HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 29, 2019

Dkt Kalemani azindua uunganishaji wa Gesi ya asilia Kiwanda cha Cocacola

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani, akikata utepe kuashiria kukiunganishia Gesi asilia kiwanda cha Cocacola cha jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Profesa Sufian Bukurura.

Na Teresia Mhagama

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani amezindua upelekaji wa Gesi asilia katika kiwanda cha Cocacola kilichopo jijini Dar es Salaam ambacho sasa kitaanza kutumia gesi hiyo kwa shughuli zake za uzalishaji.

Uunganishaji wa Gesi asilia katika kiwanda hicho ni matokeo ya kazi iliyofanywa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) katika mwaka wa fedha 2018/2019 ya kuunganisha bomba la kusafirisha gesi asilia  linalotoka Mtwara na Songo songo hadi Dar es Salaam kwenye bomba la usambazaji gesi asilia linalotoka Ubungo hadi Mikocheni  jijini Dar es Salaam.

Dkt Kalemani alifanya uzinduzi huo tarehe 28 Aprili, 2019 ambapo pia amekagua shughuli za usambazaji gesi majumbani katika eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Mikocheni na Savey.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya uzinduzi huo alisema "yapo mabomba manne yanayotumika kwa shughuli hizi za usambazaji gesi hivyo ni matumaini ya Serikali kuwa viwanda vingi zaidi vitatumia gesi hii kwa shughuli za uzalishaji ili kuleta tija kwenye  gesi, kupunguza gharama za uendeshaji wa viwanda  na pia kwa ajili ya utunzaji wa mazingira."

Kuhusu kupitisha miundombinu ya usambazaji gesi katika maeneo ambayo hayajapimwa, Dkt Kalemani aliitaka TPDC na kampuni yake tanzu ya Usambazaji Gesi (GASCO) kuhamasisha viongozi wa mitaa na wananchi ili kuitikia wito wa kupitisha miundombinu hiyo kwenye maeneo yao hivyo kuunganishia gesi wananchi wengi zaidi.

Aidha, aliagiza kuwa, zaidi ya robo ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wasambaziwe Gesi Asilia katika miaka mitatu ijayo na kueleza kuwa kuna umuhimu kwa vyombo vya usafiri kama magari, majumbani na viwanda kutumia gesi hiyo ambapo kwa sasa magari zaidi ya 200 yameunganishwa na gesi hiyo nchini.

Pia alisisitiza matumizi ya vifaa vinavyozalishwa nchini katika kazi za usambazaji wa gesi kama vile mabomba na viunganishi ili kutochelewesha kazi hizo, kuepusha usumbufu na kupunguza gharama katika usambazaji gesi asilia.

Kuhusu bajeti ya usambazaji gesi asilia,  alisema kuwa Serikali inalipa kipaumbele suala hilo na imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kazi hizo ambapo kwa sasa imetenga zaidi ya shilingi bilioni 50 kwa ajili ya mradi huo.

katika ziara hiyo, Waziri wa Nishati aliambatana Kaimu Kamishna wa Petroli na Gesi, Mwanamani Kidaya, Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu , Mhandisi Innocent Luoga na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mhandisi Kapuulya Musomba.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani ( wa pili kushoto) akiangalia miundombinu ya usambazaji gesi majumbani katika eneo la Mlalakua jijini Dar es Salaam. Wa pili kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Mhandisi Kapuulya Musomba na wa Tatu kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya TPDC, Profesa Sufian Bukurura.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Mhandisi Kapuulya Musomba ( wa pili kutoka kulia) akimuonesha Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani ( wa kwanza kulia) miundombinu ya usambazaji gesi majumbani katika eneo la Mlalakua jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa tatu kutoka kushoto) akikagua miundombinu ya usambazaji gesi majumbani katika eneo la Mlalakua jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Waziri ni Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Profesa Sufian Bukurura na kushoto kwa Waziri ni Kaimu Kamishna wa Petroli na Gesi, Mwanamani Kidaya.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa pili kushoto) akizungumza jambo wakati alipofanya ziara ya kukagua miundombinu ya usambazaji gesi majumbani katika eneo la Mlalakua jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Waziri ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), Mhandisi Kapuulya Musomba na Mwenyekiti wa Bodi ya TPDC, Profesa Sufian Bukurura. Kushoto kwa Waziri ni Kaimu Kamishna wa Petroli na Gesi, Mwanamani Kidaya.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad