HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, December 11, 2018

TGNP YAZIDI KUENDELEZA MIKAKATI KUPUNGUZA UKATILI YA KIJINSIA KWA ASILIMIA 50 IFIKAPO 2030

Na Leandra Gabriel, Blogu ya jamii
MTANDAO wa ujinsia nchini (TGNP) umefanya mkutano na mjadala kuhusiana na haki ya afya ya uzazi uliowakutanisha wadau mbalimbali wanaofanya kazi katika sekta ya afya ikiwa ni katika kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia. Akizungumza katika mkutano huo Afisa programu wa wanaharakati na ujenzi wa pamoja (TGNP) Anna Sangai amesema kuwa lengo la kufanya mkutano huo ni kufanya tathimini ya wapi walipo na wanapoenda kuhusiana na hali ya jinsia nchini.

Akieleza tathimini ya nchi Sangai amesema kuwa Tanzania inafanya vizuri kiutekelezaji katika kupinga ukatili wa kijinsia hasa kwa wanawake na watoto. Pia ameeleza kuwa changamoto zinazozikabili mapambano hayo ni pamoja na kutofika kwa  elimu ya afya ya uzazi katika maeneo mbalimbali, utekelezaji wa sheria na mipango dhidi wanaovunja sheria na kufanya vitendo vya ukatili pamoja na mazingira magumu ya upatikanaji wa haki kwa kuwa kesi huchukua muda mrefu huku waathirika wakisumbuka kutafuta haki zao.

Sangai amesema kuwa mjadala huo utaweka mazingira wezeshi na kutoka na kampeni mbalimbali zitakazohusisha wadau  kutoka sekta ya afya nchini kote na hiyo itasaidia kufikia malengo  ya kupunguza asilimia 50 ya vitendo vya ukatili wa kijinsia ifikapo 2030. Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa kituo cha kuzuia unyanyasaji wa kijinsia, Sophia Komba amesema kuwa katika mkutano huo watazungumzia haki ya afya ya uzazi ambayo imekumbwa na na matukio ya unyanyasaji hasa kwa vijana na wanawake.

Amesema kuwa matukio ya ubakaji na kulawitiwa kwa watoto wakiume ni lazima yazungumziwe ili yakome. Vilevile amesema kuwa matukio ya ukatili wa kijinsia yana uhusiano na afya  hasa yale ya kuumizwa kimwili ambayo huweza kupelekea kudhoofu kwa afya na ametoa wito kwa Serikali kutambua tatizo hilo na kuweka sera na mipango ili kuweza kuondoa ukandamizi na kujenga jamii ambayo ina ulinzi hasa kwa wanawake na watoto.
Afisa programu wa wanaharakati na ujenzi wa pamoja kutoka mtandao wa ujinsia nchini (TGNP) Anna Sangai akizungumza wakati wa mkutano huo uliolenga kujadili haki ya afya ya uzazi uliofanyika leo jijini Dar es salaam, ambapo ameeleza kuwa wanaendelea na mikakati ya kufikia malengo ya kupunguza matukio ya ukatili wa kijinsia ifikapo 2030.
Mshauri wa masuala ya kijinsia kutoka Afrika kusini Kubi Rama akifafanua jambo katika mkutano uliolenga hasa kujadili haki ya afya ya uzazi  ulioandaliwa na mtandao wa ujinsia nchini (TGNP) na kueleza kuwa usawa lazima uwepo na kuzingatia kwa kuwa matukio mengi ya unyanyasaji hutokea pale ambapo mtu hukosa chanzo chochote cha kupata kipato hasa kwa wanawake.
Mkurugenzi mtendaji wa kituo cha kuzuia unyanyasaji wa kijinsia Sophia Komba akizungumza wakati wa mkutano huo uliofanyika leo jijini Dar es salaam na kueleza matatizo ya ubakaji na kulawitiwa lazima yazungumzwe ili yaweze kukoma.
Mkutano ukiendelea

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad