Wazazi wanapaswa kutambua kuwa bado wataendelea kuwa na jukumu la
kuzaa na kulea suala ambalo kwa wakati huu wengi kati yao hujisahau
hasa katika ule mfumo wa asili wa malezi ya pamoja na badala yake kila
Mzazi huamua kulea Mtoto wake pekee.
Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi
alitoa kauli hiyo wakati akilifungua Baraza la Wazazi la Chama cha
Mapinduzi la Wilaya ya Mfenesini linalofanyika katika Ukumbi wa Chuo
cha Mwalimu Nyerere uliopo Bububu nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Mama Asha alisema hali ya ukosefu wa malezi ya pamoja kwa Watoto
imepelekea kuporomoka kwa maadili ya Watoto walio wengi katika Jamii
na matokeo yake wanashindwa kuwaheshimu Wazazi wa wenzao wakiona wa
kwao ndio wanaostahiki kupata Heshima hiyo.
Alisema Watoto wa sasa wameacha maisha mazuri yanayoongozwa na
Utamaduni wa Taifa na kuamua kufuata mila na Tamaduni za Ughaibuni
jambo ambalo limechangia kuporomoka kwa Maadili hasa wakiangaliwa
Watoto wenyewe vivazi na mienendo yao tayari imeshapoteza hadhi ya
Utamaduni wa asili.
Mke huyo wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alielezea masikitiko
yake kutokana na vitendo vya udhalilishaji vilivyoshamiri katika
mitaa mbali mbali Nchini ambavyo kwa mtazamo wa matukio hayo, maadili
tayari yameshapoteza muelekeo kutokana na jamii ya sasa kukosea njia
sahihi ya kuelekea.
Mama Asha alisema tabia ya kupigwa kwa Wanawake na Watoto hadi
kuumizwa na wakati mwengine kuchomwa moto Watoto kwa makosa madogo
madogo pamoja na kutelekezwa ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya
udhalilishaji wa makundi hayo.
Alieleza kwamba ni ukweli usiofichika kwamba wanaoendeleza vitendo
hivyo ambavyo ni vya kinyama na aibu kwa Jamii yenye kufuata mila,
silka, desturi na Utamaduni wa Watu wastaarabu ni wale waliokosa
malezi ingawa wanaelewa fika ubaya wanaoufanya.
Mama Asha aliwataka Wazazi na Viongozi wa ngazi na nyanja zote pamoja
na Wananchi wote kuchukuwa tahadhari kwa kuwa karibu na familia zao
ili kila mmoja kwa nafasi yake ailinde Jamii kwa kukemea vitendo hivyo
viovu vyenye kutia aibu.
Aliwakumbusha Viongozi wa Jumuiya ya Wazazi kwamba bado wana jukumu
kubwa la kutoa elimu, kusimamia malezi bora ya Watoto na kuhakikisha
kwamba mazingira ya Mitaa yanaimarika ipasavyo ili kuwa na Jamii yenye
ustawi na umakini mkubwa.
Akigusia janga la Dawa za kulevya Nchini ambalo huwakumba zaidi Vijana
wanaotarajiwa kuwa Viongozi wa Taifa la kesho Mama Asha alisema jamii
bado inapaswa kukemea utumiaji wa Dawa hizo ambazo ni janga
linaloendelea kuikumba Dunia na hatimae kuathiri Mataifa mengi
Ulimwenguni.
Mama Asha aliwanasihi Wananchi kwa kushirikiana na Viongozi wao ni
vyema wakashiriki kikamilivu katika mapambano dhidi ya kupiga vita
vitendo hivyo kwa kuwafichua wahalifu wanaoingiza, kusambaza na
watumiaji kwa vile madhara yake huwagusa hata wale wasiohusika kwa
kukumbwa na vitendo vya ajabu.
Alizikumbusha Taasisi zinazohusika na udhibiti wa Dawa za kulevya
kuendelea kuimarisha mashirikiano na Serikali pamoja na wadau wengine
wa Kitaifa na kimataifa ili kuona wimbi hili la Dawa za hatari
linakomeshwa au kupunguzwa kwa kiasi kikubwa.
Mama Asha alishauri katika kukabiliana na janga hilo ni budi
kuanzishwa kwa vituo vya Maandalizi katika kila Tawi la Chama cha
Mapinduzi, kuimarisha Vijana kuwa Chipukizi na kuendeleza madarasa ya
Itikadi ya Jumuiya ili kulea, kusimamia na kuwafundisha Vijana Maadili
mema ya Chama cha Mapinduzi na Jumuiya zake.
Akigusia masuala ya uchumi ndani ya Jumuiya Mama Asha aliutaka Uongozi
wa Jumuiya hiyo ya Wazazi kuhakikisha kwamba Wawekezaji
wanaoshirikiana nao wanazingatia Maadili, Heshima na Uzalendo wa
Taifa.
Alisema wapo baadhi ya Viongozi hudiriki kuiua Miradi ya Uwekezaji kwa
sababu ya kukoza asilimia Kumi ya Mradi jambo ambalo ni miongoni mwa
vitendo vya Ruishwa vinavyodumaza maendeleo ya Jumuiya pamoja na Taifa
kwa Ujumla.
Aliwapongeza Wajumbe wa Baraza la Wazazi la Wilaya ya Mfenesini kwa
umahiri wao wa kutekeleza Kanuni ya Jumuiya yao Kifungu cha 60{2}
kinachotaka kufanyika Vikao kila miezi Sita ili Wajumbe wapate fursa
ya kujadili masuala yao yenye mustakabal na Jumuiya pamoja na Chama
chenyewe.
Alisema kwa vile Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi ni kongwe
iliyoasisiwa mnamo Mwaka 1955 tokea wakati wa enzi za Vyama vya TANU
na ASP ikiwa ni miongoni mwa mihimili ya Ukombozi lazima ienziwe,
itunzwe na kuthaminiwa ili iendelee kulea na kupata maendeleo mema
yatakayokikidhi ustawi na maeneleo ya Jamii yote Nchini.
Akitoaa Taarifa fupi ya Utekelezaji wa majukumu ya Jumuiya ya Wazazi
Wilaya ya Mfenesini, Katibu wa Jumuiya Hiyo Bibi Biubwa Jabir alisema
yapo mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kazi za Jumuiya hiyo
ndani ya kipindi cha Miezi Sita iliyopita.
Bibi Biubwa alisema Viongozi wa Jumuiya hiyo bado wanaendelea
kusimamia Jukumu lao la kuwajenga Vijana katika muelekeo wa kukua
kimaadili wakizingatia kwamba Elimu ndio msingi imara wa kufanikisha
majukumu hayo muhimu kwa Taifa.
Alisema kazi iliyopo mbele ya Viongozi hao ni kuunganisha nguvu katika
kuhamasisha Wazazi waelekeze juhudi zao kwenye Utekelezaji wa Sera na
Malezi bora kwa Watoto ili kuwa na Jamii iliyostawi Kimaadili.
Hata hivyo Katibu huyo wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mfenesini
alisema zipo changamoto zinazokwaza ufanisi wa kazi wa Jumuiya
akizitaja baadhi kuwa ni pamoja na ukosefu wa Fotokopi, Mashine, Fedha
kwa ajili ya kuanzisha Mradi wa Ufugaji Nyuki, ushakavu wa Mabweni wa
Skuli ya Wazazi Dole inayokwenda sambamba na ukosefu wa Gari kwa ajili
ya Wanafunzi.
Naye kwa upande wake akitoa salamu Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya
Wazazi wa CCM Zanzibar Nd. Othman Ali Maulid alisema kuanzia sasa
Kiongozi au Mdau ye yote anayeamua kuchangia au kusaidia shughuli za
Chama na Jumuia zake lazima kuwepo kumbu kumbu kamili.
Nd. Othman alisema hatua hii ina lenga kujiepusha na vitendo vya
Rushwa wakati Taifa likikaribia kuelekea katika Chaguzi za Serikali za
Mitaa kwa upnade wa Tanzania Bara na Uchaguzi Mkuu Mwaka ujao.
Alisema wapo Watu wakiwemo baadhi ya Viongozi wanaoutumia udhaifu wa
baadhi ya changamoto zinazokuwepo Kwenye Taasisi za Chama kwa kutoa
Misaada kwa muekeo wa kujinyooshea njia ya kupata madaraka na baadae
kujinufaisha kibinafsi.
Mkutano huo wa Wajumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha
Mapinduzi {CCM} Wilaya ya Mfenesini umejadili Utekelezaji wa Majukumu
yake ndani ya Kipindi cha Miezi Sita iliyopita na kupanga Mikakati ya
Utekelezaji kwa Kipindi chengine cha Miezi Sita Ijayo.
Mke
wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi
akisindikizwa na Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi Zanzibar Nd.
Othman Ali Maulid kuingia katika Ukumbi wa Chuo cha Kumbukumbu ya
Mwalimu Nyerere kufungua Baraza Kuu la Jumuiya hiyo Wilaya ya Mfenesini.
Mke
wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi
akilifungua baraza la Jumuiya ya Wazazi wa CCM Wilaya ya Mfenesini.
Baadhi
ya Wajumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mfenesini na
Mikoa wa Magharibi na Mjini wakifuatilia ufunguzi wa baraza la Jumuiya
ya Wazazi wa CCM Wilaya ya Mfenesini.
Katibu
wa Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mfenesini Bibi Biubwa Jabiri akitoa
Taarifa fupi ya utekelezaji wa kazi ndani ya kipindi cha Miezi Sita.
Naibu
Katibu Mkuu wa Jumuiya Wazazi Zanzibar Nd. Othman Ali Maulid akitoa
salamu wakati akimkaribisha Mgeni rasmi kuufungua Mkutano wa Baraza Kuu
la Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mfenesini.
Mama Asha akimkabidhi mchango wake Katibu wa
Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Mfenesini Bibi Biubwa Jabiri mara baada ya
kuufungua Mkutano wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya
Mfenesini Ukumbi wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Bububu.
Picha na – OMPR – ZNZ.
No comments:
Post a Comment