HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 19, 2018

TANZANIA KINARA UTEKELEZAJI WA MASUALA YA VIJANA NCHI ZA SADC

Na Leandra Gabriel, Blogu ya Jamii
TANZANIA imetajwa kuwa kati ya nchi tano ndani ya jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini mwa Afrika SADC ambazo zinatoa kipaumbele kwa masuala yanayohusu vijana.

Hayo yameelezwa katika mkutano wa vijana toka nchi za SADC uliofanyika mjini Windhoek, Namibia kati ya tarehe 13 na 15 Disemba 2018 ambapo mkutano huo ulifunguliwa na Waziri wa Michezo, Vijana na Huduma za Umma wa Namibia, Mheshimiwa Erustus Uutoni ambaye alieleza nafasi zilizopo kwa  vijana katika ukanda huo.

Sambamba na hilo Uutoni alieleza namna viongozi akiwemo Mwalimu Julius Nyerere walivyotumia vizuri ujana wao kuleta uhuru kwenye nchi za kusini mwa Afrika, na kutoa Wito kwa Vijana wa nchi 16 za SADC kutumia vema ujana kwa maendeleo ya uchumi, siasa na jamii zao.

 Uutoni alieleza kuwa wakuu wote wa chi za SADC wapo tayari kusaidia vijana kufikia ndoto zao wakiwa katika nafasi nzuri kuliko wageni wanaoingia na kupora fursa za vijana na
Aliitaja Tanzania kama msambazaji mkuu wa madawa, vifaa tiba na vitendanishi kwa nchi zote za SADC na kueleza kuwa Vijana wana nafasi kubwa sana katika maendeleo ya viwanda hasa vya vifaa tiba.

Kwa upande wake Mratibu wa masuala ya jamii na maendeleo ya watu SADC Bi. Duduzile Simelane alieleza kuwa Tanzania imekuwa na utaratibu mzuri wa kufungua fursa za kiuongozi kwa vijana, Lakini pia wizara inayohusiana na masuala ya vijana imewekwa chini ya ofisi ya waziri mkuu na ikiwa na naibu waziri ambaye ni kijana( Hapa akimaanisha Naibu Waziri Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Mheshimiwa Anthony Mavunde).

Siku ya Pili ya Mkutano huo, Sekretariati ya SADC chini ya Willys Simfukwe ambaye ni Mshauri Ufundi wa SADC masuala ya maendeleo ya SADC aliitaja Tanzania, Botswana, Afrika ya Kusini, Zambia na Mauritius kama nchi zitakazotoa uzoefu kwa nchi nyingine 11 za SADC na hiyo ni kutokana na namna zinavyotekeleza masuala ya vijana.

Akifafanua jinsi masuala ya vijana yanavyotekelezwa na serikali ya awamu ya tano chini ya Mheshimiwa Rais John Joseph Magufuli, Mwakilishi wa Tanzania katika Mkutano wa vijana, Bi Charangwa Sulemain Makwiro aligusia  jinsi halmashauri zinavyotenga asilimia nne ya mapato kwa ajili ya Vijana. Pia alieleza uwakilishi wa vijana ndani ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi(UVCCM), Utengaji wa maeneo kwa ajili ya vijana wafanyabiashara na jinsi asasi za kiraia zinazoshughulikia masuala ya vijana zinavyoshirikiana na serikali katika kuelemisha juu ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI pamoja na ushiriki wao katika siasa, uchumi na utamaduni.

Aidha kwa upande wake Francis Daudi aliyeiwakilisha Tanzania alieleza jinsi vyuo 55 vya maendeleo ya Wananchi(Folks Development Colleges) vilivyo chini ya Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia vinavyofanya kazi katika kuwawezesha vijana kupata ujuzi wa kuweza kuajiriwa na kujiajiri. Lakini pia kuna mfuko maalumu chini ya Ofisi ya Waziri mkuu unaowawezesha vijana kujikwamua kiuchumi.

Pia Daudi alitoa wito kwa mataifa ya SADC kuendelea kuboresha mfumo wa elimu ya Ufundi kwani unawapa vijana wengi Ujuzi ambao hasa unahitajika kwenye uchumi wa viwanda na kuongeza kuwa Wakuu wa SADC waangalie jinsi watakavyoweza kupunguza ada ili Vijana toka familia za kawaida waweze kupata fursa hiyo adhimu kabisa.

Mkutano huo  ulikuwa maalumu kwa ajili ya kuandaa mapendekezo muhimu kwa ajili ya ajenda za kikao cha Mawaziri wanaosimamia masuala ya Vijana ndani ya SADC utakaofanyika mwezi Mei, 2019 huko Windhoek, Namibia na ikumbukwe kuws mwaka 2019, Rais wa Tanzania, Mheshimiwa Rais John Joseph Magufuli atakuwa Mwenyekiti wa  jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini mwa Afrika SADC.

Katika mkutano huo Tanzania iliwakilishwa na Charangwa Selemani Makwiro na Francis Daudi, pia kulikuwa na wawakilishi toka Asasi ya kiraia ya Tanzania Youth Coalition(TYC) iliyowahusisha Aziza Ngalupia na Ernest Seko.
Wawakilishi kutoka Tanzania, wakiwa kwenye mkutano wa SADC 2018 uliofanyika Windhoek Namibia, kutoka kushoto ni Charangwa Makwira akifuatiwa na Francis Daudi, Aziza Ngalupia na wa mwisho kulia ni Ernest Seko.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad