HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, October 29, 2018

Airtel Tanzania yatoa msaada kwa kituo cha yatima Morogoro

Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania kupitia kitengo chake cha huduma kwa wateja imetoa msaada wa vitu mbali mbali kwa kituo cha yatima cha Mgolole Orphanage Center, Morogoro.

Msaada huo ni pamoja na vitanda, neti, magodoro, deep freezer, chupa za chai, hot pot, sukari, sahani, sabuni, nepi, pampers na toy za watoto vyote vikiwa na thamani ya TZS 18 milioni.

Kutoa kwa msaada huo ni muendeleo wa kampuni ya Airtel Tanzania kupitia programu ya Airtel Tunakujali ambapo wafanyakazi wa kampuni hiyo kukubali kutoa sehemu ya mshahara wao ili kusaidi huduma za kijamii na hasa kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Akiongea mara baada ya kutoa msaada huo kwa kituo hicho cha Mgolole cha Morogoro, Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja Airtel Tanzania Adriana Lyamba alisema muda mrefu wafanya kazi wa Airtel kupitia Airtel tunakujali imekuwa ikitembelea na kusaidia vituo mbali mbali vya yatima ikiwa ni pamoja na kuwapa misaada mbali mbali.

Leo ni siku yenye furaha sana kwetu zote kwani mayatima ni sehemu ya Jamii yetu na ni muhimu kuwapa upendo pamoja na kuwafariji. Hiki ambacho tumekuja kutoa leo hapa  ni kidogo lakini nina uhakika kitagusa mioyo yenu lakini zaidi ni kujua tuko pamoja nanyi na tunawajali sana, alisema Lyamba.

Naomba kutoa pongezi za dhati kwa wafanyakazi wenzangu wa Airtel kwa kukubali kutoa sehemu ya kipato chao na leo tumeweza kufika hapa. Lakini zaidi napongeza uongozi wa kampuni yetu kwa kukubali na kuridhia programu yetu hii hapa ya Airtel Tunakujali ambayo imekuwa ikituleta karibu na Jamii inayotuzunguka, alisema Lyamba.

Tunayo furaha kuweza kuwafikia watoto hawa ambao wako kwenye kituo hiki na dhamira yetu ni kuendelea kugusa maisha ya watoto wanaoishi kwenye mazingira mangumu na kuwafanya wajisikia kuwa sehemu ya familia ya Airtel, aliongeza Lyamba.

Kwa upande wake, Makamu Mama Mkuu wa kituo cha Mgolole Sista Valeria Mnyanzaga alisema ni furaha kwa kampuni kubwa ya Airtel kuguzwa na maisha ya watoto wanaoishi kwenye kituo hiki na hatimaye kuja kutoa msaada na kutuunga mkono.

Najua kuna vituo vingi vya mayatima hapa nchini kama sisi hapa. Kuamua kuja kuwa na sisi ni Baraka kubwa kwetu. Nachukua fursa hii kuwapongeza wote kwa kile mlichotoa ambacho mnaweza kudhani ni kidogo lakini kinaleta matumaini makubwa kwetu na hasa kwa hawa watoto. Naomba kuwakaribisha tena hapa na sio lazima kuja kutoa msaada, lakini mnapokuja kujumuika na hawa watoto wanapata faraja kubwa na kujisikia kama sehemu ya Jamii kwani wengi wao hapa hawajawahi kuona Wazazi wao, alisema Mnyanzaga.

Kituo cha Mgolole ambacho kiliazishisha mwaka 1937 kimekuwa kikilea na kusomesha watoto yatima kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania. Mmoja wa wanufaika wa kituo hicho ni Sebastian Alphonce ambaye amekulia na kusomea kwenye kituo hicho. Kama mnavyoniona mimi nimekuwa mzee kwa sasa. Lakini nimekulia na kusomesha na kituo hiki. Hatimaye nikawa Afisa polisi na kustaafu mwaka 2016 kwa mujibu wa sharia zetu. Hata hivyo, baada ya kustaafu nikaona ni busara kuja kuendelea kukaa na hawa wototo ili kutambua na kuelewa kuwa yatima sio mwisho wa maisha, alisema Aphonce.

Natoa shukrani za dhati kwa kituo cha Mgolole kwani bila kituo hiki sijui leo ningekuwa wapi. Lakini zaidi ni kwa kampuni ya Airtel ya kwa msaada huu. Kutoa msaada huu ndio kunawafanya hawa watoto wajione ni sehemu ya Jamii kwani wengi hawajawahi kuwaona Wazazi wao kabisa, alisema Alphonce.
 Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja Airtel Tanzania Adriana Lyamba (kulia) akikabidhi msaada kwa Makamu Mama Mkuu wa kituo cha yatima cha Mgolole, Morogoro. Airtel Tanzania kupitia mradi wake wa Airtel Tunakujali walitembelea kituo hicho pamoja na kutoa msaada wa vitu mbalimbali vyenye dhamani ya TZS 18 milioni mwishoni mwa wiki.
 Mkurugenzi wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja Airtel Tanzania Adriana Lyamba (kulia) akikabidhi msaada wa dogoro kwa Makamu Mama Mkuu wa kituo cha yatima cha Mgolole, Morogoro. Airtel Tanzania kupitia mradi wake wa Airtel Tunakujali walitembelea kituo hicho pamoja na kutoa msaada wa vitu mbali mbali vyenye dhamani ya TZS 18 milioni mwishoni mwa wiki. Kati kati ni Meneja wa Kitengo cha huduma kwa wateja Airtel Tanzania Deogratius Hugo. 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad