Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,
Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile ametoa rai kwa viongozi wa Kisiasa hapa
nchini kuacha kuingilia kazi za Kitaaluma katika sekta ya Afya na
kuwaomba wawaache wataalam wafanye kazi zao kwa misingi na miiko ya
Kitaaluma inayowaongoza.
Dkt. Ndugulile ameyasema hayo katika Maadhimisho ya Siku ya Wakunga
Duniani yaliyofanyika Kitaifa katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa
Bariadi, chini ya Kauli Mbiu “Wakunga Watetezi wa Haki za Wanawake”,
ambapo alikuwa akimwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Amesema hivi karibuni kumekuwa na matamko yanayotolewa na baadhi ya
viongozi wa kisiasa yanayowakatisha tamaa watumishi wa sekta ya afya
na baadhi ya viongozi wameanza kuingilia masuala ya kitaalum, hivyo
akawaomba ikiwa viongozi hao watakutana na changamoto za watendaji wa
afya waishirikishe wizara ya afya ili wachukuliwe hatua kwa mujibu wa
taaluma zao.
“Niwaombe sana viongozi wa Serikali na Viongozi wa vyama, masuala ya
kitaaluma yanashughulikiwa kitaaluma kama kuna changamoto na
wanataaluma ndiyo maana tuna mabaraza ya taaluma na ndiyo maana sisi
wizara tupo mtushirikishe, nimelisema hili kwa sababu nimeona sekta
imeanza kuingiliwa” alisema Dkt. Ndugulile.
Aidha, Dkt. Faustine Ndugulile amewataka wakunga hapa nchini kuendelea
kuzingatia miiko na misingi ya taaluma yao katika huduma wanazotoa kwa
jamii na kuahidi kuwa Serikali haitasita kuwachukulia hatua wale wote
watakaokiuka misingi hiyo kwa kuwa jamii inahitaji heshimu, utu,
upendo na kutiwa moyo
Katika hatua nyingine Dkt. Ndugulile ametoa wito kwa wadau mbalimbali
wa maendeleo na jamii kwa ujumla kuendelea kushirikiana na Serikali
katika kuboresha huduma za afya ili changamoto ya vifo vitokanavyo na
uzazi vibaki kuwa historia ambapo amesema kwa sasa wanawake 11,000
wanakufa kila mwaka kutokana na uzazi.
Rais wa Chama cha Wakunga Tanzania, Bibi. Feddy Mwanga ameiomba
Serikali kuongeza idadi ya wakunga ili mkunga aweze kutoa huduma kwa
kiwango kinachokubalika Kitaifa na kimataifa huku akisisitiza Serikali
kuona haja ya kujenga nyumba za wakunga katika vituo vyote vya kutolea
huduma za afya vinavyoboreshwa na vinavyojengwa.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga ambaye
alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthoy Mtaka amemshukuru
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli
kwa kutoa shilingi bilioni saba fedha kwa ajili ya ujenzi wa
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na shilingi bilioni 4.5 kwa ajili ya ujenzi
wa Hospitali tatu za Wilaya Bariadi, Busega na Itilima ambazo ujenzi
wake unaendelea vizuri.
Aidha, Kiswaga ameshukuru Shirika la Umoja wa Mataifa
linaloshughulikia idadi ya watu Duniani(UNPFA) kwa namna
linavyoshirikiana na Serikali mkoani Smiyu kwa kukarabati baadhi ya
vituo, kununuaa vifaa mbalimmbali, kutoa mafunzo kwa wakunga jitihada
ambazo zimechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo vitokanavyo na
uzazi.
Akitoa taarifa ya Mkoa, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne
Sagini amesema
Idadi ya wakunga katika vituo vya kutolea huduma za afya Simiyu
imeongezeka hali iliyofanya wajawazito wengi kujifungulia katika vituo
vya afya kutoka asilimia 62 mpaka asilimia 68, hivyo vifo vya mama
wajawazito vimepungua kutoka vifo 48 mwaka 2017 mpaka vifo 40 mwaka
2018.
Naye Makamu Mwakilishi Mkaazi wa UNFPA hapa nchini, Dkt.Hashina Begum
amesema kwa kushirikiana na Chama cha Wakunga nchini (TAMA) limetoa
mafunzo kwa wakunga 90 kutoka katika vituo vilivyoboreshwa ili
kuwasaidia wakina mama wajawazito na watoto kupata huduma za dharura
na kupunguza vifo kwa mama na mtoto vitokanavyo na uzazi.
Grace Magengeni Mkunga kutoka Jijini Dodoma amesema” siku yetu imefana
tunashukuru hotuba ya Naibu Waziri imetutia moyo katika kuwahudumia
wanawake na watoto, nawashauri wenzangu tusimamie taaluma zetu tufanye
kazi kwa bidii naamini hao wanaotuingilia majukumu yetu wataachaa
maana ni kweli, tunashukuru Naibu Waziri kulisemea hili suala”
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (kulia ) akipokea maelezo kutoka kwa mmoja wa wakunga ya namna wanavyowahudumia wakina mama wajawazito na watoto wakati alipotembelea Banda la Chama cha Wakunga Tanzania(TAMA), katika Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo yamefanyika Kitaifa katika Uwanja wa Bariadi Mkoani Simiyu.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (kulia ) akiangalia baadhi ya vitabu vinvyotuika kutoa elimu kwa wananchi wakati alipotembelea banda la maonesho la Shirika lisio la kiserikali la AGPAHI, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo yamefanyika Kitaifa katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mkoani Simiyu.
Baadhi ya wakunga wakiwa katika maandamano wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo yamefanyika Kitaifa Mei 05, 2019 katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mkoani Simiyu.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile akimkabidhi mmoja wa kunga wa moa wa Simiyu cheti kama zawadi ya kufanyakazi nzuri, katika Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo yamefanyika Kitaifa katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mkoani Simiyu.
No comments:
Post a Comment