HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, June 24, 2019

NAIBU WAZIRI MGALU AWASHA UMEME NJOPEKA MKOANI PWANI

Na Veronica Simba - Pwani
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, jana Juni 23, 2019 alikiwashia rasmi umeme kijiji cha Njopeka kilichopo wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani. Aliwasha umeme huo kwenye Duka la Abdul Abdulrahman, ikiwa ni ishara ya kukiwashia kijiji kizima.

Kabla ya tukio la kuwasha umeme, Naibu Waziri alizungumza na wananchi wa eneo hilo ambapo aliuagiza uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha wanafikisha umeme katika Mradi wa Maji kijijini hapo ili kutatua changamoto hiyo kwa manufaa ya wakazi wake.

“Hili siyo jambo la Wizara ya Maji; ni la Wizara ya Nishati. Nishati tumepewa dhamana ya kuboresha na kuhakikisha huduma nyingine za kijamii zinatolewa katika viwango vyenye ubora,” alisema.

Akizungumzia mikakati ya serikali kufikisha umeme katika maeneo yote nchini; Naibu Waziri Mgalu alisema kuwa matarajio ni kuvifikishia nishati hiyo vijiji 10,268 nchi nzima ifikapo Juni 2020, vikiwemo vijiji vipya 60 vya Wilaya ya Mkuranga.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri alitoa wito kwa wafanyakazi wa TANESCO katika Ofisi za Wilaya nchi nzima, hususan Kada ya Maafisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja, kuongeza bidii na weledi katika kutekeleza majukumu yao.

Alisema Kada hiyo inawajbika kufanya kazi kwa kujituma, kuhakikisha wanawafuata wateja mahala waliko kwa ajili ya kuwapelekea taarifa mbalimbali pamoja na kupokea kero zao.

Aidha, alisema watumishi hao wanatakiwa kuachana na utamaduni wa kukaa ofisini, badala yake watoke kwenda kutafuta wateja ili kuliongezea shirika mapato.

Taarifa ya TANESCO kuhusu utekelezaji wa miradi ya umeme wilayani humo inaeleza kuwa, mpaka sasa kazi ya kusambaza umeme imekamilika katika vijiji vyote 15 na kwamba kazi inayoendelea hivi sasa ni kuunganisha wateja,

Vijiji hivyo ni Kinyanya, Jaribu Magharibi, Lumionzi, Mjawa, Ngodai, Mangombela, Bungu A na Bungu B. Vingine ni Motomoto, Tomoni, Kingwila, Mtunda, Kinyamale, Mtawanya kwa Mkengelwa, Bungu Mwongozo na Njopeka.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Njopeka, wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani, kabla ya kuwasha rasmi umeme katika Kijiji hicho Juni 23, 2019.
Mmoja wa wananchi wa Kijiji cha Njopeka, wilayani Mkuranga, Mkoa wa Pwani akitoa mchango wake kuhusu sekta ya umeme, mbele ya Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (hayupo pichani), aliyefika kijijini hapo kuwasha rasmi umeme Juni 23, 2019.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad