Na Rehema Isango, Mara
TIMU ya watalaamu wa upimaji ardhi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi nchini na Taasisi za Usimamizi wa ardhi Kenya zimekutana wilayani Tarime mkoani Mara kwa lengo la kuanza utekelezaji wa uhakiki na kuimarisha mpaka wa kimataifa baina ya nchi hizi mbili.
Mwanzoni mwa Machi mwaka hu, Naibu Waziri wa Adhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dk.Angeline Mabula alitangaza azma ya Serikali ya Tanzania kuanza kuimarisha mipaka yake kwa nchi jirani za Kenya na Uganda.
Hiyo ilitokana na ziara yake ya kukagua mpaka wa Tanzania na Kenya katika Mbuga ya Wanyama ya Taifa ya Serengeti iliyopo mkoani Mara.
Kwa mijibu wa Wazara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, imefafanua hatua ya uhakiki na uimarishaji wa alama za mipaka ya mikataifa inatokana na mpaka huo kuwa wa siku nyingi na haukuwa wazi katika maeneo mengi.
Pia baadhi ya alama hizo kuharibiwa, kung’olewa au kuchakaa na hivyo kusababisha Serikali pande zote kushindwa kusimamia kwa ufanisi shughuli za mipakani, rasilimali za nchi pamoja na ulinzi na usalama.
Imeelezwa na timu ya wataalam kutoka Wazara hiyo kuwa katika uimarishaji wa alama hizo za mipaka hivi sasa, kutaongezwa alama mpya ndogo zinazoonana kwa umbali wa mita 100 na kubainisha eneo la ardhi huru kwa kila upande wa nchi (buffer zone).
Mpaka kati ya Tanzania na Kenya una jumla ya urefu wa kilommita 760 kuelekea Bahari ya Hindi ambapo awamu ya kwanza ya kazi ya uimarishaji mpaka inayofanyika hivi sasa itahusisha urefu wa kilomita 238 kutoka kando ya Ziwa Victoria mkoani Mara hadi Ziwa Natron mkoani Arusha.
Pia baadae kazi ya uhakiki na uimarishaji wa mipaka itaendelea katika mikoa ya Kilimanjaro na Tanga na kisha itafanyika katika maeneo yote yanayohusika na mipaka ya kimataifa nchini.
Uimarishaji wa mipaka ya kimataifa nchini umefanyika mara ya mwisho mwaka 1975 kwa kurudishia alama ambazo ziliondolewa na kuongeza nyingine mpya kwa kuzingatia alama zilizopo.
Mbali na Kenya nchi nyingine zinazopakana na Tanzania ni; Msumbiji, Malawi, Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Burundi, Rwanda, Uganda pamoja na visiwa vya Komoro na Shelisheli.
Mkuu wa mchakato wa Uhamasihaji katika kazi ya kuhakiki na kuimarisha mipaka ya Kimataifa kati ya Tanzania na Kenya Raymond Bagenda kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi akizungumza wakati wa kikao cha pamoja cha wataalam wa masuala ya upimaji ardhi kutoka katika ofisi za Serikali za nchi zote mbili. Kikao hiko kilichofanyika wilayani Tarime mkoani Mara kinapanga namna ya kutekeleza kazi hiyo kwa pamoja. Kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Rais nchini Kenya inayohusika na Usimamizi wa Mipaka ya Kimataifa (KIBO) Joseph Rotich.
Baadhi ya Wataalam wa masuala ya upimaji ardhi pamoja na maafisa mbalimbali kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na katika ofisi zingine za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakifuatilia mazungumzo kuhusu namna ya kutekeleza kazi ya uhakiki na uimarishaji wa mipaka ya kimataifa kati ya Kenya na Tanzania.
Wataalam wa masuala ya upimaji ardhi pamoja na maafisa mbalimbali kutoka katika ofisi za Serikali za nchi zote mbili waliojumuika pamoja wilayani Tarime mkoani Mara kupanga namna ya kutekeleza kazi ya uhakiki na uimarishaji wa mipaka ya kimataifa kwa pamoja. Wa tatu kutoka kulia (walioketi) ni Mkuu wa Msafara wa wataalam kutoka Tanzania Huruma Lugala na kulia kwake ni Mkuu wa Msafara kutoka Kenya Julius Rotich.
No comments:
Post a Comment