HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, June 8, 2018

MAKAMU WA RAIS MGENI RASMI KONGAMANO LA BIASHARA NA UWEKEZAJI KATI YA TANZANIA NA MALAWI

Na Said Mwishehe, Globu ya jamii
MAKAMU wa Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na Malawi ambalo litafanyika Julai 26 hadi Julai 27 mwaka huu mkoani Mbeya.

Kongamano hilo limeandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kwa kushirikiana na Kituo cha Uwekezaji  Tanzania(TIC), Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania(TanTrade) pamoja na Taasisi ya Biashara na Uwekezaji ya Malawi(MITC).

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika ofisi za TIC, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla amesema kauli mbiu ya kongamano hilo ni "Kuimarisha Uhusiano wa biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Malawi" huku lengo la kongamano hilo likiwa kuwatanisha wafanyabiashara /wawekezaji  wa nchi hizo mbili ili kubaini fursa mbalimbali za kibiashara na uwekezaji.

Ambapo amefafanua zitawezesha kuanzisha na kuendeleza miradi katika sekta za viwanda ,usafirishaji,utalii, uvuvi, kilimo ,madini, elimu, afya, benki, mawasiliano, tehama na biashara kwa ujumla.

Pia amesema sambamba na kongamano hilo kutakuwapo na mikutano ya wafanyabiashara (B2B), mikutano ya watendaji wa Serikali(G2G) na mikutano kati ya Serikali na wafanyabiashara (B2G) kutoka nchi hizo mbili.

"Tayari mkoa wa Mbeya umeona umuhimu wa wa kongamano hili na una kila sababu za kuandaa  na kuratibu kwasababu unaona fursa na mkoa upo tayari kwa kuna miundombinu yote muhimu,'amesema Makalla.
Ameongeza katika kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji Serikali kupitia Mkoa wa Mbeya tayari imeanza kufungua milango ya uwekezaji kwa kuwekeza katika miundombinu ya kiuchumi ikiwamo uwepo wa meli mbili ambapo moja ya mizigo na nyingine ya abiria inatengenezwa katika bandari ya Itungi na kuanza ujenzi wa kituo kimoja cha forodha katika mpaka wa Kasumulu.

Pia Makalla amesema Serikali imekwishatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa  bandari kavu katika eneo la Inyala kwa lengo la kuwezesha upokeaji na uhifadhi wa bidhaa moja kwa moja kutoka bandari ya Dar es Salaam.

Akifafanua kuhusu komgamano hilo Makalla amesema ni bure kwa washiriki isipokuwa wadau wenye nia ya kushiriki wanahamasishwa kupakua na kujaza fomu ya usajili kupitia tovuti ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ambayo ni www.mbeya.go.tz na baadae kuziwasilisha kwa barua pepe kupitia ;ras.mbeya.go.tz.

Pia kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania ambayo ni http://www.tic.go.tz.displayListPublication na baadae kutuma kwa diana.ladislaus@tic.go.tz/ au tovuti ya TanTrade ambayo www.tantrade.go.tz na kisha kutuma kwa info@tantrade.go.tz.

Pia kupitia tovuti ya Kituo cha Biashara na uwekezaji Malawi ambayo  ni https://mitc.mw/ na kisha kutuma kupitia anuani ;info@mitc.mw.

"Fomu hizo ziwasilishwe kwa barua pepe zilizoanishwa kabla ya Julai 16 mwaka huu.Tunaomba wadau wote kushiriki ili kuibua fursa za uwekezaji na kibiashara kwa faida za wananchi wote,"amesema Makalla.
 Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla, kulia akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Malawi litakalofanyika Julai 26 na 27 jijini Mbeya, kushoto ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) John Mnali.
 Baadhi ya watendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla (hayupo pichani) kuhusu kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Malawi litakalofanyika Julai 26 na 27 jijini Mbeya.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini, Godfrey Simbeye, kulia akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Malawi litakalofanyika Julai 26 na 27 jijini Mbeya.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini, Godfrey Simbeye, kulia akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu kongamano la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Malawi litakalofanyika Julai 26 na 27 jijini Mbeya, katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya , Amos Makalla na kushoto ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) John Mnali. Picha na Eliphace Marwa - Maelezo

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad