UMOJA
wa Mataifa umeingia makubaliano ya kuimarisha upatikanaji na usambazaji
wa habari za maendeleo na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
pamoja na chama cha Maafisa Mawasiliano Serikalini (TAGCO).
Makubaliano
hayo yamelenga kuimarisha upatikanaji na utoaji habari wa pamoja kuhusu
mpango wa maendeleo wa miaka mitano wa serikali na malengo ya maendeleo
endelevu ya dunia.
Kwa
mujibu Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa Bw. Alvaro
Rodriguez makubaliano hayo yatachagiza kupatikana kwa habari kuhusiana
na utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu unaokwenda sambamba na
mpango wa maendeleo wa miaka mitano wa Tanzania.
Akizungumzia
malengo hayo kwa maofisa wa mawasiliano wa serikali wanaokutana mjini
Arusha kwa semina ya wiki moja iliyoandaliwa kwa pamoja kati ya TAGCO na
Wizara ya Habari na kufadhiliwa na Umoja wa Mataifa, alisisitiza kuwa
malengo hayo yanahitaji kuwasilishwa kwa wananchi na pia kupigiwa
chapuo.
Aliwataka
maofisa mawasiliano hao wa serikali kufanyakazi ya uragibishi na pia
kuwasiliana ana kwa ana na jamii kuhusu masuala mtambuka kama kuhifadhi
mazingira,kuondoa tatizo la ukeketaji (FGM) na kupambana na ukatili wa
kijinsia dhidi ya wanawake na watoto katika kufanikisha mpango wa
maendeleo wa kitaifa na ule wa dunia.
Kwa
upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa Maelezo Dk.
Hassan Abbas alisema kwamba kwa sasa wizara ya habari iko katika
mchakato wa kuandaa makubaliano na Umoja wa Mataifa yatakayogusa masuala
ya mawasiliano katika utekelezaji wa mpango wa pili wa miaka mitano wa
maendeleo m na malengo ya maendeleo endelevu ya dunia.
Aidha
alisema semina hiyo itawapatia mafunzo mengi maofisa hao ikiwa ni
pamoja na kutembelea maeneo yenye miradi iliyopata mafanikio na kujenga
athari chanya kwa jamii.
Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Bw. Alvaro Rodriguez akiwasilisha mada kuhusu malengo ya maendeleo ya milenia na uhusiano wake na mpango wa maendeleo wa miaka mitano wakati wa mkutano wa 14 wa Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini unaoendelea Jijini Arusha.
Ofisa Habari wa taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa Takukuru akiuliza namna ambavyo mapambano dhidi ya rushwa yanavyoweza kuwa sehemu ya utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu.
Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Bw. Alvaro Rodriguez (kushoto) na Katibu Mkuu Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Bi Suzan Mlawi (kulia) wakifuatilia mada kuhusu malengo ya maendeleo ya milenia na uhusiano wake na mpango wa maendeleo wa miaka mitano wakati wa mkutano wa 14 wa Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini unaoendelea Jijini Arusha.
Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa Maelezo Dk. Hassan Abbas akizungumza na waandishi wa habari nje wakati wa mkutano wa 14 wa Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini unaoendelea Jijini Arusha.
Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini wakifuatilia mada kuhusu malengo ya maendeleo ya milenia na uhusiano wake na mpango wa maendeleo wa miaka mitano ikiwasilishwa na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Bw. Alvaro Rodriguez hayupo pichani katika mkutano huo wa 14 unaoendelea jijini Arusha.
Sehemu ya washiriki wakati wa mkutano wa 14 wa Maafisa Habari, Mawasiliano na Uhusiano Serikalini unaoendelea Jijini Arusha.
No comments:
Post a Comment