HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, February 3, 2019

Wananchi wa Igando waanza kupata huduma ya umeme

Wananchi katika Kijiji cha Igando, wilayani Chato, mkoa wa Geita, wameanza kupata huduma ya umeme kupitia mradi wa Usambazaji Umeme Vijijini wa Awamu ya Tatu (REA III) unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani ndiye aliyewasha rasmi umeme jana katika Kijiji hicho, ambapo aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhandisi Mtemi Semeon na viongozi wengine kutoka Wilaya hiyo, Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Aidha, kabla ya kuwasha umeme katika Kijiji cha Igando, Dkt Kalemani alifika katika Kijiji cha Imwelu kilichopo Kata ya Buseresere wilayani humo ili kukagua kazi ya upelekaji wa miundombinu ya umeme katika Kijiji hicho.

Akiwa kijijini hapo, Dkt Kalemani aliwaagiza REA, TANESCO pamoja na mkandarasi aliyepewa kazi ya kusambaza umeme kijijini hapo, kuhakikisha kuwa, ifikapo tarehe 28 mwezi huu, kijiji hicho kiwe kimeshawashiwa umeme.

Kwa nyakati tofauti akizungumza na wananchi wa vijiji hivyo, alisisitiza kuwa, bei ya uunganishaji umeme katika vijiji vyote nchini ni shilingi 27,000, tu, hivyo wananchi wa vijijini wasitozwe zaidi ya kiasi hicho.

Aidha, amewataka wananchi hao kutumia umeme huo pia kwa shughuli za maendeleo ambazo zitawaongezea kipato na kukuza uchumi katika maeneo mbalimbali nchini.

Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa Tatu kulia) akikata utepe kuashiria kuanza kupatikana kwa huduma ya umeme katika Kijiji cha Igando, Kata ya Bwera wilayani Chato. Wa pili kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhandisi Mtemi Semeon.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akizungumza na wananchi katika Kijiji cha Imwelu, Kata ya Buseresere wilayani Chato ambapo alimwagiza mkandarasi kuwasha umeme katika Kijiji hicho ifikapo tarehe 28 mwezi huu.
Wananchi katika Kijiji cha Igando, Kata ya Bwera wilayani Chato wakimsikiliza Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani) wakati alipofika kijijini hapo kuzindua huduma ya umeme.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad