HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 16, 2018

MHANDISI LUHEMEJA AZUNGUMZIA MAFANIKIO YA DAWASA KATIKA MIAKA MITATU YA DKT JOHN POMBE MAGUFULI


Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya MajiSafi na MajiTaka Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Cyprian Luhemeja akizungumzia mafanikio ya miaka mitatu ya Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli ikiwemo makusanyo ya maduhuli kwa mwaka 2014/15 yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 2.9 na kufikia bilion 10.5 kwa mwezi kwa mwaka 2018 leo Jijini Dar es Salaam.



Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii

Katika mafanikio ya miaka mitatu ya Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli makusanyo ya maduhuli ya Mamlaka ya MajiSafi na MajiTaka Dar es Salaam (DAWASA) kwa mwaka 2014/15 yameongezeka kutoka wastani wa shilingi bilioni 2.9 na kufikia 10.5 kwa mwezi kwa mwaka 2018.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa Habari maelezo leo Jijini Dar es Salaam, Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kuwa Kwa hivi sasa makusanyo yameongezeka hadi kufikia Shilingi bilioni 10.5 kwa mwezi kwa mwaka huu 2018 huku lengo letu na mikakati ni kufikia makusanyo ya Shilingi bilioni 12 kwa mwezi.

Mhandisi Luhemeja amesema, kwa upande wa ukusanyaji wa mapato haya yanatokana na mauzo ya huduma za maji na majitaka katika eneo la DAWASA, ambalo ni jiji la Dar es salaam na miji ya Kibaha na Bagamoyo

Ameeleza kuwa, mpaka sasa katika kipindi cha miaka mitatu ya Serikali ya awamu ya tano, miradi mikubwa iliyokamilika ni pamoja na upanuzi wa mtambo wa Ruvu juu, ujenzi wa tenki la Kibamba na ulazaji wa mabomba makuu ya kusafirisha maji.

Mhandisi Luhemeja amesema, kufuatia kukamilika kwa miradi mbalimbali , maji yanayozalishwa yameongezeka na kufikia lita milioni 502 kwa siku wakati mahitaji ya maji kwa siku ni lita milioni 554, na Serikali imejipanga kumaliza tatizo la Maji Dar es Salaam ifikapo mwaka 2020 kwa upatikanaji wa huduma za maji katika jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani kufikia asilimia 95 kwa maji safi na asilimia 30 kwa maji taka.

Amesema, Katika miaka hii mitatu ya Serikali ya awamu ya tano miradi mingine inayotekelezwa ni pamoja na ile ya kufikisha huduma katika maeneo ambayo hapo awali yalikuwa na changamoto ya upatikanaji wa maji kwa kutumia fedha za ndani.

Sehemu kubwa ya jiji inapata maji, ambayo hayakuwa na huduma sasa yamefikiwa kwa mfano maeneo ya Segerea, Kinyerezi, Kipawa, Ukonga, Changanyikeni, Goba, Mivumoni, Salasala, Madale kwa Msuguri, kwa Mbonde, Misugusugu, Kiwalani, Miti Mirefu na baadhi ya maeneo ya Kigamboni", amesema Mhandisi Luhemeja. 

Mhandisi Luhemeja amesema kuwa, mafanikio haya yanakuja baada ya ufanisi katika utekelezaji wa miradi mbalimbali iliyopelekea kuongezeka kwa maji yanayozalishwa pamoja na kuimarika kwa utendaji kazi kunakozingatia usimamizi mahiri wa utoaji huduma bora.

“Katika kuhakikisha kuwa maji yalioongezeka yanawafikia wananchi wengi zaidi hasa katika maeneo ambayo zamani hayakuwa na mtandao wa mabomba, miradi mbalimbali mikubwa na midogo imetekelezwa, miradi hiyo inahusisha ujenzi wa matenki ya maji matano yenye ujazo wa kati ya lita milioni 5.0 na 6.0 pamoja na ulazaji wa mtandao wa mabomba”, amesema.

Matenki hayo yamejengwa katika maeneo ya Changanyikeni, Salasala,Wazo, Mabwepande na Bagamoyo na katika maeneo yote ya miinuko ili kuwezesha maji kufika katika maeneo mengi Zaidi kwa msukumo mzuri na mradi huo umetekelezwa na serikali kupitia mkopo wa masharti nafuu kutoka benki ya Exim ya India na upo katika hatua za ukamilishwaji.


Mhandisi Luhemeja amesema kilometa 176 za mtandao chakavu wa maji zimebadilishwa na hivyo kuchangia kupungzua kiwango cha maji yanayopotea, kwa ujumla kiasi cha kilomita 500 za mabomba mapya zzimelazwa mitaani ili kuweza kugawa maji kwa uwiano mzuri zaidi na kufanya mamlaka kuwa na mtandao wa Kilomita 3,000 kutoka 2,500 zilozokuwepo 2015. 

Ili kuboresha huduma na kufikia lengo la kufikishia asilimiaa 95 ya wananchi ndani ya eneo la huduma ya DAWASA maji safi, bora na ya gharama nafuu kuna miradi imendelea kutekelezwa ambapo kuna mradi wa Chalinze III, Kibamba-Kisarawe , Chalinze Mboga, Mlandizi - Manelomango, Kilindoni- Mafia, Mkuranga na miradi mipya inayolenga kufikia watu wenye kipato waishio katika maeneo yasiyo na huduma ya maji.

Miradi mitatu mikubwa ya kisasa ya uchakataji majitaka inatarajiwa kujengwa hivi karibuni ikiwa ni sehemu ya kufikishwa asilimia 30 ya huduma ya majitaka. Pia miradi midogo ya uchakataji majitaka ipatao 50 itejengwa kuhakikisha kuwa wananchi wa ngazi zote wanafikiwa na huduma bora ya majitaka.
Mkurugenzi wa idara ya habari maelezo Tanzania Dr. Hassan Abbas akimkabidhi kitabu cha nchi yetu kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya MajiSafi na MajiTaka Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Cyprian Luhemeja leo Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad