HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, April 5, 2019

Waziri Biteko akutana na kufanya mazungumzo na Wadau mbalimbali wa Madini

Na Issa Mtuwa, Dodoma
Waziri wa Madini Doto Biteko amekutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na makundi mbalimbali ya wadau wa madini    Aprili 3, 2019, Ofisini kwake Jijini Dodoma.
Miongoni mwa aliokutana nao ni pamoja na Kampuni ya MAGAL Security System inayojihusisha na ufungaji wa mitambo ya usalama (security system) katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya migodini.
Mkurugenzi wa Biashara na Uendelezaji wa Masoko wa kampuni hiyo, Michael Gur Arie, amemweleza Waziri kuwa, kampuni yake inataka kufanya kazi na Wizara ya madini katika masuala ya ufungaji wa mitambo ya usalama kwenye migodi hususani Mirerani.
Amesema kuwa, kampuni hiyo ina uwezo wa kufunga mitambo Mirerani na wizara ikawa na uwezo wa kufuatilia kinacho fanyika kwenye eneo lote la mgodi huku shughuli nyingine za ofisi zikiendelea.
Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Biteko ameishukuru kampuni ya MAGAL kwa kumtembelea na kuzungumza nae kuhusu suala la usalama hususani Mirerani. Amesema suala la usalama mirerani linapewa kipaumbele na uzito mkubwa katika kulinda raslimali hiyo ili iwanufaishe Watanzania wote.
Ameongeza kuwa, serikali imelipa kipaumbele suala la usalama katika eneo la Mirerani na Wizara imekuwa na mpango wa awamu mbili katika kutekeleza suala hilo. Amesema, Awamu ya kwanza ilikuwa ni kujenga ukuta kuzunguka eneo lote la migodi ya Mirerani na kufunga kamera na awamu ya pili inasubiri ushauri wa namna ya kutekeleza huku utekelezaaji wake ukitarajiwa kutafanyika baada ya kupitishwa kwa Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pia, waziri Biteko amekutana na Viongozi wa Shirikisho la Wachimbaji Wadogo Nchini (FEMATA) wakiongozwa na Rais wa Shirikisho hilo, John Bina.
Bina na ujumbe wake wamemtembelea Waziri Biteko kwa lengo la kukutana na kuzungumzia masuala mbalimbali yanayohusu shirikisho hilo ukizingatia kwamba, tangu ateuliwe kushika wadhifa huo hawajawahi kukutana na kufanya mazungumzo rasmi zaidi ya kukutana kwenye ziara mbalimbali.
Pamoja na mambo mengine, Bina amemweleza Waziri kuwa, Shirikisho lina laani vikali tukio la udanganyifu uliotokea hivi majuzi huko Chunya na kuongeza kwamba, FEMATA haikubaliana na udanganyifu unaofanywa na wachimbaji kwa kushirikiana na baadhi watendaji wa serikali waliopewa dhamana na kwamba halipo tayari kuwalinda wala kuwateteta.
Pia, Bina amezungumzia kuhusu Mgodi wa Buhemba uliofungwa na serikali akimuomba waziri kuufugua mgodi huo kwani  wanachi wengi walio katika eneo hilo wanategemea maisha yao  kutokana na uwepo wa mgodi huo.
Aidha, amemwomba Waziri maeneo mbalimbali yanayochukuliwa na serikali, afikirie kuwapatia wawekezaji wazawa ili wayaendeleze kwa  shughuli za uchimbaji. Bina ameongeza kuwa, FEMATA ina mpango wa kuanzisha Benki ya Wachimbaji (Miners Bank) kwa ajili ya kuwahudumia wachimbaji nchini.
Kwa upande wake, Waziri Biteko amemshukuru Rais wa FEMATA na ujumbe wake kwa kumtembelea. Amesema FEMATA na Wizara ya Madini huwezi kutenganisha kwa kupiga mstari kwa kuwa watu wa FEMATA ndio wadau wa wizara na kwamba hawajawahi kutofautiana na  kuomba ushirikiano huo uendelee.
Vilevile, Biteko amewashukuru FEMATA kwa kuunga mkono na kulaani kitendo cha udanganyifu uliofanywa na wachimbaji kwa kushirikiana na watendaji wa wizara huko Chunya kwa kutoa taarifa za uongo kuhusu uzalishaji wa madini.
Kuhusu kufunguliwa kwa mgodi wa Buhemba, Biteko amesema Wizara ina thamini maisha ya watu kuliko shuguli za uchimbaji na kuongeza kwamba hivi sasa kuna timu ya wataalamu ambao wamekwenda  Buhemba kufuatilia utekelezaji wa  waliyokubaliana katika kikao cha tarehe  6 Machi, 2019, na ripoti  hiyo inategemewa kuwa mwongozo wa iwapo mgodi huo ufunguliwe au ufungwe.
Akizungumzia kuhusu uanzishwaji wa Benki ya Wachimbaji amesema ni jambo zuri na kushauri kuanza na SACCOS ili kupima imani ya uaminifu wa wanchama wake katika kurejesha amana watakazo kuwa wanakopa.
Waziri Biteko amewahakikishia FEMATA kuwa wizara yake itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake.
 Waziri Doto Biteko akitoa ufafanuzi wa mambo mbalimbali kwa Michael Gur Arie, Mkurugenzi wa Biashara na Uendelezaji wa Masoko  wa Kampuni ya MAGUL Security System wa kwanza kushoto kwa Waziri alie ambatana na Idan   Segev wa kwanza kulia walipo mtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma kwa mazungumzo.
 Waziri Doto Biteko katikati akiwa katika picha ya pamoja na Michael Gur Arie, Mkurugenzi wa Biashara na Uendelezaji wa Masoko  wa Kampuni ya MAGUL Security System kulia na kushoto ni Idan   Segev  afisa masuala ya Biashara na Mauzo wa kampuni hiyo.
 Waziri Doto Biteko akimsikiliza Rais wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA), John Bina kulia wakati wa mazungumzo yao ofisini kwake Dodoma. Kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho hilo amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega.
 Waziri Doto Biteko akiongea na Viongozi wakuu wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA) wakati wa mazungumzo yao ofisini kwake Dodoma. Kulia  ni Rais wa Shirikisho hilo John Bina na kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega.
Waziri Doto Biteko katikati akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA) walipo mtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma kwa mazungumzo. Kulia  kwake ni Rais wa Shirikisho hilo John Bina na kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho hilo amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad