Wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wameungana na wenzao
duniani kushiriki maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani ambayo
hufanyika Mei Mosi kila mwaka.
Wafanyakazi wa MNH walianza maandamano katika hospitali hii kuelekea
Uwanja wa Uhuru ambako wameungana na wenzao kutoka taasisi mbalimbali
jijini Dar es Salaam kuadhimisha siku hii muhimu kwa wafanyakazi
nchini na duniani kote.
Katika kuadhimisha siku hii wafanyakazi wametakiwa kufanya kazi kwa
bidii ili kujenga uchumi imara, huku kauli mbiu ikiwa ni, “Utawala
bora ni kwa maendeleo ya nchi.”
Mgeni rasmi katika maadhimisho haya, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Paul Makonda amesema ongezeko la mshahara ni moja ya jambo muhimu kwa
wafanyakazi na kwamba linamgusa kila mmoja. Pia, ametaka kuwapo kwa
usalama mahala pa kazi ili kuondoa hofu kwa wafanyakazi.
“Naomba suala la usalama na afya katika sehemu ya kazi lizingatiwe,
pia nawaomba viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam kufuatilia usalama na
afya mahala pa kazi, niwaombe viongozi wanipatie taarifa ni kampuni
zipi hazipeleki michango ya wafanyakazi katika mifuko ya hifadhi. Hili
lifuatiliwe ili kuondoa kero kwa wafanyakazi.”
Pia, amewapongeza wafanyakazi mbalimbali kwa utumishi bora kwani
wamekuwa wakifanya kazi nzuri licha ya kuwapo kwa changamoto
mbalimbali.
Makonda pia amewapongeza walimu kwa kazi nzuri wanayofanya na
amewaleza Watanzania kwamba walimu wanaowajenga watu hasa wanafunzi
kufikia mafanikio mazuri katika maisha.
Baadhi ya wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwa kwenye maandamano ya kuadhimisha siku ya wafanyakazi duniani ambayo hufanyika Mei Mosi kila mwaka.
Maandamano yakiendelea jijini Dar es Salaam ambako wafanyakazi mbalimbali wameshiriki leo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha siku ya wafanyakazi duniani.
Baadhi ya wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwa katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam ambako wameshiriki maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani pamoja na wenzao kutoka taasisi na kampuni mbalimbali jijini Dar es Salaam.
Maandamano yakiendelea karibu na Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam katika barabara ya Taifa.
Wafanyakazi wa Muhimbili wakiwa na wenzao kutoka taasisi
mbalimbali wakishiriki kwenye maandamano leo jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment