HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, February 5, 2018

WAZIRI MAHIGA AHITIMISHA ZIARA YAKE KOREA KUSINI

Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa kwenye mazungumzo na Bw. Chang Yaong Hun, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Exim ya Korea Kusini. Viongozi hao wawili walikutana kwenye ofisi za Benki hiyo Jijini Seoul Korea Kusini wakati wa ziara ya kikazi ya siku tatu ya Waziri Mahiga nchini humo.

Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa na ujumbe wake kwenye mazungumzo na Bw. Chang Yaong Hun, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Exim ya Korea Kusini. Viongozi hao wawili walikutana kwenye ofisi za Benki hiyo Jijini Seoul Korea Kusini.
Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa na ujumbe wake kwenye mazungumzo na Bw. Jundong Kim, Makamu Mwenyekiti wa Korea Chamber of Commerce and Industries (KCCI).

Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiwa kwenye picha ya pamoja na Bw. Jundong Kim, Makamu Mwenyekiti wa Korea Chamber of Commerce and Industries (KCCI). Mwingine pichani ni Balozi wa Tanzania nchini Jamhuri ya Korea Mheshimiwa Matilda Masuka.

Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akimkabidhi zawadi ya majani ya chain a kahawa za Tanzania Bw. Choi Jong-won, Makamu Mwenyekiti wa Kampuni ya Dong Myeong ya Korea Kusini.
                                                                        
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Augustine Mahiga ameahidi kusimamia uimarishwaji wa uhusiano wa kiuchumi na biashara kati ya Tanzania na Korea Kusini ili wananchi wa pande zote mbili wapate manufaa.

Waziri Mahiga ameyasema hayo alipokuwa anahitimisha ziara yake ya kikazi ya siku tatu ambapo siku ya mwisho aliitumia kikamilifu kukutana na taasisi za umma za biashara na viwanda, Benki ya Exim ya Korea pamoja na makampuni binafsi yanayojipanga kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo nchini Tanzania.

Amesema kuwa miaka 25 ya kwanza ya uhusiano wetu na Jamhuri ya Korea ilijikita kwenye kuweka misingi imara ya uhusiano wa kidiplomasia ambapo nchi zetu zilikuwa zinajiimarisha kama mataifa huru. “Sasa ni wakati wa kushamiri kiuchumi tuone sekta binafsi zinavyoshiriki katika kukuza uchumi, wananchi wa Tanzania waje kwa wingi nchini Korea kujifunza masuala ya teknolojia, uhandisi na hata usanifu na ubunifu. Huu ndio uhusiano wenye tija kwa mataifa yetu”. Mheshimiwa Waziri alisema.

Akizungumza na Bw. Chang Yaong Hun, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Exim ya Korea, Mheshimiwa Mahiga mbali na kuishukuru taasisi hiyo kwa kuendelea kutoa mikopo na misaada nchini Tanzania, Waziri Mahiga alieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli sasa imejikita kwenye mapambano dhidi ya rushwa na ujenzi wa viwanda ili kuleta maendeleo ya kweli kwa wananchi wetu. Kwasasa Benki hiyo inatekeleza miradi ya ujenzi wa miundombinu ya umeme na maji mikoa mbalimbali ya Tanzania ukiwemo Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mahiga alifafanua kuwa ajenda ya Mheshimiwa Magufuli ya viwanda, haiwezi kukamilika bila kuwa na miundombinu ya msingi kama vile uzalishaji wa umeme wa kutosha na ukuaji wa sekta ya uchukuzi na mawasiliano ambapo Korea Kusini ni wabobezi kwenye masuala hayo.

Alitumia fursa hiyo kumkaribisha Bw. Chang na timu yake kwenda Tanzania kufanya tathmini ya miradi tunayoshirikiana nao, lakini pia miradi mipya kwenye sekta ya uchukuzi kama ujenzi wa Standard Railway Gauge “SRG” kutoka Isaka hadi Kigali, n.k. ambayo ni miradi ya kipaumbele kwa sasa kwa taifa letu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Chang alisifu utendaji kazi wa Rais John Pombe Magufuli, na Serikali ya awamu ya tano ya Tanzania na kusema kuwa utendaji kazi wa aina hii ni wa kupigiwa mfano barani Afrika, na umekuja wakati muafaka tunapoingia kwenye hatua nyingine ya uhusiano wa kiuchumi baina ya nchi zetu mbili. Aidha aliongeza kuwa, wakati umefika sasa wa kufanya kazi, nay eye yuko tayari kufanya kazi na Tanzania kwani Serikali yake, imetoa kipaumbele kwa nchi hii.  

Korea Exim Bank ni taasisi ya Serikali inayosimamia mikopo na misaada ya Jamhuri ya Korea inayotoa kwa nchi nyingine. Katika kipindi cha miaka minne (tangu 2016 hadi 2020), Korea Kusini kupitia taasisi hiyo, imeongeza mikopo ya maendeleo kwa bara la Afrika kwa asilimia 20. Uamuzi wa Serikali iliyokuwa madarakani mwaka 2016 wa kuichagua Tanzania kupokea kiasi kikubwa cha msaada huo kuliko nchi nyingine ya Afrika, umeendelezwa na Serikali iliyopo sasa madarakani ya Mheshimiwa Moon Jae-in, Rais wa Jamhuri ya Korea.
Ujumbe wa Mheshimiwa Augustine Mahiga pia ulikutana na kufanya mazungumzo na Bw. Judong Kim, Makamu Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara na Viwanda ya Korea (Korea Chamber of Commerce and Industries KCCI), ambapo Waziri Mahiga aliwasisitiza kuja Dar es salaam kuangalia fursa zilizopo ili kuwashawishi wanachama wao kutafuta bidhaa na masoko nchini Tanzania.

Akielezea umuhimu wa KCCI kuzuru Tanzania na kujifunza soko la biashara, Bw. Edwin Rutageruka Mkurugenzi Mkuu wa TANTRADE aliyeongozana na ujumbe wa Mheshimiwa Waziri Mahiga, alisema njia nzuri ya kupata picha halisi ni kupitia  Maonesho ya Biashara ya Saba Saba. Hivyo alitumia fursa hiyo kualika ujumbe wa KCCI kushiriki kwenye maonesho ya 42 yanayotarajiwa kuanza tarehe 28 Juni – 10 Julai, 2018.

Kabla ya kuhitimisha ziara yake, Mheshimiwa Mahiga pia alikutana na kufanya mazungumzo na watendaji wakuu wa makampuni ya DOHWA, ambao wamejikita kwenye ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya reli n.k. Makampuni mengine ni KORAIL, STX Engine, KTMI & STX Offshore pamoja na GS E&C, ambao wote wameonesha nia ya kuwekeza au kufanya biashara nchini Tanzania. Ujumbe mkuu kwa taasisi na makampuni hayo ulikua ni kupanua fursa za ushirikiano wa biaashara na uwekezaji, ubadilishanaji wa ujuzi na ujengaji uwezo wa wafanyakazi ambao ndio nguvu kazi ya taifa letu.

Pamoja na kuzungumza na makampuni ya umma na sekta binafsi yaliyoorodheshwa hapo juu, ziara ya Mheshimiwa Augustine Mahiga, ilimuwezesha kuwa mgeni rasmi kwenye Kongamano la Kwanza la Biashara kati ya Tanzania na Korea Kusini ambapo alihutubia mamia ya wafanyabiashara wa Korea kuhusu utayari wa Tanzania kushirikiana na nchi hiyo kibiashara.

Mkutano huo uliopewa kauli mbiu ya “Eplore Tanzania” ulifuatiwa na mikutano midogo midogo iliyowakutanisha baadhi ya wafanyabiashara wa Tanzania na Korea Kusini ili kuangalia kwa ukaribu maeneo ya ushirikiano. Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini na mwenzake wa Korea Kusini nchini Tanzania wameazimia kuendeleza makongamano hayo ya kila mwaka ili kuwa na ushirikiano wa karikiano wa karibu wa kibiashara kwa mataifa hayo mawili kwa maendeleo ya wananchi wote.  

Wajumbe wengine walioongozana na Mheshimiwa Waziri Mahiga nao walipata fursa ya kuhutubia hadhara hiyo kuhusu Tanzania ambapo Bw. Geoffrey Mwambe, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Investment Centre alitoa utangulizi kuhusu uwekezaji Tanzania; Kanali (mstaafu) Joseph Simbakalia, Mkurugenzi Mkuu wa EPZA alizungumzia maeneo ya kipaumbele kwenye maeneo maalum ya uwekezaji nchini Tanzania. Naye Bi. Nasriya Nassor, Mkurugenzi wa Biashara wa Taasisi ya Uwekezaji Zanzibar alitoa taarifa fupi kuhusu Zanzibar kama kivutio cha utalii ndani ya Tanzania na eneo linalopendelewa na watalii wengi duniani.

Jamhuri ya Korea, kama inavyojulikana rasmi na Umoja wa Mataifa, ni mojawapo ya nchi zinazofanya vizuri zaidi duniani kiuchumi kwa sasa. Viashiria vya uchumi vinaonyesha uchumi wa nchi hiyo utaendelea kukua kwa viwango kutokana na jitihada za dhati za viongozi wa nchi hiyo za kufuta kabisa umaskini kwa wananchi wao. Kwa sasa wastani wa pato kwa mtu “per capital income” inakadiriwa kuwa zaidi ya US$ 34,000, ukilinganisha na US$ 22,670 mwaka 2012. Baada ya vita ya Korea kwenye miaka ya mwanzo ya 1950, nchi ya Korea Kusini ilikua maskini kuliko nchi nyingi barani Afrika ikiwemo Tanzania ambapo wastani wa pato kwa mtu ilikua na US$67.

Mheshimiwa Mahiga anatarajiwa kurejea nyumbani baada yakuhitimisha ziara hiyo aliyosema italeta faida sio tu kwa wafanyabiashara, ila kwa jamii kwa ujumla. Nchi hii ni tajiri sana kiuchumi; lakini utajiri wake mkubwa pia uko kwenye taaluma ya rasilimali watu, hivyo kwa Tanzania kufanikiwa kufungua ubalozi hapa, sasa tumefungua milango ya ushirikiano wa karibu, kuliko ilivyokuwa mwanzo. Tuchangamke tuige mfano wa uchapa kazi wao, na sisi tutaondoka kwenye umasikini Waziri Mahiga alisema kwa umaliza, kabla ya kuondoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Incheon, uliopo mjini Seoul, Jamhuri ya Korea.

-Mwisho-

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Seoul, Korea Kusini,
3 Februari 2018.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad