Na Stella Kalinga, Simiyu
Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias
Andengenye ameliagiza Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, kuendelea kufanya
ukaguzi wa kinga na tahadhari ya moto kwa shule zote za sekondari
za mabweni nchini kujiridhisha ikiwa vigezo vimezingatiwa, kwa lengo
la kuepusha majanga ya moto yanayogharimu maisha ya watu na mali.
Andengenye ametoa maagizo hayo Juni 19, 2019 Mkoani Simiyu wakati
akizungumza na wanafunzi wa baadhi ya shule za msingi na sekondari za
Mjini Bariadi katika shule ya sekondari Simiyu, katika Halmashauri ya
Mji wa Bariadi.
Akizungumza na wanafunzi Kamishina Jenerali Thobias Andengenye amesema
kumekuwa na matukio ya moto katika shule kadhaa za bweni ambayo
yameleta athari mbalimbali ikiwa ni pamoja na kusababisha vifo kwa
wanafunzi, kuteketea kwa mali, hivyo jeshi la zimamoto na uokoaji
linaendelea kuweka mikakati ya kukabiliana na majanga hayo.
Amesema mikakati hiyo ni pamoja na kusogeza huduma za zimamoto karibu
na wananchi kufanya ukaguzi wa tahadhari na kinga ya moto katika
majengo, kusoma ramani za majengo na kuanzisha klabu za zimamoto
katika shule, ili kuwajengea wanafunzi uwezo wa kujua vitu vya kufanya
na vya kuepuka na uwezo wa kukabili moto katika hatua za awali na
kuuzima.
Katika hatua nyingine Andengenye amewataka wamiliki wa shule
kuzingatia ushauri wa kitaalam unaotolewa na wataalam wakati wa
ukaguzi juu ya namna ya kufanya mabweni , madarasa na ofisi ziwe
salama kwa kuwasilisha michoro ya majengo hayo katika Ofisi za
Zimamoto ili ushauri wa kitaalam uweze kutolewa.
“Niwaombe wanaomiliki shule wazingatie ushauri wa kitaalam unaotolewa,
wazingatie ujenzi unaofuata ushauri wa kitaalaam kwa kuwasilisha
michoro kama wanataka kujenga mabweni, kuongeza madarasa au kuongeza
vyumba vya ofisi basi wazingatie ushauri ili majengo yanayojengwa yawe
salama zaidi” alisema.
Aidha, amewaasa wananchi kuacha kuweka mitungi ya gesi ndani na
kutikisa mitungi ya gesi kama njia ya kufahamu kiasi cha gesi
kilichopo; kwa kuwa kunaweza kusababisha moto na kushauri kuwa njia
sahihi ya kupima kiasi cha gesi katika mtungi ni kuweka mtungi katika
maji, ambapo baada ya kuutoa sehemu isiyo na gesi itaonekana kuwa
kavu.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema kumekuwa na
mwamko mkubwa wa watu kutumia gesi, hivyo ameshauri Jeshi la Zimamoto
na uokoaji kuendelea kutoa elimu katika mikusanyiko ya watu na kupitia
vyombo vya habari kuhusu dhana ya matumizi sahihi ya gesi ili kuepusha
majanga ya moto.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga
amelishukuru Jeshi la Zimamoto na uokoaji kutoa elimu kwa wanafunzi na
akawataka wanafunzi wote waliopata elimu hiyo kuwa mabalozi katika
maeneo yao wanayoishi.
Magreth Sonda mwanafunzi wa kidato cha pili shule ya sekondari Simiyu
ameshukuru kupata elimu ya tahadhari na kinga dhidi ya moto na kuahidi
kuwa yeye pamoja wanafunzi wenzake watakuwa mabalozi wa kueneza elimu
hiyo kwa jamii inayowazunguka ili kuepusha majanga ya moto ambayo yana
athari nyingi ikiwemo vifo na kuteketea kwa mali.
Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye akiweka kizimia moto katika moja ya vyumba vya madarasa katika shule inayotarajiwa kuwa shule ya wanafunzi wenye vipaji vya michezo Simiyu Sekondari, wakati wa ziara yake Mjini Bariadi Mkoani Simiyu, Juni 19, 2019.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (kushoto) akimtambulisha Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye kwa baadhi ya wanafunzi wa shule za msingi na sekondari za Mjini Bariadi kabla ya kuzungumza nao juu ya kinga na tahadhari ya majanga ya moto wakati wa ziara yake mkoani Simiyu, Juni 19, 2019.
Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka wakiwasha moto kwa ajili ya kuwaonesha wananchi namna ya kuzima moto pindi moto unapotokea, wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu, Juni 19, 2019.
Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye akizungumza na wanafunzi wa baadhi ya shule za msingi na sekondari za Mjini Bariadi, kuhusu tahadhari na kinga dhidi ya majanga ya moto,wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu Juni 19, 2019.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(kulia) akimuongoza Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye kukagua moja ya mabweni yanayojengwa katika Shule ya Sekondari ya Simiyu, wakati alipotembelea shule hiyo na kuzungumza na wanafunzi wa baadhi ya shule za msingi na sekondari za Mjini Bariadi, kuhusu tahadhari na kinga dhidi ya majanga ya moto,wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu Juni 19, 2019.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(kulia) akimuongoza Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye kukagua moja ya mabweni yanayojengwa katika Shule ya Sekondari ya Simiyu, wakati alipotembelea shule hiyo na kuzungumza na wanafunzi wa baadhi ya shule za msingi na sekondari za Mjini Bariadi, kuhusu tahadhari na kinga dhidi ya majanga ya moto,wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu Juni 19, 2019.
Askari wa jeshi la Zimamoto na uokoaji mkoa wa Simiyu, akimuelekeza mmoja wa wanafunzi namna ya kuzima moto wakati wa ziara ya Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina Jenerali Thobias Andengenye katika shule ya Sekondari Simiyu, wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu Juni 19, 2019.
Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini Kamishina
Jenerali Thobias Andengenye(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na
wajumbe wa kamati ya Ulinzi naUsalama ya Mkoa wa Simiyu wakati wa
ziara yake Mkoani hapa Juni 19, 2019.
No comments:
Post a Comment