HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, April 27, 2018

SERIKALI YAIPELEKA SERA YA TAIFA YA MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI KWA WADAU KUPATA MAONI

Na Mwandishi Wetu- Arusha
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imedhamiria kufanya mabadiliko katika Sera zake mbalimbali ili kuweza kuendana na wakati na kuwezesha kushirikiana na wadau wa maendeleo kutoa huduma kwa watanzania.

Katika kulifanikisha hilo Wizara imeamua kuipeleka Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2001 kwa wadau ili iweze kutolewa maoni na baadae kufanyiwa marekebisho kuiwezesha kuendana na wakati.

Akifungua kikao kazi cha wadau wa Mashirika Yasiyo ya kiserikali kuijadili Sera ya Taifa ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali Jijini Arusha, Katibu Mkuu Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Bibi Sihaba Nkinga amesema  kuwa  maoni ya wadau ni muhimu sana  katika mchakato wa maboresho wa Sera hiyo.

Bibi. Sihaba Nkinga ameleza kuwa Serikali imeamua kuwashirikisha wadau hao kwani kwa asilimia kubwa ndio watekelezaji wa Sera hiyo katika majukumu yao ya kila siku.

Ameongeza kuwa Serikali inatambua mchango wa kazi zinazofanywa na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini na zoezi hili la kuiboresha Sera hiyo litaleta mageuzi makubwa katika Sekta.

Katibu Mkuu Sihaba Nkinga amesisitiza kuwa upatikanaji wa Sera nzuri utasaidia kupata Sheria nzuri na kukiwa na Sheria nzuri itasaidia utendaji mzuri wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini.

“Tuitumie fursa hii kujadiliana vizuri ili tupate Sera itakayopeleka Sekta yetu ya NGOs mbele” alisisitiza Bibi. Sihaba.

Kwa upande wake Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini Bw. Marcel Katemba amewataka wadau kuzingatia kikao kazi hicho kwani ndio fursa ya kutoa maoni yao ya kuiboresha Sekta ya Mashirika ya Yasiyo ya Kiserikali nchini

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Bw. Nicholous Zakaria ameishukuru Serikali kwa ushirikiano na kuahidi kuendelea kusimamia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na kuratibu upatikanaji wa maoni kwa ajili ya maboresho ya Sera ya Mashirka Yasiyo ya Kiserikali nchini.
  Katibu Mkuu Idara Kuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Sihaba Nkinga akizungumza na wadau wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali wakati akifungua kikao kazi kilichofanyika Jijini Arusha kilichowakutanisha wadau hao kujadili maboresho ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
 Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Marcel Katemba akitoa ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali  ya kisera wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi kilichofanyika Jijini Arusha kilichowakutanisha wadau wa NGOs kujadili maboresho ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
 Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Nicholous Zakaria  akieleza kuhusu umuhimu wa Baraza katika kuratibu utendaji kazi wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali nchini wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi kilichofanyika Jijini Arusha kilichowakutanisha wadau hao kujadili maboresho ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
  Baadhi ya wadau wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali wakifuatilia mada mbalimbali katika kikao kazi kilichofanyika Jijini Arusha kilichowakutanisha wadau hao kujadili maboresho ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.
Katibu Mkuu Idara Kuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bibi Sihaba Nkinga akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini mara baada ya kufungua kikao kazi kilichofanyika Jijini Arusha kilichowakutanisha wadau hao kujadili maboresho ya Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali watatu kulia waliokaa  ni Mkurugenzi na Masajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Bw. Marcel Katemba. Picha na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad