HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 20, 2018

PROF. MBARAWA AWATAKA MAKANDARASI WAZAWA KUKAMILISHA MIRADI YA UJENZI KWA WAKATI

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, amewataka makandarasi wazawa wa kampuni ya Samota, Anam na Jossam JV wanaojenga barabara ya Urambo-Kaliua yenye urefu wa KM 28 kwa kiwango cha lami wahakikishe wanakamilisha ujenzi wa barabara hiyo kwa muda uliowekwa.

Prof. Mbarawa ametoa agizo hilo katika kijiji cha Motomoto, Wilaya ya Urambo mkoani Tabora alipokuwa katika ziara yake ya kikazi ya kukagua mtandao wa barabara mkoani humo na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi wa barabara hiyo.

“Nataka nione kazi za ujenzi zinafanyika kwa haraka, kwani uzoefu unaonesha baadhi ya makandarasi wazawa wamekuwa na kasi ndogo, hivyo mjipange vizuri ili barabara ikamilike kwa wakati”, amesema Prof. Mbarawa.

Amesema kuwa nia ya Serikali ni kuwajengea makandarasi wazawa uwezo ili waweze kutekeleza miradi mikubwa mingine ya ujenzi hapa nchini lakini haitasita kuwanyima kazi hizo kama miradi hiyo itacheleweshwa, haitakidhi viwango vinavyohitajika na kama hawataonekana eneo la kazi kwa kipindi kirefu.

“Mkandarasi mzawa atakayechelewesha mradi wowote wa ujenzi hatapewa kazi nyingine kwa sababu atakuwa amechelewesha maendeleo ya wananchi”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Ameongeza kuwa Serikali imejipanga kuwalipa makandarasi wazawa kwa wakati ili waweze kutekeleza miradi yao kwa ufanisi.

Naye Mbunge wa jimbo la Urambo, Magreth Sitta, amemueleza Waziri Prof. Mbarawa kuwa ujenzi wa barabara hiyo ni muhimu kwa wananchi wa wilaya yake na Kaliua na hata mikoa jirani kwani usafirishaji wa mazao na abiria utarahisishwa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Urambo, Angelina Kwingwa amesema wamejipanga vyema kutoa ushirikiano kwa wakandarasi wazawa hao, na kuahidi kumsimamia ili amalize kazi hiyo kwa wakati, lakini kwa kiwango.

Awali akitoa maelezo ya mradi wa ujenzi wa barabara hiyo, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani humo Mhandisi Damian Ndibalinze, amesema mkandarasi ameshapewa fedha za mradi hivyo hakuna sababu ya kuchelewesha mradi huo na kuahidi kuwasimamia ili wakamilishe kabla ya mwaka 2020.

Ameongeza kuwa ujenzi wa barabara hiyo utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 37.6 na zote zikiwa zinafadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia 100.

Katika hatua nyingine, Waziri Prof. Mbarawa amekagua ujenzi wa barabara ya Tabora-Pangale yenye urefu wa KM 30 inayojegwa na mkandarasi CICO kwa gharama ya shilingi bilioni 28.6 na kumtaka mkandarasi huyo kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo ifikapo mwishoni mwa mwezi wa sita. 

Waziri Prof. Mbarawa yuko mkoani Tabora kwa ziara ya siku mbili akiwa na lengo la kukagua utekelezaji wa miundombinu ya barabara, mkoani humo

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akimsikiliza kwa makini Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri (kushoto), alipomtembelea ofisini kwake katika ziara yake ya kikazi mkoani humo kwa lengo la kukagua miradi ya ujenzi ya barabara iliyokamilika na inayoendelea. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Queen Mlozi.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akizungumza na uongozi wa Wilaya ya Urambo, alipokutana nao katika ziara yake ya kikazi ya kukagua mradi wa ujenzi wa barabara ya Urambo-Kaliua yenye urefu wa KM 28 inayojengwa kwa kiwango cha lami, mkoani Tabora.
 Mbunge wa jimbo la Urambo, Mhe. Magreth Sitta, akimshukuru Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (kulia), kwa kufuatilia maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Urambo-Kaliua yenye urefu wa KM 28 inayojengwa kwa kiwago cha lami, mkoani Tabora.
 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani), kuhusu hatua za mradi wa ujenzi wa barabara ya Urambo-Kaliua yenye urefu wa KM 28 na kusisitiza nia ya Serikali ya kuwajengea uwezo wakandarasi wazawa ili waweze kutekeleza miradi ya ujenzi hapa nchini.
 Mbunge wa jimbo la Urambo, Mhe. Magreth Sitta, akiagana na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, mara baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Urambo-Kaliua yenye urefu wa KM 28 kwa kiwango cha lami, mkoani Tabora.
 Muonekano wa Daraja la Kasisi lenye urefu wa mita 54 lililopo katika barabara ya Tabora-Pangale yenye urefu wa KM 30. Ujenzi wa barabara hiyo umefikiwa asilimia 80 na inajengwa na mkandarasi CICO kwa gharama ya shilingi bilioni 28.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri, na uongozi wa wilaya ya Tabora wakipita juu ya daraja la Wala lenye urefu wa mita 34 katika barabara ya Tabora-Pangale yenye urefu wa KM 30, katika ukaguzi wa ujenzi wa barabara hiyo, mkoani humo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad