengo kuu la siku ya wachangia damu ni kuwapongeza, kuwajali na kuwahamasisha wachangiaji damu na kuwashajiisha wengine wapya ambao wanaweza kujitolea damu kwa hiari ili kuokoa maisha ya wengine.

Waziri wa Afya alikumbusha kuwa siku ya wachangiaji damu duniani ndiyo siku aliyozaliwa mvumbuzi wa makundi ya damu, Raia wa Australi Dr. Karl Landsteiner hivyo inapaswa kuenziwa.

Meneja Uhusiano na Uhamasishaji wa Kitengo cha damu salama Hamad Bakari Magarawa alisema maadhimisho hayo ambayo hufanyika kila ifikapo tarehe 14 ya mwezi Juni kila mwaka kwa Zanzibar yatafanyika Mwanakwerekwe.

Amesema maadhimisho hayo yanafuatiwa na Bonanza kubwa la kuchangia damu linalofanyika maeneo tofauti na wananchi wametakiwa kujitokeza katika mabonanza hayo na siku ya kilele kwa lengo la kuchangia damu.

Hamad Bakari Magarawa alisema Kaulimbiu ya siku ya wachangiaji damu duniani mwaka huu ni ‘’Damu kwa wote’’.
 Baadhi ya Waandishi wa Habari waliohudhuria katika mkutano wa Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohamed kuhusiana na Siku ya Wachangiaji Damu Duniani (WORLD BLOOD DONOR DAY)ambayo itafanyika siku ya Ijumaa 14/06/2019.hafla iliofanyika katika ukumbi wa Wizara hio Mnazi mmoja.
 Waziri wa Afya Hamad Rashid Mohamed akisisitiza jambo wakati akitoa hotuba yake mbele ya Waandishi wa Habari kuhusiana na Siku ya Wachangiaji Damu Duniani (WORLD BLOOD DONOR DAY)ambayo itafanyika siku ya Ijumaa 14/06/2019.hafla iliofanyika katika ukumbi wa Wizara hio Mnazi mmoja.
 Waziri wa Afya Hamad Rashid mohamed akitolea ufafanuzi baadhi ya maswala yalioulizwa na Waandishi wa Habari katika mkutano kuhusiana na Siku ya Wachangiaji Damu Duniani (WORLD BLOOD DONOR DAY)ambayo itafanyika siku ya Ijumaa 14/06/2019.hafla iliofanyika katika ukumbi wa Wizara hio Mnazi mmoja.
Meneja Uhusiano na uhamasishaji Damu Salama Hamad Bakar Magarawa akizungumza kuhusiana na Siku ya Wachangiaji Damu Duniani (WORLD BLOOD DONOR DAY)ambayo itafanyika siku ya Ijumaa 14/06/2019.hafla iliofanyika katika ukumbi wa Wizara hio Mnazi mmoja. PICHA NA YUSSUF SIMAI/MAELEZO ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad