HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, February 14, 2019

SINGIDA YATINA HATUA YA 16 BORA BAADA YA KUIFUNGA JKT TANZANIA 1-0

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii
KIKOSI cha timu ya Singida Singida  United kimefanikiwa kuingia katika  hatua ya 16 Bora ya Kombe la Shirikisho Azam Sports Federation Cup (ASFC)  baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya JKT Tanzania kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.

Mchezo huo wa hatua ya 32 bora ulikuwa wa ushindani mkubwa sana kwa pande zote mbili kila timu ikitaka kuvuka hatua hiyo.

Kocha Mkuu wa Singida United Mserbia, Dragan Popadic amesema kuwa mchezo huo ulikuwa ni muhimu sana kwao na amefurahi kwa matokeo waliyoyapata wakiwa Uwanja wa nyumbani na kufanikiwa kusonga hatua inayofuata.

Popadic amesema, mechi hiyo ilikuwa ngumu sana kwao ila wachezaji walijituma katika dakika zote 90 na kufanikiwa kushinda, kikubwa timu ya JKT Tanzania ni nzuri na ina wachezaji wazuri na vijana wanaojituma muda wote.


Goli la Singida United lilifungwa na kiungo wake Kenny Ally Mwambungu kwa shuti la umbali wa mita 45, akiiwezesha SIngida United kuitoa JKT Tanzania kwa mara ya pili mfululizo kwenye michuano hiyo baada ya kukutana msimu uliopita kwenye hatua ya nusu fainali.

Baada ya  matokeo hayo, Singida United itakutana na Coastal Union ya Tanga katika hatua ya 16 Bora kati ya Februari 22 na 25, mwaka huu, kwa mara nyingine wakiwa nyumbani Uwanja wa Namfua.


Mechi nyingine za hatua ya 16 Bora ni Yanga SC na Namungo FC Uwanja Namungo Lindi, KMC na Mtibwa Sugar, African Lyon na Mbeya City FC Uwanja wa Uhuru, Azam FC na Rhino Rangers Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam, Alliance FC na Dar City Uwanja wa Nyamagana mjini Mwanza, Lipuli FC na Dodoma FC Uwanja wa Samora mjini Iringa na Boma FC na Kagera Sugar mjini Mbeya.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad