HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, October 17, 2018

MAHAKAMA KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUTOA HAKI


Na Lydia Churi-Mahakama Sengerema
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema Mahakama itaendeleza ushirikiano uliopo kati yake na mihimili mingine ili kurahisisha suala la utoaji na upatikanaji wa haki nchini.
Akizungumza na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Sengerema ikiongozwa na mwenyekiti wake ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Jaji Mkuu alisema Mahakama inapata nguvu zaidi ya kutekeleza majukumu yake ya msingi pale inapopata ushirikiano kutoka mihimili mingine yaani Bunge na Serikali.
Alisema endapo Mihimili yote mitatu ya dola haitashirikiana ni wazi kuwa kazi ya utoaji na upatikanaji wa haki itakuwa ni ngumu. Aliongeza kuwa mihimili hii imewekewa utaratibu wa kutekeleza majukumu yake pasipo kuingiliana.
Aidha, Prof. Juma aliipongeza Mahakama ya wilaya ya Sengerema pamoja na Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Sengerema kwa kuwa na uhusiano wa karibu na ushirikiano kwenye utekelezaji wa majukumu yao.
Akizungumzia kuhusu rushwa na uvunjifu wa maadili, Jaji Mkuu alisema Mahakama ya Tanzania imeamua kupiga vita rushwa na ukosefu wa maadili kwa watumishi wake ambapo pia alimtaka Mkuu wa wilaya ya Sengerema kutosita kuwaita na watumishi wa Mahakama watakaopotoka kwenye suala la rushwa na maadili.
Alisema Mahakama imeamua kutoa nakala za hukumu bure pamoja na kuingia mkataba na shirika la Posta ili kusambaza nakala hizo pamoja na nyaraka nyingine, kama hatua ya kupambana na vitendo vya rushwa.
Naye Mkuu wa wilaya ya Sengerema Bwana Emmanuel Kipole alisema mahusiano kati ya Serikali na Mahakama kwenye wilaya yake ni mazuri kwani wamekuwa wakifanya kazi kwa kushirikiana na kuheshimiana bila kuingiliana majukumu.
Mkuu huyo wa wilaya pia amemwomba Jaji Mkuu kuongeza idadi ya Mahakimu kwenye Mahakama ya wilaya kwa kuwa hivi sasa Mahakama hiyo ina hakimu  moja ambaye haendani na idadi ya mashauri yaliyopo kwenye Mahakama ya wilaya.
Aidha Mkuu huyo wa wilaya pia alisema kwa kurahisisha hudumu kwa wananchi, wilaya yake imetenga eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 24,282 kwa ajili ya kujenga Mahakama, kituo cha Polisi na Magereza.
Wakati huo huo, Ofisi ya Takukuru wilaya ya Sengerema imetoa pongezi kwa Mahakama kwa kuanzisha program maalum ya kuelimisha Umma kila siku ya Alhamis kuhusu taratibu za Mahakama kwani program hiyo imesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza malalamiko ya rushwa wilayani humo. 
Jaji Mkuu anaendelea na ziara ya kikazi mkoani Mwanza ambapo leo alitembelea Mahakama ya wilaya ya Sengerema pamoja na Mahakama za Mwanzo za Sima, Busisi, Buyagi na Mahakama ya Mwanzo Sengerema mjini. Jaji Mkuu pia alimtembelea Mkuu wa wilaya ya Sengerema. 
  Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwasili katika wilaya ya Sengerema kuendelea na ziara ya kukagua kazi za Mahakama aliyoianza jana katika Mkoa wa Mwanza. 
  Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisalimiana na watumishi wa Mahakama ya wilaya ya Sengerema alipowasili katika wilaya hiyo leo kuendelea na ziara ya kukagua kazi za Mahakama aliyoianza jana katika Mkoa wa Mwanza. 
 Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akisaini kitabu cha wageni alipowasili katika wilaya ya Sengerema kuendelea na ziara ya kukagua kazi za Mahakama aliyoianza jana katika Mkoa wa Mwanza. 
 Mkuu wa wilaya ya Sengerema, Emmanuel Kipole akizungumza wakati alipotembelewa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ofisini kwake leo.Wa kwanza kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Mwanza Mhe. Sam Rumanyika na wa kwanza kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Sengerema Mhe. Monica Ndyekobora.
 Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akimuelezea Mkuu wa wilaya ya Sengerema, Mhe. Emmanuel Kipole kuhusu kitabu cha Mpango Mkakati wa Mahakama kabla ya kumkabidhi. 
  Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Bwn. Samson  Mashalla (wa pili kushoto) akifuatilia jambo wakati wa ziara ya Jaji Mkuu wilayani Sengerema. 
  Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania Bwn. Anatory Kagaruki akielezea jambo kuhusu masuala ya Utumishi wakati Jaji Mkuu alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Mahakama ya wilaya ya Sengerema.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad