Na Munir Shemweta, Tabora
Kamishna
Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi Idrisa Keyera amesema manispaa ya
Tabora pekee inadai zaidi ya shilingi bilioni sita kwa wamiliki wa ardhi
na mashamba mkoani humo kama kodi ya ardhi.
Kayera
alisema hayo jana wakati akizungumza na watendaji kata wa Manispaa ya
Tabora alipokutana na watendaji hao kuhamasisha ulipaji wa kodi ya ardhi
na mashamba katika mkoa huo, mkutano uliofanyika ukumbi wa VETA Tabora.
Alisema,
mpaka kufikia sasa katika manispaa ya Tabora zimekusanywa jumla ya
shilingi bilioni 3.2 ikiwa ni pungufu ya malengo waliyojiwekea ya
kukusanya shilingi bilioni nne katika mwaka huu wa fedha unaoishia juni
mwaka 2018.
Alisema,
kanda yake inayohusisha mikoa ya Tabora, Shinyanga, Kigoma na Katavi
imeanza kuchukua hatua kwa wadaiwa sugu wa kodi za ardhi kwa kuwapatia
hati za madai ambapo wahusika watatakiwa kulipa madeni yao ndani ya wiki
mbili na wasipofanya hivyo wanapelekwa mahakamani na huko vifaa vyao au
nyumba zitauzwa kufidia deni huku umiliki nyumba ama shamba ukifutwa.
‘’Unapopelekwa
mahakamani uwezekano wa kushinda haupo na pia itakulazimu kulipa
gharama za madadlali kwa kushindwa kulipa’’ alisema Kamishana Msaidizi
Kayera.
Kwa
mujibu wa Kayera, kikao chake na watendaji wa kata za manispaa ya
Tabora ni moja ya harakati za ofisi yake ya Kanda ya magharibi
kuhakikisha kodi ya serikali inapatikana sambamba na kuwashirikisha
watendaji kuwatambua na kuwapelekea hati za madai wadaiwa sugu wa kodi
ya ardhi katika mitaa yao ili kuwabana waweze kulipa madeni yao.
Aidha,
Kamishna Msaidizi wa ardhi Kanda ya Magharibi alisema, utaratibu wa
kulipa kodi ya ardhi kwa sasa ni rahisi kwani unaweza kulipia kwa njia
ya simu na malipo hayo yanafanywa na wananchi waliopimiwa maeneo yao
ingawa serikali iko katika hatua za kuhakikisha maeneo yote ya mijini
hata yale yasiyopimwa wamiliki wake wanalipa kodi ya ardhi.
Kwa
upande wao watendaji wa kata za manispaa ya Tabora pamoja na kuunga
mkono jitihada za uhamasishaji wa ulipaji kodi ya ardhi wametaka
kupatiwa taarifa pamoja na ramani za maeneo yao kwa lengo la kutambua
maeneo hasa pale yanapotokea mabadiliko ya matumizi ya ardhi katika
maeneo husika jambo linalowapa wakati mgumu wakati wa kutekeleza
majukumu.
Hata
hivyo, wametaka halmashauri ya Manispaa ya Tabora na ofisi ya Kamishna
wa Ardhi Kanda ya Magaharibi kuwawezesha wakati wa kufanya kazi ya
kuwapelekea wadaiwa wa kodi ya ardhi ikiwemo kuwapa motisha hasa wale
watendaji wanaoishi maeneo ya pembezoni ambapo watendaji wake wamekuwa
na wakati mgumu kuwafikia wananchi kutokana na kukosa nauli na gharama
nyingine.
Wizara
ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia ofisi zake za Kanda
imekuwa na kampeni kamambe ya kuhamasisha wananchi kulipa kodi ya ardhi
na mashamba kabla ya Juni 30 mwaka huu wa 2018, huku wale wadaiwa sugu
wakipatiwa hati za madai ili waweze kulipa madeni yao kabla ya hatua za
kisheria hazijachukuliwa dhidi yao.
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi Idrisa Kayera akizungumza na watendaji wa Kata za Manispaa ya Tabora jana wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji wa kodi ya ardhi katika kanda hiyo mkoani Tabora, kampeni inayoendeshwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kushoto ni Mwanasheria wa Kanda Ramadhani Jongo.
Watendaji wa Kata za Manispaa ya Tabora wakimsikiliza Kamishna Msaidizi wa Ardhi wa Kanda ya Magharibi Idrisa Kayera (hayupo pichani) wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji kodi ya ardhi katika kanda ya magharibi mkoani Tabora, kampeni inayoendeshwa ma Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mmoja wa watendaji wa kata za Manispaa ya Tabora akichangia maoni wakati wa kampeni ya uhamasishaji wa kulipa kodi ya ardhi kanda ya magharibi ulioendeshwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi Idrisa Kayera akiwaonesha Hati ya Madai watendaji wa Kata za Manispaa ya Tabora wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji wa kodi ya Ardhi na Mashamba katika kanda hiyo mkoani Tabora jana, kampeni inayoendeshwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi akimpatia Hati za Madai Mtendaji wa Kata ya Kaloleni Manispaa ya Tabora Monica Toba kwa ajili ya kuziwasilisha kwa wadaiwa wa kodi ya ardhi katika kata yake wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji kodi ya ardhi mkoa wa Tabora.
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi akimpatia Hati za Madai Mtendaji wa Kata ya Mbugani Manispaa ya Tabora Paul Masunga kwa ajili ya kuziwasilisha kwa wadaiwa wa kodi ya ardhi katika kata yake wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji kodi ya ardhi mkoa wa Tabora.
Mmoja wa waendesha Bajaji katika Manispaa ya Tabora akibandika Stika ya uhamasishaji wa kulipa kodi ya ardhi katika Bajaji yake wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji kodi ya ardhi katika kanda ya magharibi mkoani Tabora, kampeni iliyoendeshwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Waendesha Bodaboda katika kituo cha mabasi katika manispaa ya Tabora wakiangalia vipeperushi vinavyoeleza njia rahisi ya kulipa kodi ya ardhi kwa simu wakati wa kampeni ya kuhamasisha ulipaji kodio ya ardhi katika mkoa wa Tabora, kampeni iliyoendeshwa na Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Picha zote na Munir Shemweta Wizara ya Ardhi.
No comments:
Post a Comment