HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 26, 2019

WAZIRI MKUCHIKA ATOA SIKU 34 KWA AFISA UTUMISHI HALMASHAURI YA WILAYA YA KILWA KUWEKA TAARIFA SAHIHI ZA WATUMISHI KWENYE MFUMO WA HCMIS

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) ametoa siku 34 kwa Afisa Utumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Bi. Jovita Buyobe kuhakikisha anaweka taarifa sahihi za watumishi wa halmashauri yake katika Mfumo Shirikishi wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCMIS).
Agizo hilo amelitoa wakati wa mkutano kati yake na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa katika ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa.
Mkuchika amemtaka Afisa Utumishi huyo kuhitimisha zoezi la kuweka taarifa sahihi za watumishi wa halmashauri yake kwenye mfumo wa HCMIS ndani ya siku 34 kuanzia sasa mpaka mwishoni mwa mwezi wa tatu.
 Mkuchika amesema, ripoti zinaonyesha kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa inaongoza kwa kuwa na taarifa zisizo sahihi za watumishi kwenye mfumo wa HCMIS, hivyo amemtaka Afisa Utumishi huyo kutimiza wajibu wake.
Awali, akizungumzia taarifa za watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa zilizomo kwenye mfumo wa HCMIS, Afisa Utumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Bi. Jovita Buyobe amekiri kuwepo kwa taarifa zisizo sahihi za watumishi kwenye mfumo wa HCMIS na kutoa sababu ya uhaba wa watumishi.
Bi. Buyobe amefafanua kuwa, amekuwa akijitahidi kuweka taarifa sahihi za watumishi kwenye mfumo wa HCMIS bila mafanikio kwa kuwa anafanya kazi zote za kiutumishi na kiutawala peke yake, lakini amemhakikishia Waziri kumaliza suala hilo kwa kushirikiana na Afisa Utumishi mpya aliyeajiriwa hivi karibuni.
Mkuchika amehitimisha ziara ya kikazi mkoani Lindi yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma pamoja na kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF mkoani humo ambapo ametembelea Wilaya ya Liwale, Nachingwea, Ruangwa, Manispaa ya Lindi na Kilwa.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb), akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa mkoani Lindi (hawapo pichani) katika kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa. Kushoto ni Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Lindi, Dkt. Bora Haule na Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Christopher Ngubiagai (kulia kwake).
 Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Lindi, Dkt. Bora Haule akitoa utambulisho wa makundi ya watumishi waliohudhuria kikao kazi kati ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) na watumishi wa halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa.
Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Christopher Ngubiagai akimkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora,  Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) kuzungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Kilwa katika kikao kazi kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa.
 Baadhi ya Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) (hayupo pichani) wakati wa kikao kazi kilichofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa.
Afisa Utumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Bi. Jovita Buyobe akijibu hoja wakati wa kikao kazi cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Kilwa kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii, wilayani Kilwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad