HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, February 2, 2018

UJENZI RASMI BOMBA LA MAFUTA KUANZA MEI

Na Veronica Simba – Dodoma
Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Nishati na Kampuni ya Total wamekubaliana kuharakisha hatua zote za awali katika Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima Tanga ili shughuli za ujenzi rasmi zianze mwezi Mei mwaka huu.
Makubaliano hayo yalifikiwa Alhamisi, Februari 1, wakati Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani alipokutana na uongozi wa juu wa kampuni hiyo wizarani Dodoma.
Aidha, makubaliano mengine yaliyofikiwa katika kikao hicho ni kuwa kazi za awali za maandalizi ya ujenzi ziwe zimekamilika ifikapo mwezi Machi mwaka huu.
“Ni lazima tuharakishe mchakato huu kama Mheshimiwa Rais Magufuli alivyoagiza. Hivyo, tumekubaliana kwamba shughuli zote za maandalizi ziwe zimekamilika ifikapo Machi mwaka huu ili kuwezesha shughuli rasmi za ujenzi wa Bomba kuanza mwezi Mei,” alifafanua Waziri Kalemani.
Vilevile, katika kikao hicho, Rais wa Kampuni ya Total sehemu ya Afrika, Guy Maurice ambaye alikuwa kiongozi wa Ujumbe huo, alibainisha nia ya kampuni yake kuwekeza katika shughuli nyingine mbalimbali zinazohusiana na Mradi wa Bomba jambo ambalo alisema litainufaisha zaidi Tanzania. 
Mbali na makubaliano yote yaliyofikiwa, Waziri Kalemani pia alisisitiza kuwa ni muhimu kampuni ya Total iwasilishe Mpango-Kazi wake wizarani mapema iwezekanavyo ili utumike kama mwongozo-rejea katika kutathmini utekelezaji wa Mradi huo mkubwa.
Kampuni ya Total ndiyo mwekezaji katika utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima, Tanga.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Mwinyimvua, Mkurugenzi wa Utawala na Utumishi wa Wizara Lusius Mwenda, Mkurugenzi wa Sera na Mipango Haji Janabi na maafisa wengine waandamizi kutoka wizarani.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (katikati), akiongoza kikao baina ya viongozi na wataalam wa Wizara (kulia) na Ujumbe kutoka Kampuni ya Total (kushoto). Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani, akisalimiana na Ujumbe kutoka Kampuni ya Total kabla ya kuanza kwa kikao baina yao kujadili utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima-Tanga. Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu.
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kushoto), akimsikiliza Rais wa Kampuni ya Total sehemu ya Afrika, Guy Maurice (kulia) wakati wa kikao baina yao kujadili utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima-Tanga. Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt. Hamisi Mwinyimvua, akisalimiana na Ujumbe kutoka Kampuni ya Total kabla ya kuanza kwa kikao baina ya Wizara na Ujumbe kutoka Kampuni hiyo kujadili utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima-Tanga. Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu na kiliongozwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani.
 Viongozi na wataalam wa Wizara ya Nishati, wakiwa katika kikao baina ya Wizara na Ujumbe kutoka Kampuni ya Total kujadili utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima-Tanga. Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu na kiliongozwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani).
Ujumbe kutoka Kampuni ya Total wakiwa katika kikao baina yao na Viongozi na wataalam wa Wizara ya Nishati kujadili utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Hoima-Tanga. Kikao hicho kilifanyika Makao Makuu ya Wizara mjini Dodoma, Februari Mosi, mwaka huu na kiliongozwa na Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (hayupo pichani).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad