HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, December 20, 2018

Watumishi OSHA Waaswa Kufanya Kazi Kwa Kuzingatia Maadili

Watumishi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA ) wametakiwa kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, weledi, sheria na kanuni zinazosimamia utumishi wa umma ili kufikia malengo yakutoa huduma bora kwa wananchi hasa wanyonge kama dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano inavyoelekeza.

Akizungumza  kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi Vijana Ajira na Wenye Ulemavu, wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa OSHA, Mkurugenzi wa Idara ya Vijana Bw. James Kajugusi amesema kuwa kikao hicho ni fursa pekee ya kutathmini utendaji wa wafanyakazi na kuangalia namna ya kuboresha ili kufikia malengo yaliyowekwa. “Baraza hili la Wafanyakazi linasisitiza umuhimu wa watumishi kufanya kazi kwa maadili na nidhamu ya hali ya juu kama wakaguzi wa masuala ya Afya na Usalama  katika maeneo ya kazi ili muweze kuwa mfano wa kuigwa na Taasisi nyingine za Umma zinazofanya kazi zinazoshabihiana na za kwenu.”

Akifafanua Bw. Kajugusi  amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati, kuondoa uzembe, ubadhirifu pamoja na vitendo vyovyote vya rushwa mahala pa kazi, ikiwa ni pamoja na kubana matumizi yasiyo ya lazima ili kuongeza tija. Aliwaasa watumishi hao kuhakikisha kuwa wanatekeleza wajibu wao kwa kuzingatia malengo yaliyopangwa kwa wakati husika ili kuchochea maendeleo.

Pia aliwahakikishia kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu iko tayari na itaendelea kushirikiana na OSHA kutatua changamoto zitakazoibuliwa ili kusaidia katika kutekeleza dhana ya ujenzi wa uchumi wa viwanda kwa wakati. Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija  Mwenda, amesema kuwa wameshiriki kikamilifu katika kuchochea uchumi wa viwanda kwa kupunguza gharama za ufanyaji biashara kupitia tozo na ada mbalimbali zilizoondolewa pamoja na kuondoa urasimu katika kutoa huduma.

Tozo hizo zimeondolewa baada ya Serikali ya Awamu ya Tano kujikita katika kujenga uchumi wa Viwanda na kuboresha mazingira ya Biashara na uwekezaji nchini. Alibainisha kuwa baadhi ya Ada na tozo zilizoondolewa ni pamoja na; Ada ya Usajili wa eneo la kazi iliyokuwa ikitozwa kati ya shilingi elfu 50,000/ hadi 1,800,000/, Ada ya fomu ya Usajili sehemu ya kazi (2000/-), kufuta faini zinazohusiana na vifaa vya kuzima moto ya shilingi laki 5,000,000/-.

Ada nyingine zilizoondolewa ni pamoja na Ada ya Leseni ya kukidhi matakwaa ya sheria ya Afya na Usalama iliyokuwa inatozwa shilingi 200,000/ kwa mwaka na kuondoa tozo ya ushauri wa kiutaalamu wa Usalama  na Afya ya shilingi laki 450,000/kwa sasa. Hatua nyingine zilizochukuliwa ni pamoja na kupunguza urasimu katika muda wa kupata cheti cha usajili wa sehemu ya kazi kutoka siku 14 hadi siku 1 kwa sasa.Pia upatikanaji wa leseni ya kukidhi matakwa ya sheria ya Usalama na Afya mahali pa kazi imepungua kutoka siku 28 hadi siku 3.

Baraza la Wafanyakazi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA) limefanyika Jijini Dodoma kwa siku mbili likilenga kutathmini utendaji kwa kipindi cha miezi sita iliyopita na kuweka mikakati ya pamoja ya kuongeza tija katika huduma za Wakala huo ili kufikia malengo ya kuanzishwa kwake.
  Mkurugenzi wa Idara ya Vijana Kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi,Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Bw. James Kajugusi, akizungumza  kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Jijini Dodoma wakati wa kikao cha Baraza la wafanyakazi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA) kuhusu umuhimu wa kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.
 Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda, akimkaribisha  Mkurugenzi wa Idara ya Vijana Kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi Vijana Ajira na Wenye Ulemavu, Bw. James Kajugusi, kufungua kikao cha baraza la wafanyakazi wa Wakala huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi Vijana Ajira na Wenye Ulemavu, Bw. Andrew Massawe, Jijini Dodoma.
 Sehemu ya washiriki wa Kikao cha Baraza la wafanyakazi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA) kinachofanyika  Jijini  Dodoma.

 Mkurugenzi wa Idara ya Vijana Kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Bw. James Kajugusi, akishiriki kuimba wimbo wa mshikamano na  washiriki wa Kikao cha Baraza la wafanyakazi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA) kilichofanyika  Jijini  Dodoma.
Mkurugenzi wa Idara ya Vijana Kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Bw. James Kajugusi, (wa nne kutoka kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Wakala wa Usalama na Afya Mahala Pa Kazi (OSHA).
                                                          

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad