HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, April 4, 2018

Waziri Jafo asimamisha Ujenzi wa Vivuko Barabara ya Lamelock - Loltepes - Sunya


Nteghenjwa Hosseah, Kiteto

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo amesimamisha ujenzi wa vivuko vyote katika ujenzi wa barabara ya Namelock-Loltepes Sunya yenye urefu wa Km 88.1 inayojengwa katika Wilaya ya Kiteto na Mkandarasi Deniko Constraction Ltd.

Waziri Jafo ametoa agizo hilo mapema jana wakati wa ziara yake Wilayani humo kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na kubaini mapungufu makubwa katika ujenzi wa vivuko zaidi ya kumi alivyovipitia ndipo alipoagiza kusitisha ujenzi huo mara moja hadi hapo Wataalamu wa Wakala wa barabara Mijini na Vijijini (TARURA) watakapofika kukagua barabara ma kuwasilisha ripoti.

Aidha kutokana na hali hiyo ya aligiza Mkandarasi aliyepewa kazi ya ujenzi wa barabara hiyo Deniko Construction sambamba na Mhandisi Mshauri Luptain Consult Ltd, Mhandisi Consulting Engineers pamoja na ACE Consultant kufika Ofisini kwake mara moja kutoa maelezo ya kina ya mapungufu hayo yaliyojitokeza katika ujennzi wa barabara hiyo.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Kulia) akiendelea na ukaguzi wa ujenzi wa Vivuko katika barabara Namelock-Sunya wakati wa ziara yake Wilayani Kiteto.

“Ni mara ya tatu sasa nakuja kukagua Barabara hii na kila mara nabaini changamoto tofauti sjui kuna tatizo gani nahitaji kusikia zaidi kutoka kwa wataalamu wa pande zote ili tutafute suluhisho kwa pamoja”Alisema Jafo.

Aliongeza kuwa hapo awali Barabara hii iligawanywa kwa wakandarasi wajenzi wawili ambaye ni huyu Deniko alikuwa anajenga upande mmoja wenye Km 44 na Km 44 zilizobakia alipewa Maginga Construction ambaye alishindwa kabisa kazi hii ndipo nilipoagiza taratibu zifuatwe ili kuvunja mkataba wa awali na kazi ile apewe Mkandarasi mwingine.

“Kazi hiyo aliongezewa Deniko Construction ambaye kwa sasa ndiye anayejengwa barabara hii yote yenye Km 88. Hapo awali kazi yake ilionekana nzuri sana na ya kuridhisha lakini baada ya mvua za msimu huu mapungufu makubwa yamebainika hasa katika vivuko vyote vilivyojengwa haviendani na mahitaji ya barabara hii” Alisema Jafo.
Huu ni muonekano wa baadhi ya Kivuko kinachojengwa katika barabara ya Namelock – Loltepes – Sunya ambavyo Waziri Jafo amesimamisha ujenzi wake kutokana na dosari zilizojitokeza.

Naye Kaimu Meneja wa TARURA Wilaya ya Kiteto Elias Paul alisema kuwa tatizo lililobainika katika ujenzi wa vivuko hivyo ni Vivuko hivyo haviendani na wingi wa maji ya maji yanayopita na vipenyo vya vivuko ni vidogo hivyo havina uwezo wa kuhimili maji na takataka zingine zinazotakiwa kupita hapo na ni rahis sana kuziba na hata kivuko chote kubebwa na maji ndani ya kipindi kifupi.

Mradi wa ujenzi wa barabara ya Nmelock – Loltepes – Sunya unatekelezwa na Serikali kupitia Fedha za wafadhili kutoka Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Watu wa Marekani (USAID) chini ya mpango wa (FEED FOR FUTURE) unaotekelezwa katika Wilaya Nne Nchini ambazo ni Kilombero, Mvomero, Kongwa na Kiteto.

Wilaya ya Kiteto kupitia kwa Wakala wa Babarabara za Mijini na Vijiji (TARURA) inahudumia mtandao wa barabara zenye jumla ya urefu wa Km 1,088.35 kati ya barabara hizo km 2.8 ni za Lami, Changarawe Km 132 na Udongo Km 955.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Kulia) akitoa maelekezo wakati wa ukaguzi wa ujenzi wa barabara ya Namelock – Loltepes – Sunya yenye urefu wa Km 88 wakati wa ziara yake Wilayani Kiteto. 
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Kushoto) akikagua ujenzi wa Vivuko katika barabara ya Namelock-Loltepes- Sunya yenye urefu wa Km 88 iliyopo katika Wilaya ya Kiteto.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad