HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, September 25, 2018

SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR YAAHIDI KUENDELEZA USHIRIKIANO NA OFISI YA MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA NCHINI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa ushirikiano kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini ili Ofisi hiyo iweze kutekeleza vyema majukumu yake katika kuimarisha demokrasia nchini.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Septemba 25, 2015 alipokuwa na mazungumzo na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania Mhe. Mohammed Ali Ahmed aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais akiwa amefuatana na Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania Mhe.Jaji Francis Mutungi.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatambua umuhimu wa Ofisi hiyo pamoja na uongozi wake kwa Taifa, hivyo kuna kila sababu ya kutoa ushirikiano wake kwa lengo la kuimarisha demokrasia.

Dk. Shein alimpongeza Naibu Msajili huyo wa Vyama vya siasa kwa kuteuliwa nafasi hiyo na kueleza matumaini yake makubwa ya utendaji kazi wa kiongozi huyo.

Aidha, Rais Dk. Shein alimuhakikishia kiongozi huyo kwamba kwa upande wa Zanzibar atapewa kila aina ya msaada na mashirikiano ili aweze kufanikisha kazi zake vyema hasa ikizingatiwa kuwa ofisi yake ipo hapa Zanzibar.

Nae Jaji Francis Mutungi aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa mashirikiano makubwa inayoyapata Ofisi yake hatua ambayo imeweza kusaidia kufanikisha vyema kazi za Ofisi hiyo.

Mapema Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Mohammed Ali Ahmed alitoa shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa kuteuliwa kushika wadhifa huo ambao aliahidi kuutumikia vyema.

Naibu Msajili huyo ameahidi kutekeleza vyema majukumu yake ya kazi kwa kusimamia vyema sheria za vyama vya siasa nchini huku akieleza kuwa atahakikisha anatekeleza ipasavyo sheria hizo kwa lengo la kuwatumikia wananchi ili waweze kupata maendeleo sambamba na kuimarisha amani, utulivu, umoja na mshikamano mkubwa uliopo nchini.

Rais Dk. John Magufuli alimteua Mohammed Ali Ahmed tarehe 20 Juni 2018 ambapo kabla ya uteuzi huo alikuwa Mwanasheria na mtafiti katika Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar ambaye amechukua nafasi iliyoachwa wazi na Rajab Baraka Juma ambaye amestaafu. 
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini Mhe. Jaji Francis Mutungi  katika ukumbi wa Ikulu mjini Zanzibar katika hafla ya utambulisho wa Naibu Msajili mpya wa Vyama vya Siasa Mhe. Mohammed Ally ahmed Ikulu mjini Zanzibar Septemba 25, 2018 
Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini Mhe. Jaji Francis Mutungi na Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa Mhe. Mohammed Ally Ahmed (kushoto) wakimsilikiza kwa makini Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein wakati wa hafla ya utambulisho Ikulu mjini Zanzibar Septemba 25,2018  Picha na Ikulu Zanzibar

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad