HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, March 23, 2018

BITEKO ATOA WITO KWA WADAU KUZINGATIA SHERIA MPYA YA MADINI

Na Veronica Simba – Dodoma
Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya madini nchini, kuzingatia sheria mpya ya madini ambayo inaelekeza namna bora ya usimamizi wa sekta hiyo.
Alitoa wito huo jana, Machi 22 mwaka huu kwa nyakati tofauti, alipokuwa katika ziara ya Mkoa wa Dodoma, kukagua shughuli mbalimbali za madini.
 “Moja ya mambo muhimu ambayo sheria mpya ya madini inaelekeza ni kutunza rekodi za uzalishaji wa madini ili Serikali iweze kujua ni kitu gani kinazalishwa na hatimaye tuweze kujua kodi gani zinalipwa na wenye leseni husika,” alifafanua.
Aidha, Naibu Waziri aliwataka wenye leseni kushirikiana na wachimbaji wadogo wa madini ili waweze kunufaika kupitia kazi wanazofanya. “Kwa maneno mengine, asitokee mtu wa kumnyanyasa mchimbaji mdogo eti kwa sababu tu ana leseni,” alisisitiza.
Akizungumza na wamiliki wa leseni pamoja na wachimbaji wadogo wa madini wa dhahabu katika eneo la Nholi wilayani Bahi, Naibu Waziri alipongeza uamuzi wao wa kuanzisha kampeni ifikapo Aprili mwaka huu, kupanda miti kwenye maeneo yao ili kurejesha hali nzuri ya mazingira.
Vilevile, aliwaagiza kuweka wigo kuzunguka mashimo yaliyo wazi ili kuonyesha hali ya tahadhari kuwa eneo hilo ni hatari na linaweza kusababisha ajali, ikiwa ni hatua mojawapo ya kuzingatia usalama migodini.
Akizungumzia changamoto kuu iliyowasilishwa kwake na wachimbaji wa mawe ya nakshi aina ya Granite na Dorelite Dyke katika maeneo ya Itiso wilayani Chamwino na Ntyuka Wilaya ya Dodoma Mjini, kuhusu vibali vya kusafirisha mawe hayo nje ya nchi, Biteko alisema kuwa awali Serikali ilisimamisha utoaji vibali hivyo kuzuia usafirishaji wa mawe ghafi nje ya nchi.
“Changamoto iliyokuwepo awali, ni kuwa wako watu walikuwa wanasafirisha madini nje ya nchi yakiwa ghafi, yanaongezwa thamani huko kasha tunarejeshewa sisi tununue bidhaa hizo.”
Akifafanua zaidi, alisema kuwa, jambo linalotia moyo ni kwamba uongezaji thamani madini hivi sasa umeanza kufanyika nchini kwa kiwango kinachotakiwa kusafirishwa nje ya nchi. Alisema, jambo hilo hilo litaleta manufaa kwani thamani, ajira na teknolojia vyote vitabaki ndani na manufaa yatabaki ndani ya nchi pia.
Alipongeza wachimbaji wa mawe ya nakshi wa Itiso na Ntyuka ya kudhamiria kujenga mitambo ya uongezaji thamani mawe hayo katika maeneo husika.
Alisema kiu ya Serikali ni kuona madini yanayochimbwa Tanzania, yanaongezwa thamani nchini na hatimaye kusafirisha bidhaa zinazotokana na madini hayo na kuziuza katika nchi nyingine mbalimbali na siyo vinginevyo.
Aidha, Naibu Waziri aliwasisitiza wamiliki wote wa leseni za madini kufanya kazi zao huku wakizingatia kujenga mahusiano mema na jamii zinazowazunguka.
Alisema kuwa kmujibu wa kanuni mpya iliyopo hivi sasa, mwenye leseni anapaswa kuwasilisha mpango wake wa utoaji huduma kwa jamii (CSR) kwenye Halmashauri husika ili iuthibitishe mpango huo kabla ya utekelezaji wake.
“Ule utaratibu wa mtu anajifungia ofisini, anasema nitawajengea shule pasipo Serikali ya Kijiji au Wilaya kujua, tumeufuta kwa sababu mwanzo ulikuwa unatengeneza matatizo mengi,” alifafanua Biteko.
Alisema, Serikali itafanya kazi ya kuangalia na kuthibitisha thamani halisi ya fedha zitakazotumika katika mpango huo, ili kujiridhisha.
Naibu Waziri alimwagiza Afisa Madini Mkazi wa Dodoma Silimu Mtigile kuandaa na kuendesha semina siku ya Jumatatu, Machi  26 mwaka huu, kwa ajili ya wachimbaji wa eneo la Nholi kuhusu sheria mpya ya madini, kufuatia maombi waliyowasilisha kwake alipokuwa akizungumza nao.
Hata hivyo, alisema kuwa semina za aina hiyo zitaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini kote ili kuwajengea uelewa wa sheria hiyo mpya wadau wa madini waweze kufahamu haki na wajibu wao.
Akizungumzia suala la baadhi ya watu kueneza propaganda kuhusu sheria hiyo kuwa ni kandamizi; Biteko aliwataka watanzania kupuuza kauli hizo kwani sheria husika imelenga kuwanufaisha watanzania na siyo kinyume chake.
“Kama kuna bepari anadhani kwamba tunaweza kurudi nyuma katika hili, amekwama. Heri tuwe na wawekezaji wachache wanaofuata sheria kuliko kuwa nao wengi wenye kutaka tu kuchuma mali na kuondoka.”
Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Biteko aliambatana na Afisa Madini Mkazi wa Dodoma Silimu Mtigile, wataalam kutoka wizarani na ofisi ya madini Dodoma pamoja na viongozi wa Wilaya na Halmashauri akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Bahi Elizabeth Kitundu.
 Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko, akizungumza na wananchi wa Nholi wilayani Bahi, kulipo na machimbo ya madini ya dhahabu, alipowatembelea Machi 22 mwaka huu, kujionea shughuli wanazofanya.
 Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (wa pili kutoka kushoto) akiwa na viongozi mbalimbali wa Wilaya na Halmashauri, wakati wa ziara yake kukagua shughuli za uchimbaji dhahabu katika eneo la Nholi, Wilaya ya Bahi, Machi 22 mwaka huu. Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Elizabeth Kitundu.
 Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Dodoma, Silimu Mtigile (kulia) akifafanua jambo kwa wananchi wa Kijiji cha Nholi wilayani Bahi, wanaojishughulisha na uchimbaji wa dhahabu; wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (kushoto), Machi 22 mwaka huu

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad