HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, January 8, 2019

Balozi Seif aweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la shule ya Sekondari ya Uweleni kisiwani Pemba

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo Jipya la Skuli ya Sekondari ya Uweleni Mkoa wa Kusini Pemba.
 Wananfunzi wa Skuli ya Sekondari ya Uweleni wakishangiria kumpokea mgeni rasmi wa Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Jengo lao la Skuli ya Sekondari.
 Haiba ya Jengo Jipya linalojengwa katika Skuli ya Sekondari ya Uweleni Wilaya ya Mkoani Mkoa wa Kusini Pemba.
 Baadhi ya Wanafunzi wa Skuli ya Sekondari ya Uweleni wakifuatilia hafla ya uwekaji wa Jiwe la Msingi la Skuli yao inayojengwa ya Ghorofa.
 Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mheshimiwa Mmanga Mjengo Mjawiri akitoa ufafanuzi wa takwimu za ongezeko la Skuli Nchini kabla na baada ya Mapinduzi.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akimpongeza Ustaadhi Khamis Ali wa Wilaya ya Mkoani baada ya kusoma Quran kwenye hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Skuli ya Sekondai ya Uweleni Kusini Pemba.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akizungumza na Wananchi wa Pemba  baada ya kuweka Jiwe la Msingi la Jengo Jipya la Skuli ya Sekondari ya Uweleni Pemba. Picha na – OMPR – ZNZ.

Wazanzibari wana kila sababu ya kujivunia Maendeleo makubwa yaliyopatikana katika Sekta ya Elimu yaliyosimamiwa na Chama cha Afro Shirazy Party  na Baadae CCM katika kipindi chote cha  Miaka 55 tokea kufanyika kwa Mapinduzi ya Zanzibar ya Mwaka 1964 yaliyoondoa Utawala wa Kibaguzi katika Elimu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati wa hafla ya kuweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Skuli ya Sekondari ya Uweleni iliyopo Mkoani Kisiwani Pemba katika Smra shamra za kusherehekea Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar  ya Mwaka 1964 kutimia Miaka 55.

Balozi Seif Ali Iddi alisema hatua iliyofikia Taifa hivi sasa katika Sekta ya Kielimu ni kubwa kiasi kwamba wale wanaokebehi wanashindwa kujifahamu kwamba wanajidharau wao wenyewe  na dawa yao ni kupuuzwa kwa sababu hawajui thamani ya kuwa na chao na wala sio watu wanaothamini cha wenzao. Alisema tokea Wananchi wa Zanzibar walipojitawala  kutoka katika makucha ya kibeberu, Vijana wa Visiwa hivi wanaendelea kupata Elimu bila ya malipo, kuanzia maandalizi hadi Sekondari ya Juu ambapo pia wakifikia Vyuo Vikuu kuna utaratibu wa kuwapatia udhamini kwa wale wanaofanya vizuri.

Balozi Seif  alieleza kwamba miongoni mwa mambo yaliyoahidiwa na Chama cha Afro Shirazy Party wakati wa kupigania Uhuru kwamba iwapo Chama hicho kitashika hatamu Elimu kwa Watoto wa Wakulima na Wafanyakazi itatolewa bure bila ya malipo.

Alifahamisha kwamba Historia inaonyesha wazi kuwa kabla ya ukombozi Skuli za Sekondari zilikuwa kidogo akatolea mfano kisiwani Pemba ilikuwepo Skuli Moja tu ya Fidel Castro, hii ikimaanisha kwamba Wilaya nzima ya Mkoani wakati huo haikuwa na Skuli ya Sekondari. “ Tulipofikia kielimu ni hatua kubwa ni lazima tujivunie sana. Wale wanaokebehi hatua hii wanajidharau wao wenyewe na dawa yao kubwa ni kuwapuuza”. Alisema Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  alisema uwepo wa Jengo hilo utarahisisha upatikanaji wa Taaluma ambayo itawaandaa Vijana mbali ya kuwa Wataalamu wa Taasisi za Umma hapo baadae lakini pia watajiepusha na mambo yanayoweza kuwaletea madhara. Balozi Seif alipongeza Umoja ulitumika katika Ujenzi wa Jengo hilo la Skuli ikiwa ni ushahidi tosha utakaowafanya walengwa wake kushiriki kikamilifu kuhimiza malengo ya Kitaaluma na kimaadili yaliyokusudiwa.

Akitoa Taarifa ya Kitaalamu ya Ujenzi wa Jengo hilo la Ghorofa la Skuli ya Sekondari ya Uweleni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Nd. Abdullah Mzee Abdullah alisema ujenzi huo umekuja kutokana uhaba ya Madarsa sambamba na kuzingatia Sera ya Elimu ya Ujenzi wa Skuli za ghorofa kwa lengo la uhifadhi ya Ardhi ndogo iliyopo.

Nd. Abdulah alisema inapendeza kuona Wananchi mbali mbali hasa wale wenye Asili ya Skuli hiyo wamejitolea nguvu zao zilizowezesha maendeleo ya Ujenzi wa Jengo hilo kwenda kwa kasi kubwa. 
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  imeamua kujenga majengo makubwa ya Ghorofa ili kila Mtoto wa Visiwa Vya Unguja na Pemba waliotokana na Mifupa ya Wakwezi na Wakulima wanapata haki yao ya  Elimu.

Naibu katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya  Amali Zanzibar alisisitiza kwamba ongezeko la Skuli za Sekondari Nchini hivi sasa linatia moyo na kuleta faraja kwa Jamii kutoka Skuli 4 za Sekondari Kabla ya Mapinduzi na kufikia Skuli 204 za Sekondari Unguja na Pemba. Takwimu hiyo inaonyesha wazi kwamba Kisiwa cha Unguja hivi sasa kimezunguukwa na Skuli za Sekondari zipatazo124 wakati Kisiwani cha Pemba kimefanikiwa kuwa na Skuli 80 kiwango kinachoonyesha wastani wa Skuli 10 za Sekondari kwa kila Wilaya ya Zanzibar.

Akimkaribisha mgeni rasmi katika hafla hiyo ya uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo jipya la Skuli ya Sekondari ya Uweleni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh.Mmanga Mjengo Mjawiri alisema Zanzibar hivi sasa ina skuli 202 za Msingi kutoka Skuli Moja kabla ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Mwaka 1964.

“ Kwa sasa Zanzibar tumefanikiwa kuwa na Skuli zipatazo Mia Tisa Msingi na Sekondari kwa zile za Serikali pamoja na Binafsi”. Alisema Naibu Waziri huyo wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar. Mh. Mmanga alisema mfumo wa Elimu Zanzibar hivi sasa umeimarika vyema kutokana na ongezeko kubwa la Wanafunzi  zaidi ya Elfu 9,000 kwenye vyuo vikuu vya Zanzibar  pekee.

Alisema ufaulu wa Wanafunzi hivi sasa umefikia asilimia 98% katika kiwango sha Sekondari kinachowawezesha kuwa na sifa za kujiunga na vyuo Vikuu mbali mbali. Akigusia suala la Madaftari Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya  Amali Zanzibar Mh. Mmanga Mjengo Mjawiri alisema Madaftari ya matumizi kwa Wanafunzi wa Zanzibar yapo na kuwatoa wasi wasi Wazazi kwa vile yaliyopo yana uwezo wa matumizi ya Miezi Sita.

Mh. Mmanga alisema Madaftari hayo kwa upande wa Kisiwa cha Pemba yameshafikishwa na kinachosubiriwa kwa sasa ni kumalizika kwa Sherehe za Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Mwaka 1964 zinazofikia Kilele chake Mnamo Tarehe 12 Januari 2019 katika Uwanja wa Gombani Chajke Chake Pemba ili yagaiwe katika Skuli mbali mbali Kisiwani humo.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshatenga Shilingi za Kitanzania Bilioni Mbili {2,000,000,000/-} kwa ajili ya ununuzi wa Madaftari mengine ya vipindi vijavyo na mchakato wa ununuzi huo unaendelea.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad