HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, April 30, 2019

TIMUN 2019 YAANZA RASMI MORO

MKUTANO kivuli wa Baraza la Umoja wa mataifa (TIMUN2019) umeanza Jana tarehe 29/4/2019 katika mji wa Morogoro, kiasi cha kilometa 192 kutoka mji wa kibiashara wa Dar es salaam.

Mkutano huo ambao unahudhuriwa na vijana 200 kutoka duniani kote unafanyika chini ya kaulimbiu "Sauti za Vijana kwenye Malengo ya Maendeleo Endelevu: Uwezeshwaji Ujumuishwaji na Usawa."

Afisa wa Habari katika kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa (UNIC)  Bi. Nafisa Didi akizindua rasmi mwanzo wa mkutano kwa niaba ya Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa alihimiza vijana kutumia vizuri muda wao katika mkutano huu wa siku tano na kuonyesha vipaumbele vinne muhimu vya kujadiliwa kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu ya dunia (SDGs).

Mkutano huo mkubwa unaendeshwa kwa mfano wa mfumo wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kisheria na kikanuni. Mkutano huo unatambuliwa kimataifa kama Tanzania International Model United Nations (TIMUN) 2019 unajumuisha vijana kuanzia miaka 15-30.

Kwa mujibu wa taarifa majadiliano katika mkutano huo yatalenga zaidi ushiriki wa vijana katika kipengele cha tatu cha SDG kinachogusa Afya na ustawi; Kipengele cha nane kazi zenye staha na ukuaji wa uchumi; kipengele cha 13 mabadiliko ya tabia nchi na kipengele cha 16 cha amani, haki na kuwa taasisi zenye uwezo .

TIMUN  inaendeshwa na Vijana wa Umoja wa Mataifa (YUNA), na hufanyika kila mwaka kwa vijana kuletwa pamoja kutoka mataifa mbalimbali duniani .

Tukio la mwaka huu limedhaminiwa na Umoja wa Mataifa Dar es salaam, ofisi ya Waziri Mkuu, UNICEF, UNFPA, UNIC, Ubalozi wa Marekani, Pathfinder, Plan International na International Youth Foundation.
Mratibu wa TIMUN 2019, Kevin Edward akitoa neno la ukaribisho kwa washiriki (hawapo pichani) wakati wa mkutano kivuli wa Baraza la Umoja wa Mataifa (TIMUN2019) ulioanza kuunguruma jana mjini Morogoro.
Afisa wa Habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa (UNIC) Bi. Nafisa Didi akifungua rasmi mkutano wa kivuli WA Baraza la Umoja wa Mataifa kwa niaba ya Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa ulioanza kuunguruma jana mjini Morogoro.
Baadhi ya vijana wanaoshiriki mkutano kivuli wa Baraza la Umoja wa Mataifa (TIMUN 2019) kutoka nchini mbalimbali unaoendelea kuunguruma mjini Morogoro.
Picha ya pamoja ya makundi ya vijana wanaoshiriki mkutano kivuli wa Baraza la Umoja wa Mataifa unaoendelea kuunguruma mjini Morogoro.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad