HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, April 7, 2018

SERIKALI YAPATA MKOPO WA SHILINGI BILIONI 34 KUTOKA MFUKO WA MAENDELEO YA KIUCHUMI WA KUWAIT

Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
Serikali ya Kuwait kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), na Serikali ya Tanzania zimetiliana saini  rasimu ya mkataba wa  kuipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu wa dola milioni 15.3, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 34, kwa ajili ya mradi wa  kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma,  lenye ukubwa wa  hekta 3,000.

Rasimu hiyo ya Mkataba imesainiwa na Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait,  Dkt. Abdulrida Bahman na  kwa upande wa Tanzania ikisainiwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Khatibu Kazungu, mjini Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb)  amesema hatua hiyo imfikiwa baada ya timu ya wataalamu kutoka Kuwait kutembelea eneo la mradi mkoani Kigoma na kuridhishwa na umuhimu wake kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo na taifa kwa ujumla.

 “Mradi huo una umuhimu mkubwa kwa watanzania kwa kuwa wataweza kuwa na kilimo cha umwagiliaji cha Mpunga na Mbogamboga kwa mwaka mzima badala ya kilimo cha msimu cha kutegemea mvua, na katika siku zijazo Kigoma itakua miongoni mwa mikoa inayozalisha mchele kwa wingi”, alisema Dkt. Mpango.

Dkt. Mpango amesema kuwa Serikali ya Tanzania na Kuwait zitatia saini mkataba rasmi wa mkopo huo wenye masharti nafuu ifikapo mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu ili mradi huo uanze kutekelezwa ili kuongeza kipato cha wananchi na  kuwa na uhakika wa chakula.

Amesema Nchi ya Kuwait imekuwa ikiisaidia Tanzania katika kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ya ukarabati wa Hospitali ya Mnazi mmoja, Zanzibar kwa kiasi cha dola za Marekani milioni 13.6 sawa na shilingi bilioni 31.

"Kwa upande wa Tanzania Bara wametoa mkopo nafuu wa shiingi bilioni 115 kwa ajili ya kuboresha barabara ya Chaya hadi Nyahua (km 85) kwa kiwango cha lami ambayo ni muhimu kwa kuwa inaunganisha mikoa ya Magharibi mwa Tanzania" aliongeza Dkt. Mpango

Miradi mingine ambayo  nchi hiyo imeonesha nia ya kuisaidia nchi, ni pamoja na ujenzi wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza, uboreshaji wa barabara ya kutoka Morogoro hadi Dodoma na ujenzi wa barabara za mzunguko za kuingia na kutoka mjini Dodoma ambazo zitasaidia kuondoa msongamano wa magari yanayopita katikati ya mji huo kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu na vyombo vya moto baada ya Makao Makuu ya Serikali kuhamia Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mpango ameishukuru nchi ya Kuwait kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait, kwa nia yake njema na thabiti katika kusaidia nchi ya Tanzania kutekeleza kwa mafanikio miradi ya Maendeleo ya kiuchumi katika nia yake ya kupata maendeleo Stahiki.

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait, Dkt. Abdulrida Bahman, ameishukuru Serikali ya Tanzania kupitia Waziri wa Fedha na Mipango kwa ukarimu pamoja na Idara ya Taifa ya Umwagiliaji kwa ushirikiano mzuri katika hatua za kufanikisha utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji  wa Bonde la Luiche, Mkoani Kigoma.

“Tumetembelea eneo la mradi kwa takribani wiki mbili tumejionea uzuri wa nchi hii na fursa zilizopo, hii ni nchi tajiri na inaweza kuwa tajiri kuliko Kuwait kwa kuwa kila kitu kinachoweza kufanya nchi hii iwe tajiri kipo”.Alieleza Dkt. Bahman.

Amesema mradi huo wa umwagiliaji hautakuwa wa mwisho kupewa fedha na mfuko huo bali utaendelea kusaidia kutekeleza miradi mingine mingi kama ilivyokuwa ikifanya, kutokana na ushirikiano mzuri, wa kihistoria, na wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango (SERA), Dkt. Khatibu Kazungu (kushoto) na Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), Dkt. Abdulrida Bahman, wakibadilishana rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma,
Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kulia), akiagana na Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), Dkt. Abdulrida Bahman, baada ya tukio la kusainiwa kwa  rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma, tukio lililofanyika mjini Dodoma.
Ujumbe wa wataalamu kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), ukiongozwa na  Dkt. Abdulrida Bahman (wa tano kutoka kulia), na ujumbe kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, ukiongozwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (wa nne kutoka kulia), wakiwa katika picha ya pamoja nje ya Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango Mjini Dodoma, baada ya tukio la kusainiwa kwa  rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango (SERA), Dkt. Khatibu Kazungu (kushoto) akisaini rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma.
Ujumbe wa wataalamu kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), ukiongozwa na  Dkt. Abdulrida Bahman (kushoto), wakisikiliza maelezo kutoka kwa Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango (Mb) (hayupo pichani), kabla ya tukio la kusainiwa kwa  rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango (Mb) (kulia), akiongoza mazungumzo kabla ya tukio la kusainiwa kwa  rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 34 kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma.
Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), Dkt. Abdulrida Bahman, akitia saini rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (kulia), akiagana na mmoja wa wajumbe kutoka Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), Dkt. Abdulrida Bahman, baada ya tukio la kusainiwa kwa  rasimu ya mkataba wa mkopo wa dola milioni 15.3 za Marekani, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 34.4, kwa ajili wa kujenga mradi wa kilimo cha umwagiliaji maji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma, tukio lililofanyika mjini Dodoma.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano-Wizara ya Fedha na Mipango)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad